JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Katika
baadhi ya magazeti ya leo tarehe 27 Juni, 2014 yameandika taarifa
ambazo sio sahihi likiwemo gazeti la Uhuru lenye kichwa cha habari
“BILA KUPITIA JKT HAKUNA AJIRA SERIKALINI na gazeti la Tanzania Daima
lenye kichwa cha habari “IKULU: RUSHWA YA NGONO IMEKITHIRI SERIKALINI”.
Magazeti
yote haya yameandika habari za kupotosha Umma kuhusu hotuba ya Katibu
Mkuu Kiongozi aliyoitoa tarehe 26/6/2014 katika mkutano wa Mwaka wa
Wakurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Makatibu Tawala uliofanyika
mjini Dodoma. Magazeti hayo yamejenga taswira kwamba Katibu Mkuu
Kiongozi alitoa taarifa kwamba “Hakuna ajira bila kupitia Jeshi la
Kujenga Taifa” na “Rushwa ya ngono imekithiri Serikalini”.
Serikali
inapenda kutoa ufafanuzi kwamba taarifa hizo siyo za kweli wala
hazielezi taarifa halisi aliyoigusia Katibu Mkuu Kiongozi, Mhe. Balozi
Ombeni Sefue. Katika hotuba yake alisema “Aidha, ningependa mjue kuwa
kuanzia sasa tutaweka mkazo mkubwa sana kwenye sifa ya uzalendo kwenye
ajira Serikalini. Hatuwezi kuwa na Watumishi wa Umma ambao hawana
uzalendo.Pale ambapo waombaji kazi kwenye Utumishi wa Umma wana sifa
zote sawa, lakini wakawepo wale ambao wamepitia Jeshi la Kujenga Taifa
watapewa kipaumbele.lakini narudia, kipaumbele hicho kitumike pale tu
ambapo sifa zingine zote ziko sawa, na si vinginevyo”.
Kuhusu
suala la rushwa ya ngono lililoripotiwa na gazeti la Tanzania Daima, si
kweli kwamba Katibu Mkuu Kiongozi alisema kumekuwa na ongezeko au
kukithiri kwa rushwa ya ngono katika utoaji wa ajira serikalini.
Alichokisema Katibu mkuu kiongozi ni kwamba “Lakini bado malalamiko
yanasikika kuwa ati huwezi kuajiriwa kwenye Utumishi wa Umma isipokuwa
kama unajulikana au unatoa rushwa, ama ya fedha au ya ngono. Jambo hilo
linanisononesha sana. Mimi naamini mambo hayo yamepungua sana. Lakini
kama yanafanyika, ni kinyume kabisa na Sera, Sheria, Kanuni na Taratibu
za Utumishi wa Umma na lazima tulio katika ukumbi huu tuyapige vita kwa
bidii zote, bila kuoneana haya, hadi wananchi waone kuwa kweli hayapo.
Tusipuuze hata kidogo malalamiko ya wananchi, bali tujichunguze na
tuchunguzane, ili kama mambo hayo bado yapo, kwa pamoja tuazimie
kuyakomesha kabisa kwenye Utumishi wa Umma”. Hotuba halisi ya Katibu
Mkuu Kiongozi inaweza kupatikana kwenye website ifuatayo www.chiefsecretary.go.tz
IMETOLEWA NA IDARA YA HABARI – MAELEZO
27/6/2014
Post a Comment