Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

MKAPA APONGEZWA KUWAKUTANISHA MAGUFULI NA LOWASSA

BAADHI ya viongozi wa dini na wasomi, wamempongeza Rais mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa kwa hatua yake ya kuwakutanisha Rais John Magufuli na Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa.

Wamesisitiza kuwa hatua hiyo, inaonesha jinsi ambavyo demokrasia na amani imekomaa nchini. Viongozi hao walikutana juzi katika Misa Takatifu ya kuadhimisha Jubilee ya Miaka 50 ya ndoa ya Rais mstaafu Mkapa na mkewe, Anna, iliyofanyika juzi kwenye Kanisa la Mtakatifu Petro Oysterbay, Dar es Salaam.

Viongozi wa dini waliozungumza na gazeti hili na kupongeza hatua hiyo ni Askofu Msaidizi wa Jimbo la Bukoba la Kanisa Katoliki, Mhashamu Methodius Kilaini, Askofu wa Kanisa la Good News for All Ministry, Dk Charles Gadi na Shehe Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhadi Mussa Salum.

Kwa upande wa wasomi, gazeti hili lilizungumza na wahadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Benson Bana na Profesa Kitila Mkumbo ambaye pia ni Mshauri Mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo. Mwingine ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Profesa Mwesiga Baregu.

Maoni ya viongozi wa dini Akizungumza na gazeti hili jana kwa njia ya simu, Askofu Kilaini alisema jambo walilolifanya viongozi hao ni la kuungwa mkono na Watanzania wote.

“Jambo hili tumeliona na tumelifurahia sana na inatupa funzo kwamba tunapofanya siasa, tusisahau utu wetu. Siasa tuiache kama siasa… pia tumejifunza kwamba siasa si uhasama kwa sababu viongozi hawa wameweza kukutana na kupeana mikono,” alisema.

Alisema; “Mtu unapopeana mkono na mtu na kuangaliana usoni inaonesha kwamba hakuna uadui kati yenu hivyo kwa viongozi hao wameonesha kwamba wanakinzana katika siasa tu...” alisema.

Askofu Kilaini alisema, wanaamini kwamba kukutana kwa viongozi hao ambao wana mrengo tofauti ni mwanzo mzuri wa maridhiano ya pande zote mbili ambazo zimekuwa na misuguano ya kisiasa.

“Nawashauri Watanzania wenzangu kwamba kama viongozi wetu wakuu wameweza kukutana na kupeana mikono na kusalimiana tena na kupiga picha ya pamoja wakiwa karibu basi na sisi wafuasi wao tusijengeane chuki bali tupendane… tusiendelee kusigana na kupigana maana viongozi wetu wenyewe wanaelewana ila wanatofautiana tu katika siasa,” alisema.

Kwa upande wake, Askofu Gadi alisema kwa viongozi hao kukutana wanaamini kwamba maombi wanayoyafanya yanazidi kuimarisha umoja, amani na mshikamano wa nchi.

“Watanzania tuzidishe maombi maana yana nguvu na kupitia maombi hata yasiyowezekana yanawezekana, viongozi wa dini tuombe sana na tuhamasishe watu waombe maana hata hawa viongozi wetu ni waumini wetu na ni washiriki wazuri wa nyumba za ibada na tunashika nafsi zao,” alisema.

Aidha alisema viongozi hao wameonesha kwamba ni watu wanaomuogopa na kumheshimu Mungu kwa kusalimiana kwa upendo na kusisitiza kwamba maombi huleta upatanisho na kubadilisha jamii.

Alisema kupitia kanisa hilo, wamekuwa wakifanya huduma ya maombi mara kwa mara ambapo kwa sasa wameanza maombi ya siku 1,001 na wiki iliyopita walifanya maombi wilayani Chato mkoa wa Geita kwa ajili ya kumuombea Rais Magufuli katika utendaji wake.

Shehe Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhadi Mussa alisema tukio hilo ni la heri, kwa kuwa watu walikuwa wakiwatazama viongozi hao kama maadui, hivyo kwa kupeana mikono wameithibitishia jamii kwamba wanatofautiana tu katika siasa.

“Walichokifanya viongozi wetu wameonesha kwamba, siasa si uadui na tunaomba kukutana huko kuwe heri na waendelee kukutana mara kwa mara kwa ustawi wa Taifa letu,” alisema.

