Monduli. Waziri mkuu wa zamani, Edward Lowassa
ameipa wiki moja Halmashauri ya Wilaya ya Monduli kuzipatia ardhi kaya
63 za Kijiji cha Nanja, ambazo zimetakiwa kupisha eneo la Jeshi la
Wananchi wa Tanzania (JWTZ) wilayani hapa.
Akizungumza katika uzinduzi wa Bwawa la Migwara
lililojengwa upya na kampuni ya Ms Meero Contractors kwa thamani ya
Sh870.1 milioni. Lowassa ambaye ni mbunge wa jimbo hilo, alisema
wananchi hao wanapaswa kuhamishiwa katika shamba lililokuwa la mwekezaji
la Oguru ambalo sasa linamilikiwa na halmashauri.
Alisema sambamba na mifugo yao, wanapaswa kuhamia
katika eneo hilo kabla ya mwezi huu, kwani tayari Halmashauri ya Monduli
ilishafanya uamuzi wa kuwapa ardhi hiyo zaidi ya miaka miwili
iliyopita, lakini suala hilo halijatekelezwa.
“Halmashauri ya Monduli ina madiwani wengi vijana,
lakini cha ajabu wanafanya kazi taratibu kama konokono. Tukifanya
uamuzi inachukua muda mrefu kutekelezwa, tulishaamua Shamba la Oguru
litakaliwa na familia 63 za Nanja na mifugo yao,” alisema Lowassa.
Alisema wakati halmashauri hiyo ikiwa inatekeleza
mpango wa kuwanyang’anya wawekezaji mashamba 43 waliyoyatelekeza, yale
ambayo tayari yapo mikononi mwa halmashauri wayagawe kwa wananchi.
Post a Comment