SHIRIKISHO
la Soka Afrika (CAF) limeikumbusha klabu ya Yanga SC kutomtumia kiungo
Athumani Iddi ‘Chuji’ katika mchezo wake wa Jumamosi dhidi ya Komorozine
ya Comoro, wa Ligi ya Mabingwa Afrika, kwa kuwa bado anatumikia adhabu
ya kadi nyekundu aliyopata kwenye msimu uliopita.
Akizungumza
na waandishi wa habari katika Makao Makuu ya Klabu hiyo mitaa ya
Jangwani leo, Ofisa Habari wa Yanga SC, Baraka Kizuguto, amesema kuwa,
CAF iliwaandikia barua kuwakumbusha kuwa Chuji alipewa kadi nyekundu
mara ya mwisho klabu hiyo ilipocheza michuano ya Afrika katika mechi
dhidi ya Zamalek hivyo Yanga haitamtumia Chuji hadi atakapomaliza adhabu
yake. Aidha
Kizuguto, amesema hawatamtumia mshambuliaji wao, Emmanuel Okwi
,japokuwa CAF imempa leseni ya kucheza michuano hiyo mwaka huu, hadi
hapo Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) litakapotoa baraka zake.
Okwi
amesajiliwa msimu huu Yanga SC kutoka SC Villa ya Uganda baada ya
kugoma kuendelea kuichezea Etoile du Sahel ya Tunisia iliyomsajili kwa
Mkataba wa miaka kutoka Simba SC ya Tanzania pia.
Okwi alifungua kesi Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA)
akilalamika kutolipwa mishahara na Etoile ndipo akaruhusiwa kujiunga na
SC Villa.
Baada
ya Villa kumuuza Yanga ikidai ina haki zote, TFF imeandika barua FIFA
kutaka ufafanuzi kama inaweza kumuidhinisha kucheza Yanga na imeizuia
klabu hiyo kumtumia hadi majibu yapatikane.
Yanga ilitolewa Raundi ya Kwanza katika Ligi ya Mabingwa mwaka 2012
na Zamalek ya Misri, mechi ya kwanza wakilazimishwa sare ya 1-1 Uwanja
wa Taifa, Dar es Salaam Februari 18, na marudiano Machi 3, wakifungwa 1-
0 Cairo.



Post a Comment