Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

MTEULE NAFASI YA UKUU WA WILAYA AJIUZULU KABLA HAJAAPISHWA

Kada aliyeteuliwa kuwa mkuu wa Wilaya ya Mbozi, Ally Muswanya ameachia wadhifa huo hata kabla ya kuapishwa.

Wakati uteuzi wa makada watatu wa kwanza ulisahihishwa na Ikulu, Maswanya hajaibuka kwenye hafla ya kiapo na tayari mtu mwingine amekwenda kuziba nafasi yake. 

Maswanya, ambaye alikuwa aapishwe juzi na mkuu wa Mkoa wa Songwe, Chiku Galawa, hakuapishwa na badala yake aliapishwa John Palingo ambaye katika uteuzi uliotangazwa na Ikulu alikuwa aongoze Wilaya ya Kongwa. 

Taarifa za Maswanya kuachia nafasi hiyo zilianza kusambaa kwenye mitandao ya kijamii juzi usiku zikieleza kuwa amejiuzulu nafasi hiyo, lakini haikuelezwa sababu za kuchukua uamuzi huo wa kukataa kumwakilisha Rais wilayani. 

Hata hivyo, Maswanya, ambaye ni meneja wa kampuni ya huduma za simu ya Tigo, Kanda ya Ziwa, hakutaka kuzungumzia kwa kina sakata hilo. 

“Kama ambavyo inajulikana, mimi ni meneja wa Kanda wa Tigo,” alisema Maswanya alipozungumza na Mwandishi

“Hayo ndiyo yako kwenye mamlaka yangu kuzungumzia. Kama ni suala la Tigo, karibu tuzungumze yote kuhusu mipango na mikakati yetu.” 

Maswanya alisema kwa sasa, nguvu akili na uwezo wake wote anaelekeza katika kutimiza wajibu kwenye nafasi hiyo yake Kanda ya Ziwa. 

Hata baada ya kuulizwa kama ndiye aliyekataa uteuzi, Maswanya alisisitiza “Hayo yatazungumziwa na mamlaka husika ambazo naamini kwa nafasi yako unazijua.” 

Alipoulizwa kama Maswanya alihudhuria hafla ya kula kiapo ya wakuu wa wilaya katikati ya wiki, kaimu mkurugenzi wa Idara ya Mawasiliano ya Rais, Gerson Msigwa alisema hafahamu kama alikuwapo au la kwa kuwa wengi ni wakuu wapya hivyo haikuwa rahisi kwake kujua nani hakuwapo.

Sarakasi ya meneja huyo kutochukua madaraka aliyopewa na Rais inafanya idadi ya watu walioteuliwa na kushindwa kuanza kazi kutokana na sababu tofauti kufikia wanne. 

Kabla ya wakuu wateule kula kiapo cha maadili Ikulu jijini Dar es Salaam, Rais Magufuli alieleza kuwa uteuzi wa wakuu hao ulifanywa kwa makini na kwamba anafahamu kwa majina watu wote aliowateua, akisema alizingatia umri, elimu na uzoefu. 

Tukio la kwanza lilikuwa la uteuzi wa Fikiri Said kuwa mkuu wa Wilaya ya Ikungi, lakini akabadilishwa kwa maelezo kuwa jina lake liliwekwa kimakosa. Badala yake aliyekuwa katibu wa CCM wa Mkoa wa Mwanza, Miraji Mtaturu akateuliwa kuchukua nafasi hiyo. 

Pia aliyeteuliwa kuongoza Wilaya ya Rombo, Fatma Toufiq alibadilishwa kwa maelezo kuwa tayari alishakuwa na wadhifa mwingine wa ubunge wa viti maalum na nafasi yake akapewa Agness Hokororo. 

Rais John Magufuli alisema wakati akielezea suala hilo kuwa hakutaka mtu ashike nafasi mbili kwa wakati mmoja na kwamba hiyo ndiyo tafsiri ya falsafa ya “Hapa Kazi Tu”. 

