Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

Kishindo kingine makinikia chaiva

KISHINDO kingine kuhusiana na sakata la usafirishaji wa mchanga wa madini (makinikia) kwenda ughaibuni kimeiva baada ya kuwapo kwa taarifa za ujio wa vigogo wa kampuni ya Barrick Gold nchini ili kuanza tena mazungumzo mazito na serikali.

Hivi karibuni, Serikali ilitangaza kuzuia usafirishaji makinikia kwenda ughaibuni na pia Mamlaka ya Mapato (TRA) kuwataka Barrick, ambao humiliki hisa nyingi za kampuni ya Acacia Mining, kulipa kodi na adhabu inayofikia jumla ya dola za Marekani bilioni 190, sawa na zaidi ya Sh. trilioni 400.

Kodi hiyo ni matokeo ya taarifa zisizokuwa sahihi kuhusiana na madini yaliyochimbwa kuanzia mwaka 2000 -- kiasi ambacho kilibainishwa na ripoti za kamati mbili teule za Rais kuchunguza makontena 277 ya makinikia yaliyozuiliwa kwenye bandari ya Dar es Salaam.

Taarifa ambazo Nipashe ilizipata jana na kuthibitishwa na Barrick na Acacia, ni kwamba viongozi wa juu wa Barrick wanatarajiwa kutua nchini wiki ijayo ili kuendelea na mazungumzo na serikali kwa nia ya kufikia mwafaka juu ya suala hilo.

Nipashe inatambua kuwa ikiwa ujio huo wa Barrick utafanyika wiki ijayo, itakuwa ni siku chache baada ya Rais John Magufuli kutangaza wazi akiwa katika ziara zake mkoani Kigoma kuwa anaweza kutaifisha migodi yote ya wawekezaji hao na kuwapa Watanzania ikiwa watachelewa kufanya mazungumzo kwa lengo la kulipa mapato ya serikali yaliyopotea katika kipindi chote tangu waanze shughuli zao nchini.

“Kwa sasa tumewaita wafanye mazungumzo wamekubali, lakini wakichelewa nitafunga migodi yote, ni mara kumi migodi hii tukaigawa kwa Watanzania wachimbe wao wauze tupate kodi kuliko hawa wawekezaji ambao hawalipi kodi,” alisema Rais Magufuli.

Akizungumzia ujio huo wa vigogo wa Barrick nchini, mmoja wa maofisa wa Acacia aliiambia Nipashe jana kuwa hawashiriki moja kwa moja kwenye mazungumzo hayo, lakini chochote kitakachoamriwa watakiridhia.

Aidha, katika ripoti ya mapato ya robo mwaka ya Barrick iliyopo kwenye tovuti yao, imeelezwa kuwa wataendelea na mazungumzo na Serikali ya Tanzania kuanzia wiki ijayo kuhusu makinikia yaliyozuiliwa kusafirishwa nje na mambo mengine yanayohusu utendaji wa kampuni hiyo nchini.

Mbali ya hilo, kampuni hiyo ilielezea mwenendo wa biashara kwa kipindi kilichomalizika Juni 30 mwaka huu kuwa ni mzuri, licha ya kuongezeka kwa gharama za uchimbaji dhahabu kwa asilimia 10.

Makubaliano ya kufanyika kwa mazungumzo kati ya Barrick na Serikali yalitokana na kikao kilichofanyika Juni 14, mwaka huu Ikulu jijini Dar es Salaam, kati ya Rais Magufuli na Mwenyekiti wa Barrick, Prof. John Thornton.

Katika mazungumzo hayo, Prof. Thornton alisema kampuni yake iko tayari kufanya mazungumzo na Tanzania ili kulipa fedha ambazo Tanzania imezipoteza.

Mazungumzo hayo yalifanyika zikiwa zimepita siku tatu baada ya Rais Magufuli kukabidhiwa ripoti ya pili ya mchanga wa madini na kamati ya pili aliyoiunda kuchunguza suala hilo.

Alipoulizwa kuhusu ujio wa viongozi wa Barrick, Kamishna wa Madini, Mhandisi Benjamin Mchwampaka, alijibu kuwa suala hilo haliratibiwi na wao.

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Gerson Msigwa, ambaye alisema atafutwe Naibu Waziri wa Wizara ya Nishati na Madini, Dk. Medard Kalemani ili azungumzie ujio huo mwingine wa viongozi wa Barrick.

Hata hivyo, jitihada za gazeti hili kumpata Dk. Kalemani zilishindikana jana baada ya kukosekana kupitia simu yake ya mkononi.

Source: Nipashe
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top