JESHI
la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam limezuia maandamano ya baadhi ya
Waislamu yaliyotangazwa kufanyika Novemba mosi na mbili mwaka huu ya kushinikiza
kutolewa rumande kwa Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Sheikh
Issa Ponda.
Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es
Salaam, Suleiman Kova, alisema jana kuwa maandamano hayo ni batili kutokana na
kutopewa baraka na jeshi hilo.
Alisema polisi imejipanga kuwashughulikia wote watakaofanya maandamano katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.
Aidha, alisema Jeshi la Polisi linamsaka mtu
anayechapisha vipeperushi vya kuchochea maandamano ambayo ni hatari kwa
wananchi.
Aliwataka wananchi kuendelea na shughuli za
kiuchumi kutokana na kuimarishwa kwa usalama katika siku hizo ambazo watu hao
wanataka kuandamana kinyume cha sheria.
“Hatutarudi nyuma kwa wale ambao watavunja
sheria na kuvuruga amani ya nchi katika siku hizo mbili,” alisema
Kova.
Kova alisema haki itapatikana mahakamani, hivyo
hakuna haja ya kufanya maandamano katika mahakama hiyo ambayo inasikiliza kesi
ya kiongozi huyo.


Post a Comment