Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

TAMKO LA MHESHIMIWA DKT. BINILITH MAHENGE (MB), WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MAZINGIRA) KUHUSU JANGWA NA UKAME DUNIA


IMG_9826
 Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Makamu wa Rais (Mazingira) Mhe. Ummy Mwalimu akizungumza na waandishi wa Habari katika Ukumbi wa Habari, Bungeni alipokutana nao kutoa Tamko kwa niaba ya Waziri kuhusu Siku ya kupambana na Kuenea kwa hali ya Jangwa na Ukame Dunia leo tarehe 16 Juni, 2014.  Picha na Owen Mwandumbya
……………………………………………………..
TAMKO LA MHESHIMIWA DKT. BINILITH MAHENGE  (MB), WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MAZINGIRA)  LILILOSOMWA NA MHE. UMMY MWALIMU – NAIBU WAZIRI OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MAZINGIRA)  KUHUSU SIKU YA KUPAMBANA NA KUENEA KWA HALI YA JANGWA NA UKAME DUNIANI TAREHE 16 JUNI  2014
 
Ndugu Wananchi,
Tangu  mwaka 1994  Baraza la Umoja wa Mataifa liliazimia kuwa kila  tarehe 17 Mwezi Juni  nchi wanachama  wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Kupambana na Kuenea kwa Hali ya Jangwa na Ukame, ziadhimishe siku ya  Kupambana na Kuenea kwa Hali ya Jangwa na Ukame. Tanzania ni mwanachama wa mkataba huu na hushirki maadhimisho haya kila mwaka. Madhumuni ya maadhimisho haya ni kuimarisha utekezaji wa mkataba huo kwa kutambua juhudi za nchi mbalimbali na changamoto  zilizopo na kushirikishana katika kuzitafutia ufumbuzi.  Afrika ndilo bara linaloathirika sana na hali ya jangwa na ukame.  Takriban asilimia 73 ya ardhi ya Afrika inakabiliwa na hali ya ukame na inakadiriwa kuwa kama juhudi za makusudi hazitachukuliwa kubadili hali hii, ifikapo mwaka 2030 Afrika itakuwa imepoteza theluthi tatu za ardhi iliyo bora kwa kilimo na ufugaji. 
Ni kwasababu hii, kesho tarehe 17 Juni, Watanzania tunaungana na wenzetu kote duniani katika kuadhimisha siku hii. Kauli mbiu ya mwaka huu ni “Ardhi ni mustakabali wa maisha yetu, tuilinde dhidi ya athari za mabadiliko ya tabianchi” (‘Land Belongs to the Future, Let’s Climate Proof It’). Kauli mbiu hii ina lengo la kuhimiza nchi zote duniani  kuongeza juhudi za  matumizi endelevu ya  ardhi katika juhudi za   kuhimili mabadiliko ya tabianchi ili  kufanisha  upatikanaji wa chakula. Sekta ya kilimo sasa inahitaji kulisha watu takriban bilioni tano kote duniani na watu bilioni tisa ifikapo 2050. Bila mipango madhubuti ya matumizi bora ya ardhi yanayozingatia mabadilko ya tabianchi itakuwa vigumu kuhakikisha usalama wa chakula kwa kizazi cha sasa na kijacho hasa kwa nchi za Afrika.
Ndugu Wananchi,
Pamoja na kukumbushana juu ya kuweka juhudi zaidi katika matumizi bora ya ardhi, siku ya kesho tarehe 17 inatukumbusha kuweka juhudi katika kuzuia uharibifu mwingine unaosababisha  kuenea kwa hali ya jangwa na ukame hususan ukataji wa miti na ufyekaji wa misitu ovyo.  Lazima tuongeze juhudi katika kuongoa na kuhifadhi maeneo ya ardhi kame yaliyoharibika kwa kufyeka misitu, kilimo cha kuhama hama na ufugaji usio bora.  Hata kama maeneo siyo kame, vitendo vya uharibifu wa mazingira kama hivi vinaweza kubadili eneo likawa jangwa kama juhudi za kuyaongoa na kuyatunza hazitafanywa.
Ndugu wananchi,
Tatizo la kuenea kwa hali ya jangwa na ukame ni kubwa pia hapa nchini. Inakadiriwa kuwa kiasi cha asilimia 45 hadi 75 ya nchi yetu ni eneo kame na linakabiliwa na tatizo hili la kuenea kwa hali ya jangwa na ukame. Maeneo ya katikati ya nchi ikiwa ni pamoja na mikoa ya Dodoma na Singida; na baadhi ya sehemu katika mikoa ya Mwanza, Shinyanga, Simiyu, Mara, Iringa, Manyara na Arusha na baadhi ya maaeneo ya Mkoa wa Kilimanjaro kama vile Same ndiyo yameathirika kwa kiwango kikubwa. Ni maeneo haya ambayo pia yana upungufu mkubwa wa misitu.
Hali hii inasababisha madhara makubwa yatokanayo na uharibifu wa ardhi ikiwa ni pamoja na kupungua kwa uwezo wa ardhi kuzalisha mazao bora;  na upungufu wa malisho bora ambao pia umepunguza uzalishaji kwa upande wa mifugo. Aidha ukataji wa misitu umesababisha kupungua kwa mvua katika baadhi ya maeneo haya na hivyo kusababisha  kuongezeka kwa hali ya ukame.  Wote tumeshuhudia maeneo haya yakikumbwa na uhaba wa chakula wa mara kwa mara na moja ya sababu kubwa ni kuenea kwa hali ya jangwa na ukame; pamoja na kutambua ukweli kuwa kwa kiasi kikubwa hali hii imesababshwa na mabadilko ya tabianchi.
 
