Wakizungumza
na gazeti hili wasomi nchini wamesema mabadiliko ya wakuu hao huwa na
sababu nyingi, lakini sababu ambayo haielezwi huwa ni ile ya kisiasa.
Katika
mabadiliko hayo Rais Kikwete alimpandisha cheo Mkuu wa Wilaya ya
Karatu, Daudi Ntibenda kuwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha na kuwahamisha vituo
vya kazi wakuu wengine sita wa mikoa kuanzia juzi. Ntibenda aliapishwa
jana Ikulu na Rais Kikwete.
Uhamisho
huo umekuja ikiwa ni mwezi mmoja kamili tangu Rais Kikwete alipofanya
uteuzi wa wakuu wapya wanne wa mikoa na kuwahamisha sita, huku wengine
watatu wakipangiwa kazi nyingine.
Wakuu
wa mikoa wanne wapya ni Dk Ibrahim Msengi (Katavi), Amina Masenza
(Iringa), Halima Dendego (Mtwara) na John Mongella (Kagera).
Akizungumza
na gazeti hili Dk Slaa alisema, “Mabadiliko haya ni viashiria vya
Serikali kuchoka na kutokuwa na uhakika kama itabakia madarakani baada
ya Uchaguzi Mkuu 2015. Ndiyo maana wanawahamisha ili kuona nani atafaa
wapi na kwa malengo gani.”
Alisema
kumhamisha mkuu wa mkoa ndani ya mwezi mmoja ni gharama zisizo na
msingi, “Hizi gharama zote za nini? Hivi hawazioni, iweje katika kipindi
hiki kifupi wafanye mabadiliko haya?
“Katika
kipindi hiki ambacho nchi inahitaji fedha kwa ajili ya shughuli nyingi
za maendeleo, yanapofanyika mabadiliko kama haya lazima ujiulize
kipaumbele cha Serikali ni nini,” alisema.
Mhadhiri
Mwandamizi wa Chuo Kikuu Ruaha, Profesa Gaudence Mpangala alisema:
“Binafsi naona mabadiliko haya yanalenga uchaguzi mkuu maana kila
unapokaribia huwa yanafanyika.”
Mhadhiri
Mwandamizi wa Sayansi ya Siasa, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk
Alexander Makulilo alisema: “Suala la gharama haliepukiki. Sababu za
kuhamisha wakuu wa mikoa ni nyingi ila kubwa ni changamoto za mkoa
husika au kupwaya katika utendaji.”
Hata
hivyo, Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue amesema mabadiliko hayo
ni ya kawaida na yametokana na kupewa likizo ya ugonjwa kwa aliyekuwa
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Paschal Mabiti ambaye nafasi yake imechukuliwa
na Elaston Mbwilo aliyetoka Manyara.
“Kunapokuwa
na tatizo kama hilo ni lazima Rais ateue watu wengine. Rais anapoteua
anatazama hata changamoto za mkoa husika na uteuzi unazingatia zaidi
utendaji si masuala ya kisiasa. Baadaye utafanyika uteuzi wa wakuu wa
wilaya,” alisema.
Katika
uteuzi huo wa juzi, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Joel Bendera anahamia
Manyara kutoka Morogoro na nafasi yake inachukuliwa na Dk Rajabu
Rutengwe kutoka Tanga alikokaa kwa mwezi mmoja akitokea Katavi.
Magalula
Magalula amehamishiwa Tanga kutoka Lindi ambako naye alikaa kwa mwezi
mmoja akitokea Geita na nafasi yake inazibwa na Mwantumu Mahiza kutoka
Pwani. Mhandisi Evarist Ndiliko amehamishiwa Mkoa wa Pwani kutoka Arusha
alikohamia hivi karibuni akitokea Mwanza. Walioachwa kwa ajili ya kazi
nyingine ni Dk Christine Ishengoma (Iringa), Kanali Fabian Massawe
(Kagera) na Kanali Joseph Simbakalia.
.aliyekuwa
Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, ambaye tayari ameteuliwa kuwa Mkurugenzi
Mtendaji wa Mamlaka ya Maeneo Maalumu ya Uwekezaji kwa Mauzo ya Nje
(EPZA).
Akizungumza
Ikulu jana mara baada ya kuapishwa, Ntibenda alisema, “Siendi Arusha
kupambana na vurugu, ninakwenda kusimamia masuala ya maendeleo.”
Alisema
changamoto zinazoukabili mkoa huo ni migogoro ya ardhi na kusisitiza
kuwa ataitatua migogoro hiyo kwa kushirikiana na wananchi pamoja na
wakuu wa mikoa.
chanzo: gazeti mwananchi
Post a Comment