Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

WABUNGE WAWA MBOGO, WAIRARUA BAJETI YA SERIKALI 2013-2014 ..... HAYA HAPA NI MAONI YAO

BAADHI ya wabunge wametoa maoni yao kuhusiana na Bajeti ya Serikali ya mwaka 2013/14, yakionekana kung’ata na kupuliza. Hali hiyo, ilitokana na wabunge wengi wa CCM kudai bajeti hiyo ni nzuri na imegusa kila idara, huku wapinzani wakidai haina jipya kutokana na kushindwa kubuni vyanzo vipya vya mapato.

Akitoa maoni, Kingozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe (Chadema), alisema hakuna jambo la kushangilia katika bajeti hiyo, kwa kuwa utaratibu ni uleule.

Alisema Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), bado imeng’ang’ania kuongeza mapato katika soda, bia na sigara na kuacha sekta ambazo zinauwezo mkubwa wa kuongeza mapato ya Serikali.

“Vipo vyanzo vya mapato kama vile madini, gesi na maliasili lakini mchango wake ni mdogo.

“Nashangaa wabunge wa CCM wanaishangilia bajeti wakati inakwenda kuwaumiza wananchi, kutokana na kupandisha bei ya mafuta.

“Bajeti hii, pia haijaonyesha msisitizo wowote wa kubana matumizi ya Serikali, matumizi ya Serikali bado ni makubwa.

“Na jambo kubwa la kujifunza ni kwamba, Serikali haina utaratibu wa kutekeleza bajeti yake, kilichoelezwa hapa bungeni na utekelezaji wake itakuwa ni tofauti,” alisema Mbowe.

Mbunge wa Kuteuliwa, James Mbatia (NCCR-Mageuzi) naye aliikosoa Serikali kuongeza kodi kwa bia na vinywaji vingine, huku ikishindwa kutafuta vyanzo vingine vya mapato.

“Kwa mfano katika sekta ya bahari kuu, tunaweza kukusanya zaidi ya bilioni 821, badala ya kuongeza kodi kwenye bia.

“Kwa mujibu wa utafiti uliofanyika, hakukuwa na tija yoyote kwani baada ya Serikali kuongeza kodi ya bia katika bajeti ya mwaka jana, watu wengi walihamia katika matumizi ya pombe za kienyeji ambazo kwa kiasi kikubwa zinaathiri nguvu za kiume,” alisema Mbatia.

Mbunge wa Bariadi Mashariki, John Cheyo (UDP) alisema bajeti hii ni ya kihistoria tangu Tanzania ipate uhuru, kwa kuwa mwaka huu wabunge wameshiriki kuipitia pamoja na kuomba kuongezwa fedha katika baadhi ya bajeti za wizara.

“Tumeshuhudia leo Serikali imeongeza zaidi ya Sh bilioni 500 zilizoombwa na wabunge, zamani fursa hii haikuwepo,” alisema Cheyo.



Mbunge wa Igunga, Dk. Dalay Kafumu (CCM), aliisifia bajeti hiyo kwamba ni nzuri kwa kuwa wabunge walipata fursa ya kuipitia na hivyo kusababisha marekebisho mengi kufanyika.

Mbunge wa Viti Maalum, Magreth Sitta (CCM), alisema amepokea bajeti hiyo kwa matumaini makubwa hasa katika kipengele cha mapato ya simu, ambapo mapato hayo yataelekezwa katika sekta ya elimu.

Mbunge wa kuteuliwa, Zakhia Meghji (CCM) amezungumzia kuhusu Sera ya Fedha ambapo alisema wabunge waliipigia mno kelele sera hiyo hususan katika suala la riba kubwa kwa sekta ndogo.

Alisema kuweka sera maalum ya fedha, itawasaidia wananchi waliojiunga kwenye vikoba na SACCO's kuanzisha benki zao wenyewe ambazo zitatoza riba kidogo.

Mbunge wa Peramiho, Jenista Mhagama (CCM) alipongeza mfumo mpya wa kujadili bajeti, kwa kuwa wabunge wamepata fursa ya kujadiliana na Serikali na kuongeza fedha katika maeneo yaliyolalamikiwa kuwa na pungufu.

“Mfumo huu umesaidia kufanyiwa marekebisho katika baadhi ya maeneo ikiwemo katika sekta muhimu za umeme na maji, hivyo wananchi wengi watanufaika hususan wa maeneo ya pembezoni,” alisema.

Mbunge wa Wawi, Hamad Rashid Mohamed (CUF), alisema bajeti hiyo haina jipya kwani imebaki kupandisha kodi ya bia na sigara na kuacha maeneo muhimu yanayoweza kuliingizia taifa mapato.

Mbunge huyo pia alihoji sababu za Serikali kupata kigugumizi katika kupiga marufuku matumizi ya magari ya kifahari kama vile mashangingi, ili kubana matumizi ya Serikali.

Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (Chadema) mbali na kuzungumzia utaratibu uleule wa kuongeza kodi katika bia na soda, alisema pia misamaha mingi ya kodi bado haijaondolewa na utaratibu wa kuyabana makampuni makubwa yalipe kodi haujawekwa bayana.

“Pia Serikali imeongeza kodi ya petroli na dizeli za aina tatu kwa wakati mmoja, hali itakayochangia ongezeko la gharama za usafiri, usafirishaji na uzalishaji na hivyo kuongeza mfumuko wa bei na gharama za maisha kwa wananchi.

“Serikali haijaja na mkakati madhubuti wa kupunguza gharama zisizo za lazima na kudhibiti ufisadi kwenye manunuzi,” alisema Mnyika.


MTANZANIA
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top