Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

Slaa akosoa uteuzi wakuu wa mkoa

 Dk Willbrod Slaa 
Mabadiliko ya wakuu wa mikoa yaliyotangazwa juzi na Rais Jakaya Kikwete yametajwa kuwa na malengo ya kisiasa, huku Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willbrod Slaa akikosoa kitendo cha kuhamishwa vituo vya kazi wakuu hao sita ndani ya mwezi mmoja, kwamba ni gharama kwa Serikali.
Wakizungumza na gazeti hili wasomi nchini wamesema mabadiliko ya wakuu hao huwa na sababu nyingi, lakini sababu ambayo haielezwi huwa ni ile ya kisiasa.
Katika mabadiliko hayo Rais Kikwete alimpandisha cheo Mkuu wa Wilaya ya Karatu, Daudi Ntibenda kuwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha na kuwahamisha vituo vya kazi wakuu wengine sita wa mikoa kuanzia juzi. Ntibenda aliapishwa jana Ikulu na Rais Kikwete.
Uhamisho huo umekuja ikiwa ni mwezi mmoja kamili tangu Rais Kikwete alipofanya uteuzi wa wakuu wapya wanne wa mikoa na kuwahamisha sita, huku wengine watatu wakipangiwa kazi nyingine.
Wakuu wa mikoa wanne wapya ni Dk Ibrahim Msengi (Katavi), Amina Masenza (Iringa), Halima Dendego (Mtwara) na John Mongella (Kagera).
Akizungumza na gazeti hili Dk Slaa alisema, “Mabadiliko haya ni viashiria vya Serikali kuchoka na kutokuwa na uhakika kama itabakia madarakani baada ya Uchaguzi Mkuu 2015. Ndiyo maana wanawahamisha ili kuona nani atafaa wapi na kwa malengo gani.”
Alisema kumhamisha mkuu wa mkoa ndani ya mwezi mmoja ni gharama zisizo na msingi, “Hizi gharama zote za nini? Hivi hawazioni, iweje katika kipindi hiki kifupi wafanye mabadiliko haya?
“Katika kipindi hiki ambacho nchi inahitaji fedha kwa ajili ya shughuli nyingi za maendeleo, yanapofanyika mabadiliko kama haya lazima ujiulize kipaumbele cha Serikali ni nini,” alisema.
Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Ruaha, Profesa Gaudence Mpangala alisema: “Binafsi naona mabadiliko haya yanalenga uchaguzi mkuu maana kila unapokaribia huwa yanafanyika.”
Mhadhiri Mwandamizi wa Sayansi ya Siasa, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Alexander Makulilo alisema: “Suala la gharama haliepukiki. Sababu za kuhamisha wakuu wa mikoa ni nyingi ila kubwa ni changamoto za mkoa husika au kupwaya katika utendaji.”
Hata hivyo, Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue amesema mabadiliko hayo ni ya kawaida na yametokana na kupewa likizo ya ugonjwa kwa aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Paschal Mabiti ambaye nafasi yake imechukuliwa na Elaston Mbwilo aliyetoka Manyara.
“Kunapokuwa na tatizo kama hilo ni lazima Rais ateue watu wengine. Rais anapoteua anatazama hata changamoto za mkoa husika na uteuzi unazingatia zaidi utendaji si masuala ya kisiasa. Baadaye utafanyika uteuzi wa wakuu wa wilaya,” alisema.
Katika uteuzi huo wa juzi, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Joel Bendera anahamia Manyara kutoka Morogoro na nafasi yake inachukuliwa na Dk Rajabu Rutengwe kutoka Tanga alikokaa kwa mwezi mmoja akitokea Katavi.
Magalula Magalula amehamishiwa Tanga kutoka Lindi ambako naye alikaa kwa mwezi mmoja akitokea Geita na nafasi yake inazibwa na Mwantumu Mahiza kutoka Pwani. Mhandisi Evarist Ndiliko amehamishiwa Mkoa wa Pwani kutoka Arusha alikohamia hivi karibuni akitokea Mwanza. Walioachwa kwa ajili ya kazi nyingine ni Dk Christine Ishengoma (Iringa), Kanali Fabian Massawe (Kagera) na Kanali Joseph Simbakalia.
.aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, ambaye tayari ameteuliwa kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maeneo Maalumu ya Uwekezaji kwa Mauzo ya Nje (EPZA).
Akizungumza Ikulu jana mara baada ya kuapishwa, Ntibenda alisema, “Siendi Arusha kupambana na vurugu, ninakwenda kusimamia masuala ya maendeleo.”
Alisema changamoto zinazoukabili mkoa huo ni migogoro ya ardhi na kusisitiza kuwa ataitatua migogoro hiyo kwa kushirikiana na wananchi pamoja na wakuu wa mikoa.
chanzo: gazeti mwananchi
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top