Wasomi nao wafunguka Katika hatua nyingine, wasomi nao walieleza kupongeza kitendo hicho kilichowakutanisha walikuwa wapinzani wa karibu wakati wakigombea urais katika Uchaguzi Mkuu uliopita, Rais Magufuli na Lowassa.

Kwa namna ya pekee wasomi hao walipongeza pia kitendo hicho cha kizalendo, ambacho viongozi hao walikionesha kwa kushikana mikono, kutabasamu na kuonekana wakiteta kwa nyuso za tabasamu.

Profesa Baregu mbali na kupongeza uzalendo huo, alisema kukutana na kuzungumza kwa Rais Magufuli na Lowassa ichukuliwe kuwa ni fursa kwa viongozi hao, ambayo wanapaswa kuitumia kufanya mazungumzo ya kuimarisha amani.

“Hiyo itafsiriwe kuwa ni fursa ambazo huwa inajitokeza katika mazingira tofauti, aidha kwa kupangwa au bila kupangwa, lakini kikubwa watumie fursa hiyo vilivyo,” alisema Profesa Baregu. Alisema kukutana kwa Rais Magufuli na Lowassa ni fursa nzuri kwani walikuwa hawajawahi kukutana tangu kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu mwezi Oktoba, mwaka jana.

Alisema mambo machache ambayo viongozi hao walizungumza juzi katika muda mfupi, yataweza kutumika vizuri kutatua mambo ya kisiasa ambayo yanaendelea hapa nchini kwa sasa na kufungua njia nzuri.

“Na hii inaweza kuwa njia nzuri kuzungumzia masuala ya kisiasa, demokrasia na pia Katiba mpya ambayo ndio kilio kikubwa cha Watanzania ili tuweze kupata Katiba mpya,” alisema Profesa Baregu.

Msomi huyo alisema pia fursa hiyo itumike kuleta amani kwa wananchi na kwa maana ya kupatikana maridhiano katika masuala ya kisiasa.

Profesa Mkumbo alimpongeza Mkapa kwa kitendo hicho cha kuwakutanisha viongozi hao na pia kuwapongeza Rais Magufuli na Lowassa kwamba pamoja na walikuwa katika mchuano mkali katika Uchaguzi Mkuu uliopita na mwisho Rais Magufuli kupata ushindi, lakini wameonesha bashasha ya aina yake.

“Huo ndio utanzania ambao Watanzania wanautaka, tunaweza kutofautiana bila kugombana, utanzania wetu haujali dini, kabila wala kitu kingine chochote,” alisema Profesa Mkumbo.

Aidha alisema muonekano pia wa viongozi hao wawili, ulionesha wazi walikuwa katika hali ya amani, “hata muonekano wao uliweza kuona kabisa ilikuwa safi, na Rais wetu kama tunavyomjua si mtu wa kuficha jambo lakini walicheka na kuzungumza vizuri.”

Kwa upande wake, Dk Bana alisema kwa muonekano ambao walionesha viongozi hao wawili jana ilionesha changamoto za kisiasa zilizokuwepo, hazitaendelea kuwepo tena kwani viongozi hao walionekana kuteta kwa upendo.

“Ile inaonesha kabisa harakati za Ukuta (Umoja wa Kupambana na ‘Udikteta’ Tanzania) hazipo tena na jana (akimaanisha juzi) zilizikwa pale, walionekana kunong’ona na kupeana mikono kwa amani kabisa na inaonesha wote ni wamoja katika kujenga nchi yenye amani,” alisema Dk Bana.

Alisema nasaha ambazo zilitolewa pia viongozi wa dini katika hafla ile, zitumike pia vizuri katika kuondoa masuala yote ya kisiasa, ambayo yamekuwa yakileta mvutano na badala yake kujenga upendo na amani. Alisema uwazi wa Rais Magufuli na maneno aliyozungumza, yalikuwa ya busara.
Download Our App

1 comments:

HATA MM NAMPONGEZA ILA ZAIDI NAMPONGEZA MR LOWASA AMEUAMINISHA ULIMWENGU KUWA YEYE ANA HEKMA NAFIKIRI ANAMOYO MPANA NA JASIRI KAMA NYANGUMI, AHSANTENI

Reply

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top