Tanga. Mbunge wa Tanga Mjini, Omari Nundu amesema kuna hatari ya
viwanda vingi vya sasa kushindwa kujiendeshakama Serikali itaendelea
kutoza utitiri wa kodi na ushuru.
Amesema kwa uzoefu wake, nchi nyingi zenye zina
nia ya dhati ya kuendelea kuwalea wafanyabiashara na wenye viwanda
wazalendo zinawatoza kodi watu hao wakati viwanda vyao vinapofikia hatua
ya kujiendesha.
Alieleza wasiwasi wake huo alipotembelea kiwanda
cha maji ya chupa cha Al Hayaa cha jijini Tanga na kupokea malalamiko
kutoka kwa Mkurugenzi, Said Mbarouk kwamba ingawa kiwanda ni kichanga,
lakini kinatozwa kodi nyingi.
Nundu ambaye kabla ya kuwa mbunge alikuwa akiishi
Ulaya kwa miaka mingi alisema, hajawahi kuona katika nchi yoyote duniani
ikiwatoza wafanyabiashara wake kodi ya mauzo na siyo faida.
“Tangu Julai 7 mwaka huu, nipo katika ziara ya
kutembelea viwanda vya Tanga, nimetembelea vingi lakini nilichobaini ni
kuwa hata vinavyojiendesha kwa sasa vinaweza kufungwa siku si nyingi
zijazo kutokana na kukabiliwa na mzigo wa gharama za kuviendesha na hii
inatokana na utitiri wa kodi zinazotozwa na Serikali,” alisema Nundu.
Alisema tatizo ni kukosekana kwa mfumo wa kuwapa
wafanyabiashara na wenye viwanda wazalendo, likizo ya kodi badala yake
wanapewa wawekezaji kutoka nje ambao hata wangetozwa kodi ya aina yoyote
wangelipa bila tabu.
“Hii inatokana na ukweli kwamba wengi wao huwekeza
matawi ya vitegauchumi vilinavyozalisha faida kubwa katika nchi
mbalimbali duniani,” alisema mbunge huyo.
“Viwanda vingi hapa Tanga havipo katika hali nzuri
hata kama sasa vinazalisha lakini vinaweza kufungwa wakati wowote na
tatizo kubwa ni kodi za Serikali zimekuwa nyingi ghafla,” alisema Nundu
na kuahidi kuishauri Serikali ili iweze kuangalia athari za utitiri huo
wa kodi yake.
Kwa upande wake, Said alisema licha ya kuwa
kiwanda hicho cha maji ya chupa bado ni kichanga lakini kimekuwa
kikitozwa kodi kubwa kuliko uwezo wake wa uzalishaji.


Post a Comment