DSC03246
Picha juu na chini ni Baadhi ya wananchama wa klabu ya waandishi wa habari (Singpress) mkoa wa Singida wakijifunza uandishi wa habari kupitia mtandao. Mafunzo hayo ya siku nne yamefanyikia katika ukumbi wa mikutano wa ofisi ya mkuu wa wilaya Iramba. Mwenye fulana ya misitari ni mkufunzi wa mafunzo hayo ya uandishi kupitia mtandao (on line journalism),John Mnubi akiwaelekeza wanachama wa Singpress namna ya kufungua blog.(Picha na Nathaniel Limu).

DSC03250
Na Nathaniel Limu, Kiomboi
Wanachama wa Klabu ya Waandishi wa Habari (Singpress) Mkoa wa Singida, wametahadharishwa na vitendo vya ngono zembe vinavyochochea maambukizi mapya ya virusi  Ukimwi kwa madai kwamba baadhi ya wanawake wa mjini Kiomboi Wilaya ya Iramba hawajui kusema ‘hapana’ pindi wanapoombwa kuwa na mahusiano ya kimapenzi.
Mwenyekiti wa Singpress,Seif Takaza ambaye ni mkazi wa mjini New Kiomboi,ametoa tahadhari hiyo wakati akiwakaribisha wanachama 15 wa Singpress wanaohudhuria mafunzo ya siku nne ya uandishi bora wa habari kupitia mtandao (on line Journalism).
Mafunzo hayo yanayosimamiwa na Mwezeshaji John Mnubi kutoka mkoa wa Iringa,yanaendelea kwenye ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Iramba mkoani  Singida.
Akifafanua,Takaza alisema baadhi ya wanawake na wasichana wa mjini hapa,wana tabia ya kuchangamkia wageni hususani wanaokuja kuhudhuria mikutano na semina mbalimbali kwa madai kwamba wanakuwa na fedha za kutosha.
“Mimi niwatahadharishe tu wanachama wenzangu kwamba muwe waaangalifu na wala msiponzwe na upatikanaji rahisi wa akina ‘dada poa’ hao.Tambueni kwamba UKIMWI upo na bado hauna chanjo wala tiba hadi dakika hii”,alisema Takaza.
Kwa upande wake Mwezeshaji Mnubi,ameishauri serikali kuhakikisha mkogo wa mawasiliano taifa unapatikana katika sehemu zote za nchi,ili kusaidia kupatikana kwa urahisi mitando ya intaneti.
“Kwa sasa sehemu nyingi nchini hazina huduma ya mitandao ya intaneti na kama ipo,inapatikana kwa shida kubwa.Mitandao hiyo ikipatikana kupitia mitandao ya intaneti, itasaidia wananchi wakiwemo wakulima kupata taarifa mbalimbali pamoja na kujielimisha kwa ajili ya maendeleo yao”,alisema Mnubi.
Baadhi ya wanachama wa Singpress,wamedai kuwa pamoja na kupata mafunzo juu ya matumizi ya mitandao katika kutoa taarifa mbalimbali,elimu hiyo waliyopata haitawasaidia katika majukumu yao kwa madai kuwa huduma ya intaneti ni shida kupatikana.