Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

WANASIASA WANAVYOMZUNGUMZIA NELSON MANDELA

Rais Jakaya Kikwete (pichani) ni miongoni mwa viongozi wa kisiasa waliotuma salamu za rambirambi, kutokana na kifo cha Rais mstaafu wa Afrika Kusini, Nelson Mandela.

Kwa mujibu wa taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na Ikulu kwa Rais Jacob Zuma wa Afrika Kusini  na kupitia kwake, kwa mkewe Graca Machel, wanafamilia wote na wananchi wote wa Afrika Kusini alisema ni msiba mkubwa kwa wote.

“Afrika Kusini, Afrika na dunia kwa jumla imepoteza mtu mashuhuri na shujaa mkubwa wa karne ya 20 na 21. Tunaelewa  machungu waliyonayo wananchi wa Afrika Kusini kwa kupoteza kiongozi shupavu, jasiri, mwanamapinduzi, mvumilivu na mstahimilivu,” alisema Rais Kikwete.


Rais amemwelezea  Mzee Mandela kuwa ni  kielelezo cha aina yake kwa wanadamu kwa moyo wake wa kusamehe, huruma na upendo uliomwezesha  kuwaunganisha wananchi wa Afrika Kusini kuwa  taifa moja baada ya kipindi kirefu cha mapambano dhidi ya ubaguzi wa rangi.

“Mandela  ni mfano bora kwa wanadamu wa jinsi binadamu muungwana anavyopaswa kuwa. Ni wajibu wa wana-Afrika Kusini, Afrika na dunia kwa jumla kuiga mfano wake hasa moyo wake wa uzalendo, kujitolea hata maisha yake kwa ajili yake na wananchi wenzake,” alisema.

Rais Kikwete pia ametangaza siku tatu za maombolezo kuanzia jana na bendera zote zitapepea  nusu mlingoti.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba amemweleza Mandela kama mfano wa kuigwa na viongozi wa Afrika.

Akizungumza kwa njia ya simu na gazeti hili, Profesa Lipumba alisema:

“Tumepokea kwa mshtuko mkubwa taarifa za kifo cha Rais wa kwanza mweusi wa Afrika Kusini, Nelson Mandela. Tunamshukuru Mungu kwa Madiba kwani ametoa mchango mkubwa si kwa Afrika tu bali kwa dunia nzima katika mapambano ya ubaguzi wa rangi, ni mchango mkubwa sana,” alisema Profesa Lipumba na kuongeza:

“Hata alipotoka gerezani baada ya kufungwa kwa miaka 27, Mandela hakuwa na kinyongo bali alisamehe na alianzisha maridhiano yaliyoleta heshima na kujenga Serikali inayojali haki za binadamu.” Amewataka viongozi wa Afrika kufuata nyayo zake ili kuleta heshima ya Bara hilo:

“Afrika bado ina matatizo mengi lakini kama viongozi watafuata mfano wa Mandela wa kutokuwa na kinyongo na kusamehe hata baada ya kufungwa gerezani miaka 27, basi wataleta heshima ya Afrika,” alisema Profesa Lipumba.

Naye mwanasiasa mkongwe nchini, Ibrahimu Kaduma alisema, Mandela ameacha fundisho kuwa viongozi wanatakiwa na uthubutu katika kuamua kufanya kile wanachokiamini hata kama itawalazimu kifo.

MWANANCHI
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top