Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

Muafaka wa mtoto aliyerudishwa Tanzania Baada ya Wazazi wake Kukamatwa na Madawa ya Kulevya China

Hatimaye  pande mbili za familia ya mtoto ambaye wazazi wake walikamatwa na dawa za kulevya hivi karibuni nchini China, zimekubaliana alelewe na upande wa bibi mzaa mama yake.

Familia hizo zilikutana jana kwenye ofisi za Ustawi wa Jamii Makao Makuu jijini Dar es Salaam na kufanya mazungumzo yaliyofikia mwafaka huo.

Wazazi hao, Baraka Malali na Ashura Mussa, walikamatwa Januari 19 mwaka huu kwenye uwanja wa ndege wa Baiyun, Guangzhou nchini China wakiwa wamemeza pipi 129 za dawa za kulevya.

Mtoto huyo alirejeshwa nchini Alhamisi iliyopita katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), majira ya saa 7:42 mchana akiwa ameambatana na Ofisa wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Akizungumzia uamuzi uliofikiwa kuhusiana na familia ambayo itamchukua mtoto huyo, Kamishna wa Sheria wa Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA), Edwin Kakolaki, alisema familia hizo zilikubaliana mtoto alelewe na upande wa bibi mzaa mama ingawa watashirikiana katika matunzo yake.

“Upande wa mama yake mzazi ndiko atakakolelewa kwa sababu alishawahi kukaa huko kwa muda kwa hiyo upande wa baba yake wameridhia mtoto aendelee kukaa huko.

Lakini makubaliano ni kwamba mtoto ni wa familia zote mbili na wataendelea kumlea kwa pamoja,” alisema.

”Hayo ndiyo waliyokubaliana kwa pamoja hapakuwa na ubishani na sisi tulikuwa tunashuhudia makubaliano yao.”

Wazazi hao baada ya kukamatwa Januari 19, mwaka huu, walipimwa na kubainika kuwa wamemeza dawa za kulevya na kuwekwa katika chumba maalumu. Malali alitoa pipi 47 na Ashura alitoa pipi 82.

Wakati wazazi hao wakiwa mahabusu, serikali ya China iliwasiliana na Tanzania na kufanya utaratibu wa kumrudisha mtoto nchini huku wazazi hao wakisubiri hatima yao mahakamani.

Watu wanaopatikana na hatia ya kusafirisha dawa za kulevya nchini China huhukumiwa adhabu ya kunyongwa.

Kwa Tanzania hufungwa kifungo cha maisha kwa yeyote atakayekamatwa na ‘unga’ kuanzia gramu 20.

Kakolaki alisema bado hawajajua mzigo wa dawa za kulevya walikozichukulia kwa sababu safari yao ya kwenda China waliianzia Zanzibar.

“Walianzia safari yao Zanzibar na baadaye walikwenda hadi Nairobi wakatoka hapo na kuanza safari yao moja kwa moja hadi Guangzhou, China. Sasa kujua mzigo walichukulia wapi bado hatujajua, lakini si kwamba walipita katika uwanja wetu wa Dar es Salaam,” alisema Kakolaki.
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top