Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

MADAWATI KUFYEKA WAKUU WA WILAYA NA MIKOA

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), George Simbachawene amesema kipimo cha wakuu wa mikoa na wilaya itakuwa ni utekelezaji wa agizo la kuhakikisha hakuna mwanafunzi atakayekaa chini kwa uhaba wa madawati. 

Rais John Magufuli aliwaagiza wakuu wa mikoa wakati akiwaapisha Ikulu, jijini Dar es Salaam, kuhakikisha shughuli ya madawati inakamilika ifikapo Juni 30.

Tangu kutolewa kwa agizo hilo wakuu wa mikoa na wilaya wamekuwa wakihangaika kulitekeleza huku wengine wakilazimika kuitisha harambee ili kuomba wananchi wachangie.

Akizungumza baada ya kufungua mdahalo ulioandaliwa na Taasisi ya Uongozi kuhusu namna ya kuweka mahusiano mazuri baina ya wawekezaji na wananchi ili kupunguza migogoro ya ardhi, Simbachawene alisema kila DC na RC ajipime kwa utekelezaji wa agizo hilo.

“Mkuu wa mkoa au wilaya asiyetimiza agizo la kuhakikisha wanafunzi wote wanakaa kwenye madawati hatoshi, hivyo wanapaswa kujitafakari na kutumia siku zilizobaki kuhakikisha wanatekeleza,” alisema.

Alisema zipo wilaya zilizofanikiwa kutekeleza agizo hilo huku baadhi ya mikoa ikifikisha asilimia 80 na mingine ikiwa bado kwenye hatua za mwanzo.

Simbachawene alisema Serikali imeruhusu raslimali za misitu kutumika kwa jili ya kutekeleza agizo hilo na baadhi ya vibali vimeshatolewa kwa ajili ya uvunaji wa misitu. 

“Nitashangaa kama kutakuwa na mkoa bado unasuasua wakati Serikali imesharuhusu raslimali zilizopo zitumike kwa ajili ya kutengenezea madawati,”alisema.

Aliongeza kuwa wanatarajia kutoa tathmini ya hali ya madawati nchi nzima, mwishoni mwa mwezi huu baada ya agizo hilo kufikia ukomo wake.

Hata hivyo, alisema Rais Magufuli ndiye atakayetoa agizo la mwisho kwa wale watakaoshindwa kufikisha adhma hiyo.

Kuhusu wawekezaji Simbachawene alisema wawekezaji wanalazimika kutengeneza uhusiano mzuri baina yao na wananchi ili kuepuka migogoro.

Alisema Serikali haitahusika iwapo wananchi watakataa ardhi yao isiwekezwe licha ya kuwapo kwa mikataba na sheria zilizowaruhusu kuwekeza.

“Hata kama kuna mikataba na sheria inawaruhusu wawekezaji hawa bado wananchi lazima washirikishwe ili nao watoe kibali cha kazi hiyo kufanyika. Unadhani wakiandamana kwa mabango kuzuia eneo lao lisitumike kwa kutoona faida nini kitafanyika?Jamii ina umuhimu mkubwa kwenye suala hili,”alisema.

Aliwataka wawekezaji hususani kwenye sekta ya madini na kilimo, kuwashirikisha wananchi ili waridhike juu ya uvunaji wa raslimali zao jambo ambalo litawaondolea vikwazo.

Hata hivyo alisisitiza kuwa Serikali inaendelea kupitia mikataba ya madini ili kuhakikisha kuwa inawanufaisha wananchi kwenye maeneo husika.

“Kitu pekee ambacho huwa kinawaudhi wananchi ni pale wanapoona raslimali zao haziwanufaishi, na hata hao wawekezaji wakiondoka huwa wanaacha uharibifu mkubwa wa mazingira, ndiyo maana Serikali tunalazimika kuwataka wawekezaji kuhakikisha uhusiano baina yao na wananchi unaimarika,” alisema.

Mtafiti wa Taasisi ya Uongozi, Dk Godfrey Nyamrunda alisema mdahalo huo umeandaliwa ili kuongeza uelewa baina ya wawekezaji, Serikali na wananchi kuhusu uwekezaji.

Mtafiti Mkuu wa taasisi hiyo, Dennis Rweyemamu alisema migogoro ya ardhi isipodhibitiwa inaathiri uwekezaji na hivyo kupunguza pato la taifa.
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top