Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

Dk Mwakyembe aanza kuwang’oa vigogo wa Kampuni ya Reli TRL kwa ununuzi wa mabehewa 25 mabovu huku kutengenezwa kimyakimya

Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe.
Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe ameagiza kung’olewa kwa baadhi ya vigogo wa Kampuni ya Reli Tanzania (TRL) ambao wanatuhumiwa kuhusika katika mchakato wa ununuzi wa mabehewa ya kusafirisha kokoto kutoka India, ambayo yalibainika kuwa mabovu.
Mabehewa hayo ni kati ya 25 aina ya Ballist Hopper Bogie (BHB) yaliyoingizwa nchini Julai 24 yakiwa yamegharimu kiasi cha Sh4 bilioni na 20 yalibainika kuwa ni mabovu na kulazimika kuanza kutengenezwa kwa kificho.
Mkataba wa kununua mabehewa hayo ulisainiwa Machi 21, 2013 kati ya TRL na Kampuni ya Hindusthan Engineering and Industries ya India.
Jana, Dk Mwakyembe aliiagiza Bodi ya Wakurugenzi ya TRL kuwasimamisha kazi mara moja kupisha uchunguzi, wahandisi wote waliokwenda India kwa ajili ya kufanya uhakiki wa ubora wa mabehewa hayo.
Alitoa maagizo hayo mbele ya Menejimenti ya TRL na wafanyakazi wa kampuni hiyo, katika kikao cha kuhitimisha mchakato wa kushughulikia malalamiko ya watumishi ambao wamekuwa wakidai malipo ya kima cha chini cha mshahara cha Sh300,000.
“Natoa siku 10 Bodi ya Wakurugenzi iwe imenipa majibu ya mchakato mzima wa ununuzi wa mabehewa 25 ya kokoto ulivyofanywa. Nataka uchunguzi ufanyike lakini wale wote waliokwenda India mara mbili kwa ajili ya kuthibitisha ubora wa mabehewa hayo wasimamishwe kazi mpaka taarifa za wasio na hatia zitakapobainika,” alisema.
Aliagiza kusimamishwa kazi kwa Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TRL na kuondolewa katika nafasi yake, mkuu wa idara ya fedha pamoja na kuvunjwa kwa bodi ya zabuni ya kampuni hiyo na kusitishwa kwa mikataba yote iliyopo kati kampuni hiyo na wazabuni.
Mikataba aliyoagiza kusitishwa ni pamoja na ule wa TRL na Kampuni ya Transroads inayoshughulikia upakiaji wa mizigo na kampuni ya R&A inayotekeleza ukarabati wa reli pamoja na urekebishaji wa mfumo wa mawasiliano huku akitaka kuondolewa kwa mzabuni anayehudumu katika Shule ya Msingi Itigi.
“Nataka bodi iende Itigi na iniambie imemchukulia hatua gani msimamizi wa mradi huu ambao mkataba wake unaonyesha kuwa chakula kinatolewa shuleni hapo lakini si kweli. Huwa naongea nikiwa natabasamu lakini ikibidi nitaiondoa bodi hii. Kuna Watanzania wengi wanaweza kufanya kazi hii, kama kuna mtu anaona hawezi basi aache mara moja.”
Alisema ripoti aliyonayo inaonyesha kuwa kati ya vitanda 320 vinavyoelezwa kuwapo katika shule hiyo, 260 ni vibovu huku magodoro yakiwa hayafai kwa matumizi ya binadamu.
Mgomo
Wafanyakazi wa TRL chini ya chama chao (Trawu) walianza mgomo wa kutaka majibu juu ya ongezeko la mishahara yao pamoja na malipo ya malimbikizo ya kati ya Julai na Oktoba mwaka huu na baada ya kutoelewana na uongozi, walilifikisha suala hilo wizarani.
Waziri Mwakyembe aliunda kamati ya uchunguzi iliyofanya kazi kwa wiki tatu ambayo ilikabidhiwa kwake Jumatatu iliyopita.
Taarifa za awali zilionyesha kuwa ili kufanikisha madai ya mishahara hiyo zilikuwa zinahitajika Sh400 milioni lakini baada ya uchambuzi imebainika kuwa kiasi cha fedha kinachotakiwa ni Sh120 milioni.
“Nimesikia mkuu wa idara ya fedha (Jasper Kisiraga) hajawaingizia mishahara yenu kwa madai kwamba ana hasira baada ya ninyi kufikisha malalamiko yenu kwangu. Naiagiza bodi kumwondoa mara moja katika nafasi hiyo,” alisema Dk Mwakyembe na kuongeza:
“Nafasi yake ichukuliwe na kijana aliyekuwemo katika kamati ya uchunguzi (Mbaraka Mchopa). Nadhani bodi haitaniangusha kumthibitisha kijana huyu ambaye ameonyesha nia ya dhati ya kushughulikia matatizo ya kampuni.”
Alimwagiza Mchopa kuhakikisha kuwa madereva wote wanalipwa posho wanazostahili kwa wakati na yeyote atakayeonyesha jitihada kwa kufanya kazi ya ziada yenye mchango kwa maendeleo ya kampuni.
Pia Dk Mwakyembe alitangaza kusitisha mikataba yote kati ya TRL na kampuni tatu za ulinzi akisema hazina uwezo wala nyenzo... “Zinalinda mali ya mabilioni ya shilingi kwa manati, hazina silaha yoyote kukabiliana na chochote kinachoweza kutokea. Mikataba yote ivunjwe mara moja na uanzishwe utaratibu wa kuajiri askari wetu kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi.”
Alimtambulisha kamanda mpya wa polisi (kikosi cha reli), Simon Chillery, akimtaka kuhakikisha magenge ya wahalifu katika baadhi ya maeneo kama Nguruka, Kigoma na Mabamba, Tabora yanaondolewa mara moja.
“Huyu jamaa ni msomi. Ni mhandisi kwa taaluma, nataka ukisuke kikosi chako kwa namna itakayoonyesha tofauti kati ya kamanda msomi na ambaye hajaenda shule, ukishindwa mimi mwenyewe nitakushtaki kwa IGP,” alisema.
Mwakyembe alisema Serikali imegundua uwepo udanganyifu unaofanywa na baadhi ya wafanyakazi. “Nitakuja tena wiki ijayo kuwafukuza kazi baadhi yenu kutokana na wizi wa mafuta pamoja na udanganyifu wa upakiaji wa mizigo walioufanya. Nasikia kati yao wengine wanaendesha biashara ya daladala, nitazifuatilia na zikikamatwa zitataifishwa.”
Mabehewa mapya
Mapema jana asubuhi, Waziri Mkuu Mizengo Pinda alitembelea Bandari ya Dar es Salaam na kukagua mabehewa 72 yakiwamo 22 ya abiria na 50 ya mizigo ambayo yameingizwa nchini kwa ajili ya kuimarisha usafirishaji katika reli ya kati.
“Hii ni moja juhudi za Serikali kuboresha miundombinu ya usafiri nchini na changamoto iliyopo ni kufikia viwango vya kimataifa. Kama nchi nyingine wana treni za umeme sisi kinatushinda nini kufika huko? Nikutie moyo waziri na tuendelee kushirikiana katika hili… nitajitahidi kushughulikia masuala yote yahusuyo fedha,” alisema Pinda.
chanzo: gazeti la mwananchi
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top