Dar es
Salaam. Watu watano wamefariki dunia kutokana na mvua zinazoendelea
kunyesha jijini Dar es Salaam, watatu kati yaowakiwamo wanafunzi wawili,
wakipoteza maisha baada ya kibanda walichojihifadhi kujikinga na mvua
kuangukiwa na nguzo ya umeme na kuwaunguza.
Kaimu
Kamanda wa Polisi Mkoa wa kipolisi wa Temeke, Zakaria Sebastian alisema
vifo vya watu hao watatu vilitokea katika eneo la Mchikichini
Kimbangulile, Mbagala.
Sebastian
aliwataja waliokufa kuwa ni Ramadhan Said (10), mwanafunzi wa darasa la
nne Shule ya Msingi Mchikichini, Alhaji Jumanne (15), mwanafunzi wa
kidato cha kwanza Shule ya Sekondari ya Charambe na Monica Elistone
(26).
Alisema
wakati mvua ikiendelea kunyesha, watu hao walijihifadhi kwenye kibanda
kilichotengenezwa kwa mabati na ghafla waya wa nguzo hiyo ulikatika na
kuangukia kibanda hicho na kushika moto.
“Wakiwa
kwenye banda hilo, ghafla nguzo ilianguka na waya wake kuangukia kibanda
kilichoshika moto na kuwateketeza watu hao,” alisema Kamanda
Sebastian.
Mjumbe wa
shina namba nne wa mtaa huo, Kondo Namna alisema zaidi ya nguzo saba
zimeinamia kwenye nyumba za watu na wameshatoa taarifa Tanesco, lakini
hadi jana, hakuna hatua zozote zilizochukuliwa na shirika hilo.
Wakati
huohuo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camillius Wambura alisema
wakati mvua zinaendelea kunyesha saa sita usiku wa kuamkia jana, mkazi
wa Mwananyamala Edward Warioba (22) alifariki dunia baada ya kuangukiwa
na ukuta akiwa amelala nyumbani kwake.
Katika
tukio jingine, Kamanda Wambura alisema maiti ya mwanamume mwenye umri wa
kati ya miaka 45 na 50 iliokotwa ikielea kwenye makutano ya Mto Goba na
Makongo. Alisema huenda mtu huyo alisombwa na maji ya mvua katika eneo
ambalo bado halijajulikana. Wakati maafa hayo yakitokea, Mamlaka ya Hali
ya Hewa Tanzania (TMA), imetoa tahadhari ya kuwapo kwa mvua kubwa
katika maeneo ya ukanda wa Pwani na kuwataka wakazi wa maeneo hayo kuwa
makini.
Mikoa ambayo huenda ikapata mvua kubwa kwa mujibu wa TMA ni pamoja na Lindi, Mtwara, Tanga na Dar es Salaam.
Mamlaka hiyo ilieleza kuwa kutakuwa na mvua inayozidi milimita 50 ndani ya saa 24 kuanzia jana.
Sababu kubwa ya kuongezeka kwa mvua hizo kunatokana na kuimarika kwa ukanda wa mvua katika maeneo hayo.
Post a Comment