Tukio lililokuwa la aina yake katika uteuzi huo ni la kubatilisha uteuzi wa Emile Ntakamulenga aliyetangazwa kuwa mkuu wa Wilaya ya Serengeti. 

Hakukuwa na taarifa za awali za kubatilisha uteuzi huo na Ntakamulenga alienda Ikulu kama makada wengine, akaruhusiwa kujisajili na kuingia kwenye viwanja vya makazi hayo makuu ya nchi. 

Lakini wakati akisubiri kula kiapo cha maadili, Jaji Salome Kaganda akatoa maelezo kuwa kulifanyika makosa katika kutangaza jina lake na kwamba aliyekusudiwa alikuwa Nurdin Babu ambaye naye alikuwa ameitwa Ikulu siku hiyo.

Kutokana na makosa hayo, Jaji Kaganda alisema: “Naomba utupishe” na ndipo Ntakamulenga akanyanyuka na kuanza kuondoka kutoka viunga vya Ikulu akiacha maswali. 

Akizungumzia kutoapishwa kwa Maswanya kuwa mkuu wa Wilaya ya Mbozi na badala yake kumwapisha Palingo, Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Chiku Galawa alisema alipokea ujumbe mfupi kwa njia ya simu kutoka kwa Katibu Mkuu Kiongozi akijulishwa kwamba mtu aliyekuwa amepangiwa wilaya hiyo, John Ernest Palingo amebadilishwa kituo cha kazi, hivyo ataongoza Mbozi. 

Galawa alisema alipokea maelekezo ya ujumbe huo kutoka kwa Katibu Mkuu Kiongozi kwamba ampokee na kumuapisha ili aanze kazi mara moja, lakini akaongeza kuwa hana taarifa za mtu aliyeteuliwa awali kuwa bosi wa Mbozi. 

“Nilichofanya ni kutekeleza maagizo ya mkuu wangu,” alisema Galawa. 

“Pia mimi nilichokuwa nahitaji ni kukamilishiwa ma-DC wangu kwa wilaya zote, hivyo jana (juzi) asubuhi nilifanya mawasiliano na DC aliyeelekezwa na Katibu Mkuu Kiongozi, tukamtumia tiketi ya ndege na jana (juzi) mchana alifika na nikamuapisha kwa kuwa ni DC wa Mbozi pekee aliyekuwa amebaki.” 

Alisema siku ya Alhamisi alimuapisha mkuu wa Wilaya ya Ileje, na kwamba wengine wa wilaya za Momba na Songwe hawakutumiwa tiketi mapema, lakini walifika na juzi asubuhi aliwaapisha wakati wakimsubiri Palingo. 

Alisema kazi ya kwanza kuwapangia ni mbio za Mwenge wa Uhuru ambao uliingia jana asubuhi mkoani kwake ukitokea Mbeya. Alisema mwenge huo utawawezesha kufahamu vyema jiografia ya wilaya zao. 

Mkoani Dodoma, Jordan Rugimbana aliwaapisha wakuu wapya sita kati ya saba wa wilaya za mkoa huo baada ya Rais Magufuli kufanya mabadiliko madogo. 

Baada ya kuwaapisha wakuu hao wa wilaya, Rugimbana alielezea mabadiliko hayo ya Rais yaliyofanya akosekane mteule wa wilaya moja. 

“Aliyeteuliwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Kongwa sasa atakwenda kuwa Mkuu wa Wilaya ya Mbozi baada ya aliyeteuliwa kujiuzulu,” alisema.

Alisema kutokana na mabadiliko hayo, Wilaya ya Kongwa inasubiri uteuzi mwingine utakaofanyika wakati wowote kuanzia sasa. 

Wakuu wa wilaya walioapishwa Dodoma ni Elizabeth Kitundu (Bahi), Vumilia Nyamoga (Chamwino), Simon Odunga (Chemba), Christina Mdeme (Dodoma Mjini), Veneranda Makota (Kondoa) na Jabir Shekimweri (Mpwapwa). 
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top