Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

Maalim Seif aivaa Tume ya uchaguzi (NEC)


Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad amesema uamuzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) wa kutaka pande zinazovutana ndani ya chama hicho kuteua kwa pamoja jina la mgombea ubunge katika uchaguzi mdogo wa Jimbo la Dimani kuwa ni wa kukurupuka. 

Desemba 8, Mkurugenzi wa Uchaguzi wa NEC, Ramadhani Kailima alisema fomu za wagombea wa CUF katika uchaguzi huo zitapaswa kusainiwa na pande mbili zilizo na mgogoro wa uongozi.

“Kipengele cha 4 (5) (iii) cha Sheria ya Uchaguzi kinataka fomu za wagombea kwenye chama chenye mgogoro zisainiwe na viongozi wakuu wote wawili kwa vile wamethibitishwa na Msajili wa Vyama Siasa,” alinukuliwa Kailima.

Lakini juzi, Maalim Seif alizungumzia uamuzi huo wa NEC na kusema kila chama cha siasa kina kanuni na taratibu zake za kuwapata wagombea wa nafasi mbalimbali.

“NEC wamenishangaza kwa sababu nchi inaendeshwa kwa sheria na kanuni labda nimuulize Kailima ameitazama Katiba ya CUF inasema nini kuhusu mchakato wa wagombea? Tume inatoa uamuzi wa kisiasa ambao haukupaswa kutolewa na chombo hiki muhimu,” alisema Maalim Seif.

Hata hivyo, licha ya kushangazwa na hatua hiyo, Maalim Seif hakuwa tayari kutoa msimamo wa CUF juu ya suala hilo akisema: “Ni mapema mno kusema tutafanya nini?”

Tayari Naibu Katibu Mkuu wa CUF Zanzibar, Nassor Ahmed Mazrui amesema lengo la NEC ni kutaka chama hicho kikose mgombea. 

Wakati Maalim Seif akieleza hayo, Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba anayetambuliwa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa alisema:

“Tutaweka utaratibu na watu wajitokeze ili tuweze kufanya uteuzi wa mgombea. Ingawa kulikuwa na mgombea wa mwaka jana, nina imani watajitokeza wengine na Baraza Kuu ndilo litamteua.”

Alisema uchaguzi kwa ngazi udiwani hakuna tatizo kwa sababu mchakato wake unaishia wilayani, lakini kwa ubunge lazima wakae pamoja.

CUF imekuwa katika mgogoro baada ya Profesa Lipumba aliyejiuzulu uenyekiti mwaka jana kuibuka na kutaka kurejea kwenye nafasi hiyo, lakini viongozi wengine wakamuwekea ngumu na kuibua mgogoro uliopo mahakamani.
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top