Ndugu Wananchi,
Serikali inachukua hatua mbalimbali kuepuka changamoto hizi. Tayari Ofisi ya Makamu wa Rais imeweka  Mpango wa Taifa wa Kupambana na Kuenea kwa Hali ya Jangwa na Ukame (NAP) ambao umeweka  nyenzo muhimu ya kuongeza uzalishaji katika kilimo; kuondokana na tatizo la uhaba wa chakula; kuongoa maeneo yaliyoharibika na kurejesha misitu katika maeneo ya nyanda kame; na kupunguza umasikini kupitia usimamizi endelevu wa ardhi. Aidha mwaka 2006, Ofisi ya makamu wa Rais pia iliweka Mkakati wa kuzuia uharibifu wa ardhi na vyanzo vya maji ili kuhakikisha tatizo la kuenea  kwa hali ya jangwa na ukame linakuwa shirikishi kuanzia Serikali za Mitaa hadi Serikali Kuu. Mkakati huu umesaidia sana kuhifadhi maeneo ambayo yalikuwa yanaelekea kugeuka kuwa jangwa kutokana na kilimo kisicho endelevu, ufugaji holela na ufyekaji misitu ovyo.  Mkakati huu umekuwa muhimu sana hasa kwa kushirikisha wananchi na taasisi mbalimbali katika tuzo ya Rais ya  upandaji na utunzaji miti kama hatua muhimu katika hifadhi na matumizi bora ya ardhi.
Mwaka 2012 Serikali ilipitisha pia Mkakati wa Taifa wa kukabiliana na mabadilko ya tabianchi ambao pia kwa kiasi kikubwa umesadia kukabiliana na changamoto za kuenea kwa hali ya jangwa na ukame.
Ndugu Wananchi,
Kwa kumalizia naomba nitoe wito tena  kwa kusisitiza kauli mbiu ya mwaka huu kuwa   “Ardhi ni mustakabali wa maisha, tuilinde dhidi ya uharibifu”. Kila mmoja wetu kwa nafasi yake kesho afanye kitendo ambacho kwa namna moja au nyingine kitasaidia katika utunzaji na matumizi endelevu ya ardhi.  Inawezekana kuzuia kuendelea kwa mmomonyoko wa ardhi kwa kutumia njia mbalimbali za kuhifadhi ardhi;  kupanda miti ili kurejesha misitu pale ambapo imetoweka ili kuwezesha ardhi kuwa na rutuba ya kuweza kuzalisha zaidi katika maeneo kame na yasiyokuwa na rutuba.
Ofisi ya Makamu wa Rais itaendelea kuzihimiza Serikali za Vijiji na Halmashauri kutunga na kusimamia sheria ndogondogo za Hifadhi ya Ardhi na Misitu.
Napenda kuchukua fursa hii kuviomba vyombo vya habari kuendelea kuhamasisha na kuelimisha jamii juu ya umuhimu wa kuchukua hatua muafaka za kupambana na kuenea kwa hali ya jangwa na ukame kwa kufanya shughuli mbali mbali zinazochangia kutatua tatizo hili.  Aidha, napenda kuchukua fursa hii kuhimiza, mashirika yasiyo ya kiserikali na sekta binafsi kuongeza uwekezaji katika hifadhi ya misitu na matumizi endelevu ya ardhi ili kuhakikisha kwamba kunakuwepo na ustawi wa jamii kwa ujumla.
Ofisi ya Makamu wa Rais kama msimamizi  wa suala hili itahakikisha  inazidi kuweka mazingira bora ya ushirkishwaji ili kuhakikisha juhudi hizi zinakuwa  zetu wote kwa ajili ya  kizazi hiki na kizazi kijacho katika mazingira yanayokabiliwa na  mabadilko ya tabianchi.
Asanteni kwa kunisikiliza.
DKT.  BINILITH S. MAHENGE (MB.)
WAZIRI WA NCHI,
   OFISI YA MAKAMU WA RAIS –  MAZINGIRA
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top