Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

Wiki ya Nenda kwa usalama yazinduliwa rasmi


Serikali imeagiza Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), kuondoa matuta kwenye barabara kuu, ambayo yametajwa kuwa chanzo cha ajali.

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamad Masauni, ametoa agizo hilo jana wakati wa ufunguzi wa Wiki ya Usalama Barabarani katika Viwanja vya Kalangalala mkoani Geita.

Alisema matuta yaliyoko kwenye barabara kuu, yamekuwa moja ya vyanzo vya ajali nyingi nchini na kusisitiza kuwa hali ya ajali iliyopo ni vyema suala la usalama barabarani kuwa ajenda ya kitaifa.

Pia alivitaka vvyombo vya usalama, kuwachukulia hatua kali na stahiki wale wote wanavunja sheria za Usalama Barabarani bila kumuogopa au kumuonea mtu yeyote.

Alisema ajali za barabarani zimekuwa ni tatizo kubwa na kuwa takwimu za miaka mitatu kuanzia Januari 2013 hadi Desemba 2015, zinaonesha kuwa ajali zilizotolewa taarifa ni 46,536 ambazo zimeua watu 11,230.

Masauni alisema kuwa kundi linaloongoza kwa kuathirika na ajali hizo ni abiria ambapo watu 3,444 wamekufa, wakifuatiwa na watembea kwa miguu 3,328.

Alisema wapanda baiskeli wanashika nafasi ya tatu kwa watu 2,493 kupoteza maisha, huku madereva waliokufa ni 813 na wasukuma mikokoteni zaidi ya 400 wamepoteza maisha.

“Takwimu za miezi sita tangu Januari mpaka Agosti mwaka huu, ajali 6,971 zimetokea na kusababisha vifo 2,217 na kati ya hivyo 1,809 ni vile vilivyotokana na pikipiki. Hali ya ajali sio nzuri na ni vyema suala la usalama barabarani likawa ajenda ya kitaifa,” alisema.

Alisisitiza kutolewa elimu ya watumiaji wote kuhusu matumizi sahihi ya barabara, wamiliki na madereva kuacha kuendesha vyombo chakavu na kufanyika kwa ukaguzi wa mara kwa mara.

“Shirika la Viwango Tanzania (TBS) pia linatakiwa kuendelea kufanya ukaguzi wa matairi, bodi na vipuri vya mabasi,” alisema.

Aidha, Masauni aliwataka watumiaji wote wa barabara, kufuata sheria na kanuni za barabarani, kuacha kushabikia mwendo kasi, kuvuka kwenye vivuko vya watembea kwa miguu na waendesha baiskeli na mikokoteni kuacha kuendesha barabarani na watoto kuvuka barabara wakiwa chini ya uangalizi.

Naibu Waziri wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Usalama Barabarani, Edwin Ngonyani, alisema kutokana na kukithiri kwa ajali, Baraza lilikuja na mikakati ya miezi sita ya kupunguza ajali hususan zinazotokana na makosa ya kibinadamu.

Alisema makosa ya kibinadamu yamekuwa yakichangia ajali kwa asilimia 80 na kufuatiwa na mwendokasi ambao unachangia kwa asilimia 12, mazingira ya barabara yanachangia kwa asilimia 6 na asilimia 2 zinatokana na sababu nyingine.

“Tumekuja na mikakati ambayo inatekelezwa kwa miezi sita, lengo kuu ni kuondoa makosa ya kibinadamu yanayochangia ajali, na Februari mwakani tutatathmini mafanikio ya mikakati hiyo,” alisema.

Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani katika Jeshi la Polisi, Mohammed Mpinga, ambaye pia ni Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Usalama Barabarani, alisema katika Wiki ya maadhimisho hayo watoa elimu ya matumizi sahihi ya barabara, na kutoa elimu kwa waendesha pikipiki 300 na walimu 100, na pia watakagua vyombo vya moto na kupima afya za madereva kwa kutumia zahanati mwendo.
Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani nchini, ambaye pia ni Katibu wa Baraza la Taifa la Usalama Barabarani, Naibu Kamishna, Mohamed Mpinga akizungumza katika maadhimisho ya Wiki ya Nenda kwa Usalama Barabarani inayofanyika Kitaifa katika Viwabya vya CCM Kalangalala mjini Geita. Maadhimisho hayo yalizinduliwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Usalama Barabarani, Mhandisi Hamad Masauni (kulia).
Mgeni rasmi Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Usalama Barabarani, Mhandisi Hamad Masauni (kulia), akimsikiliza Askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani kutoka Makao Makuu, Koplo Faustina Ndunguru wakati alipokuwa anatoa maelezo jinsi magari mbalimbali yanavyovunja sheria za barabarani. Picha zote na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.
Mgeni rasmi Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Usalama Barabarani, Mhandisi Hamad Masauni (kushoto) akimpa zawadi ya Kombe la Ushindi wa kwanza Mwanafunzi wa Shule ya Msingi Bunge jijini Dar es Salaam, Veronica Innocent, ambaye alishinda nafasi ya kwanza katika uchorani wa picha zinazoonyesha usalama barabarani ambayo zilipambanishwa katika shule za Mkoa wa Dar es Salaam na Geita.
Washiriki wa maonesho (waendesha bodaboda) wakiwa katika maandamano ya kuadhimisha Wiki ya Nenda kwa Usalama Barabarani iliyozinduliwa katika Viwanja vya CCM Kalangalala, mjini Geita jana. Kauli mbiu ya Maadhimisho ya mwaka huu ni “Hatutaki ajali tunataka kuishi salama”.
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top