STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 21 Januari, 2014
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema iko tayari kushirikiana na Serikali ya
Italia katika nyanja za elimu na hifadhi ya sehemu za historia kama
ilivyo katika sekta nyingine.
Hayo
yameelezwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein wakati akizungumza na Balozi wa Italia nchini Bwana
Luigi Scotto aliyemtembelea Ikulu jana.
Katika
mazungumzo hayo Balozi Luigi alimueleza Dk. Shein kuwa nchi yake
imeanzisha Mpango wa Ushirikiano Kati ya Italia na Afrika ambao umelenga
kuimarisha ushirikiano kati ya nchi hiyo na nchi za Afrika.
Alibainisha
kuwa chini ya mpango huo Zanzibar inaweza kufaidika katika suala la
uhifadhi na ukarabati wa sehemu za historia kama vile Mji Mkongwe pamoja
na masuala ya ufundishaji wa lugha ya Kitaliano hapa nchini.
Dk.
Shein alimueleza Balozi Luigi kuwa ukarabati na uhifadhi wa mji Mkongwe
ni suala linalopewa umuhimu mkubwa na Serikali hivyo fursa ya
kushirikiana na Serikali ya Italia katika suala hilo imekuja wakati
muafaka.
Aliongeza
kuwa mpango wa kufundisha ya lugha ya kitaliano nao ni muhimu na
unaweza kutekelezwa kupitia Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar-SUZA chini
ya Skuli ya Kiswahili na Lugha za Kigeni katika chuo hicho.
Kwa
hiyo Dk. Shein alimwambia Balozi huyo kuwa Zanzibar inaukaribisha
mpango huo kwa mikono miwili na kupendekeza kuwekwa kwa utaratibu
utakaowezesha utekelezaji wake kwa kuhusisha wizara na mamlaka husika.
Katika
mazungumzo hayo Dk. Shein aliishukuru Serikali na wananchi wa Italia
kwa misaada yao kwa Serikali na wananchi wa Zanzibar.
Alitaja
baadhi ya misaada hiyo ikiwemo kupitia Mfuko wa Maendeleo wa Ulaya
(European Development Fund) ambao Italia ni mwanachama pamoja na Taasisi
ya Ivo De Carneri ya nchi hiyo inayosaidia maabara ya uchunguzi wa magonjwa ya binadamu huko Pemba.
Kuhusu
uhusiano wa kibiashara na Italia Dk. Shein alibainisha kuwa wawekezaji
kutoka Italia hususan katika sekta ya utalii wameifanya sekta hiyo kukua
haraka na kuweza kuchangia sehemu kubwa ya mapato ya Taifa.
Dk.
Shein alimhakikishia Balozi Luigi kuwa Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar itaendelea kufanyakazi na Serikali ya Italia ili kuimarisha
zaidi ushirikiano kati ya nchi mbili hizo.
Balozi
Luigi Scotto kwa upande wake alimueleza Dk. Shein kuwa nchi yake inaupa
umuhimu mkubwa uhusiano wake na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Zanzibar ikiwemo.
Alifafanua
kuwa mbali ya uwekezaji mkubwa uliofanywa na unaoendelea kufanywa na
wananchi wa Italia humu nchini, nchi mbili hizo zina mambo yanayofanana
kama vile sehemu nyingi za kihistoria.
Hivyo
kwa kuwa Italia ina utaalamu na uzoefu mkubwa katika uhifadhi na
ukarabati wa sehemu za historia hivyo alisema Zanzibar inaweza kufaidika
na uhusiano wake na nchi hiyo.
Alieleza
kuwa amefanya safari nyingi Zanzibar kikazi na binafsi na kutembelea
sehemu za historia kama Mji Mkongwe na kugundua kuwa sehemu hizo
zinahitaji ukarabati ili kuendelea kuwa kivutio na pia kudumisha
kumbukumbu hiyo muhimu ya historia ya Zanzibar na ulimwengu.
Balozi
Luigi alisema Serikali ya nchi yake iko tayari kufundisha lugha ya
Kitaliano humu nchini kwa kushirikiana na Taasisi za elimu pamoja na
kuanzisha kituo cha utamaduni cha Italia.
Alisema
kuwa lugha hiyo hivi sasa imepata nafasi kubwa katika kukuza
mawasiliano kati ya wananchi wa Italia na watu wa Zanzibar hadi kufikia
kuwa miongoni mwa lugha zinazotumiwa sana hivi sasa hapa Zanzibar hasa katika sekta ya utalii.
Post a Comment