Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

MZEE KINGUNGE NGOMBALE MWIRU AIBUKA, AVUNJA UKIMYA

Aliyekuwa kada wa CCM, Kingunge Ngombale Mwiru  amewaomba  marais wastaafu, Rais Ali Hassan Mwinyi na Benjamin Mkapa kuzungumza na Rais John Magufuli ili aitishe kikao kati ya Serikali na Chadema kwa ajili ya kusitisha maandamano yaliyopangwa kufanyika Septemba Mosi.
 
Kingunge  ametoa kauli hii  leo nyumbani kwake jijini Dar es Salaam mbele ya waandishi wa habari  wakati akiongelea mvutano kati ya Chadema na serikali unaoendelea kwa sasa.

Chadema kimeingia kwenye mvutano mkubwa na serikali kutokana na dhamira yake ya kufanya mikutano na maandamano nchi nzima chini ya mwavuli wa Umoja wa Kupinga Udikteta (Ukuta).

Hivi karibuni, Rais John Magufuli alisisitiza kutoruhusu maandamano na mikutano ya kisiasa na kuagiza kuwa, wanaotaka kufanya mikutano wafanye ndani ya mipaka ya majimbo yao na si vinginevyo jambo ambalo Chadema wanapinga.

Hali hiyo imeibua mtikisiko mkubwa nchini huku kada mbalimbali ikiwa ni pamoja na viongozi wa dini, wanasiasa, wasomi na wananchi wa kawaida wakitaka kupatikana suluhu kabla ya Septemba Mosi, tarehe iliyopangwa kuanza maandamano na mikutano hiyo.

Kwenye mkutano wake na wanahabari Kingunge anawalaumu viongozi wastaafu wakiwemo marais pamoja na mawaziri wakuu kwa kukaa kimwa wakati huu ambao nchi inatikishwa huku Katiba ya Jamhuri ikisiginwa.

Miongoni mwa viongozi wanaolalamikiwa kutosikika ama kuchukua hatua zozote ili kuilinda Katiba ni pamoja na Marais Wastaafu, Alhaj Ali Hassan Mwinyi, Benjamin Mkapa na Aman Abeid Karume (Zanzibar).

Viongozi wengine waliotajwa ni Mawaziri Wakuu Wastaafu, Cleopa Msuya; Jaji Mstaafu, Joseph Warioba.

“Mzee Mwinyi yupo kimya, Mkapa kimya, Warioba kimya, Cleopa Msuya kimya, Amani Karume kimya,” amesema Kingunge na kuongeza;

“Ukimya huu unatokana na nini? Hawa wote waliwahi kula viapo vya utii kwa Katiba. Mimi nahoji, wazee wenzangu vipi mnakuwa kimya? Nawaambia kuwa mnachofanya si sawa.

“Naomba wazee wote tujitokeze kuhesabiwa katika hili la uvunjifu wa Katiba na sheria.”

Kingunge ambaye alihamia Chadema akitokea CCM kabla ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana kutokana na kutoridhishwa na namna mchakato wa kumpata mgombea urais kutoka chama hicho amesema, Chadema inatumia haki yake ya kikatiba.

“Naomba Rais Magufuli, akubali kuitisha kikao na Chadema ambacho pia wazee wastaafu watahudhuria, akifanya hivyo hata sisi wazee tutawageukia Chadema na kuwambia wasitishe mpango wao wa maandamano,” amesema.

Amesema kwamba, kibaya zaidi Jeshi la Polisi linaandaa bunduki kwa ajili ya kupambana na raia ambao hawana kitu na kuwa, hali hiyo haipaswi kuvumiliwa.

Mwanasiasa huo amesema, Chadema wameamua kutetea haki yao ya kikatiba na kisheria kwa kufanyaa maandamano kote nchini, na kina wafuasi wengi hivyo si jambo la kubeza.

“Upande wa pili, lipo Jeshi la Polisi na watawala ambao wanaahidi kuwakabili. Kwa bahati mbaya polisi na watawala hawatetei Katiba wala Sheria,” amesema.

Amesema kuwa, Tanzania kwa sasa inakabiliwa na ombwe la uongozi na kwamba, nchi imekosa watawala wenye sifa thabiti ya kuongoza taifa.

“Kwa hakika, tatizo kubwa la sasa la nchi yetu ni ombwe la kiuongozi, kwasababu kama ni watawala tunao kweli kweli, lakini tunachokosa ni watawala wenye maarifa ya kiuongozi.

“Inashangaza kuona wazee wastaafu kukaa kimya wakati nchi inakabiliwa na tatizo linaloweza kutuangamiza.

“Upande mmoja unanoa mapanga, unaanda bunduki kwa ajili ya kuchinja na kuua na upande wa pili wapo raia tu, tena wasio na silaha zozote.”

Kingunge anasema, wananchi ambao serikali na Jeshi la Polisi wanajiandaa kupambana nao, wanalilia Katiba na sheria zifuatwe.

“Laiti kama Chadema wangekuwa hawatetei Katiba na sheria, kungekuwa na kila sababu ya kuwashughulikia, lakini kwa kuwa wanatetea Katiba na sheria, kuna umuhimu wa kuyapa uzito madai yao,”amesema Kingunge.

Mwanasiasa huyo amesema kuwa, mvutano wa sasa sio wa Chadema na serikali isipokuwa ni suala la wananchi wote wa wenye mapenzi mema na taifa lao.

“Hili ni suala la kila mtu anayependa utawala wa Katiba, Sheria na Utawala Bora,” amesema.
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top