WATU wawili akiwemo mtoto Ayubu Hassan anayekadiriwa kuwa na miaka
7-10, mkazi wa Tungi Mnadani, Kigamboni jijini Dar es Salaam
wamefariki dunia katika matukio mawili tofauti.
Akithibitisha kutokea kwa matukio hayo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa
Temeke, Englibert Kiondo, alisema mtoto huyo alifariki juzi baada ya
kutumbukia kwenye dimbwi la maji majira ya saa 5 asubuhi.
Kiondo alisema kuwa maiti ya mtoto huyo mwanafunzi wa Shule ya Msingi
Kisiwani, ilikutwa ndani ya dimbwi hilo lililochimbwa kwa ajili ya
ujenzi wa Ofisi za Shirika la Umeme (Tanesco).
Alisema kwamba taarifa za awali zinaonyesha mtoto huyo alikuwa
akiogelea na wenzake na ndipo alipozama kwenye maji, hatimaye kufariki
na maiti yake kuhifadhiwa Hospitali ya Vijibweni.
Katika tukio jingine, mfanyabiashara mkazi wa Keko, aliyetambulika
kwa jina moja la Chuka (40), amefariki dunia baada ya kugongwa na gari
la Kampuni ya Express.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camilius Wambura, alisema tukio
hilo lilitokea juzi majira ya saa 10:11 asubuhi barabara ya Kawawa eneo
la Kigogo Sambusa.
Post a Comment