WATU
zaidi ya 30 wanashikiliwa na polisi wilayani Muleba katika Mkoa wa
Kagera, wakituhumiwa kufanya vurugu na uharibifu wa mali, chanzo kikiwa
kifo cha mfanyakazi wa ndani aliyefia mkoani Arusha.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kagera, George Mayunga alisema vurugu
hizo zilitokea baada ya mwili wa mtoto huyo, Asera Tryphone (16)
kufikishwa katika Kijiji cha Bukono kilichoko Kata ya Muleba.
Kwa mujibu wa kamanda, binti huyo alikuwa akifanya kazi za ndani
mkoani Arusha, akaugua ghafla na kulazwa katika Hospitali ya Mount Meru
kabla ya kukutwa na mauti, Juni 12 mwaka huu.
Mwajiri wake, Valentina Maxmilian, alisafirisha mwili huo na baada ya
kuufikisha kijijini hapo, inadaiwa wazazi wa marehemu walikuwa wamepata
taarifa tofauti kwamba mtoto wao alifariki dunia kutokana na kipigo na
mateso.
Aidha, taarifa zilizokuwa zimeenea kijijini hapo ni kwamba, baadhi ya
viungo vya mwili, hususani sehemu za siri, mkono na mguu, vilikuwa
vimekatwa jambo lililohusishwa na ushirikina. Kamanda alisema wazazi
walitaka mwili huo ufanyiwe uchunguzi kabla ya kuupokea.
Waliamua kupiga simu Kituo cha Polisi cha Muleba, na Polisi ilitaka
kuongozana na ndugu hao hadi Kituo cha Afya cha Kaigara kwa ajili ya
uchunguzi.
Hata hivyo wanafamilia waligoma na kutaka polisi wafanye uchunguzi wa mwili huo nyumbani jambo ambalo halikuafikiwa.
Baada ya polisi kuondoka eneo hilo, inadaiwa wanafamilia walimbeba
maiti na kumtelekeza katika barabara iliyoko karibu na Kituo cha Polisi
Muleba.
Polisi walichukua mwili na kuupeleka Kituo cha Afya cha Kaigara.
Polisi walishauri ndugu hao kusubiri mganga aliyekuwa zamu aufanyie
mwili uchunguzi wa kitaalamu jambo ambalo waliafiki.
Wakati wakisubiri uchunguzi, wananchi walihamasishana tena na kuvunja
mlango wa chumba cha kuhifadhia maiti ambapo polisi waliamua kutumia
nguvu na kupiga mabomu ya machozi kuwatawanya wananchi hao.
Kulingana na maelezo ya Kamanda, baada ya kutuliza ghasia, uchunguzi
wa mwili ulifanyika na ndugu wakaridhika na kwenda kuzika ingawa
inadaiwa wapo baadhi ya watu waliokuwa wakishawishi wazazi wa marehemu
wasikubali.
Inadaiwa usiku wa kuamkia jana, wananchi walijikusanya na kwenda
Kijiji cha Buyango kilicho jirani na nyumbani kwa marehemu, na kuamua
kuchoma nyumba mbili za Veronica Maximilian (mama wa Valentina,
aliyekuwa mwajiri); ambaye anadaiwa ndiye alikwenda kuomba mtoto huyo
kwa familia ya Tryphone Joseph (54) aende kufanya kazi Arusha. Kutokana
na matukio hayo, polisi inashikilia watu hao wapatao 30 wakihojiwa
kutokana na tuhuma za kuvunja mlango wa chumba cha maiti, kuchoma
nyumba, kuhamasisha vurugu na kutelekeza mwili wa marehemu barabarani.
Miongoni mwa wanaoendelea kuhojiwa, yumo Veronica; anayedaiwa kumwomba mtoto huyo akafanye kazi kwa mwanawe.
Pia Polisi imesema inaendelea kufanya uchunguzi wa kina mkoani Arusha alikofia mtoto huyo na pia kuchunguza nyumbani kwao.
Wazazi wazungumza Mama mzazi wa mtoto huyo, Georgina Tryphone alisema
aliombwa mtoto wake kwenda kufanya kazi za ndani Januari mwaka jana.
Alisema alikuwa akipata mawasiliano ya simu kutoka kwa mwajiri wake.
Georgina alisema tangu Juni 12 mwaka huu, amekuwa, akipokea simu kupitia
kwa mwajiri wake akielezwa kwamba binti yake atakwenda karibuni
kuwasalimia.
Hata hivyo alidai, Juni 13 mwaka huu, alipigiwa simu na mwajiri huyo
akimweleza kwamba mwanawe anaumwa. Alidai baada ya saa takribani mbili,
alitaarifiwa amefariki dunia.
“Mimi na mume wangu tulianza kujawa na wasiwasi juu ya mwanetu na
hapo hapo tukapokea jeneza la maiti, lakini tulipotaka kufungua
tukazuiwa na aliyeuleta akidai umeharibika,” alisema mama huyo.
Aliendelea kudai, “tulipokuwa tunalazimisha kuuona mwili tuliambiwa
ugonjwa uliosababisha kifo chake unaambukiza hivyo ungeweza kuathiri
wananchi waliokuwa katika familia yetu.”
Taarifa hiyo ya mzazi inadai mwili huo ulikuwa na makovu na pia meno
manne ya juu hayakuwepo. Mkuu wa Wilaya Hata hivyo, Mkuu wa Wilaya ya
Muleba, Lembris Kipuyo, alisema katika kufanya uchunguzi wa mwili wa
marehemu, alikutwa na viungo vilivyodaiwa kutokuwepo.
Isipokuwa alisema, kilicholeta utata ni kukutwa meno manne hayapo na mwili kuwa na makovu mbalimbali.
Mkuu wa Wilaya amekemea wananchi kuendekeza imani za ushirikina na
kusambaza taarifa za uongo zilizosababisha uvunjifu wa amani. Kwa upande
wa familia ya mwajiri wa mtoto huyo iliyoko Kijiji cha Buyango pamoja
na mwajiri husika, haikupatikana kuzungumzia madai hayo kutokana na hali
tete iliyokuwa imewakabili.
Post a Comment