Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

KWELI LOWASSA ANA NGUVU NDANI YA CCM?




Tangu alipojiuzulu kufuatia tuhuma za kutumia madaraka yake vibaya na kusababisha taifa kuingia mkataba mbovu ya Richmond, Edward Lowassa, Waziri Mkuu wa zamani - amebakia kama enigma ndani ya chama chake na kwenye Taifa.
Lakini, vile vile amekuwa ni zaidi ya enigma kwani pia amebakia kama ishara ya mpiganaji asiyekubali kuweka silaha chini, kurudi nyuma au kusalimu amri.
Lowassa tumeambiwa na tumeshuhudiwa ati kuwa ana "nguvu sana ndani ya chama."
Kwamba mara baada ya kujiuzulu, tulidokezwa kuwa Lowassa alikuwa na nguvu sana hasa kwa "wenyeviti wa CCM wa mikoa" na hivyo ana mtandao mkubwa sana na wenye ushawishi (influential) katika ngazi mbalimbali za mikoa.
Pamoja nguvu hiyo kwenye chama tuliambiwa mapema sana mwaka 2008 kuwa Lowassa alikuwa na nguvu sana kwa wakuu wa wilaya ambao wengi waliteuliwa wakati yeye akiwa Waziri Mkuu.
Lowassa pamoja na udhaifu wote aliouonesha katika kushughulikia suala la Richmond bado alikuwa na nguvu sana bungeni.
Kule bungeni tuliambiwa alikuwa na kundi la wabunge ambao waliapa kwake wakiamini kuwa alionewa sana, hivyo mara moja walisimama nyuma yake na kuwa tayari kutumika na kutumiwa naye ili kuhakikisha kuwa anajipanga kuja kulipa kisasi.
Kundi la wabunge hawa ambao nao wengine walikuwa na nguvu ndani ya chama ndio walikuwa usalama wa Lowassa kushindwa kushughulikiwa na Bunge.
Ni kuwa yeye ndiye aliyeligawa Bunge pia - wale walioamini kuwa ametendewa vyema na wale ambao waliamini alionewa na Kamati ya Mwakyembe.
Hawa wa kundi la pili wanaamini kabisa kuwa kosa kubwa la sakata la Richmond lilikuwa linamuangikia Rais Kikwete mwenyewe.



Na hivyo wanaona kuwa Kikwete kushindwa kusimama na Waziri Mkuu wake dhidi ya mashambulizi ya inayojulikana kama "Kambi ya Sitta" ilikuwa ni udhaifu mkubwa.
Kama kulikuwa na utata wa nguvu ya "Kundi la Lowassa' utata huu utakuwa umeondolewa katika sehemu mbili. Kwanza kwenye uchaguzi wa 2010 ambapo baadhi ya maadui zake waliangushwa kwa kutumia nguvu kubwa sana na wengine walitetemeshwa.
Kuanguka kwa Selelii kwa mfano ni ishara tu ya nguvu ya kundi hilo. Lakini zaidi matokeo ya chaguzi za ndani ya chama ambazo zinaelekea kumalizika wiki hii yanadokeza kuwa kweli Lowassa ana nguvu ambazo anahofiwa kuwa nazo. Kama nguvu hizi ni zake mwenyewewa au za kivuli chake tunasubiri kuona.
Kwa muda mrefu tulisikia kuwa kuna mpango wa kutaka kumtenganishia Rais nafasi ya kuwa Mwenyekiti wa CCM na hivyo chama kiongozwe na mtu mwingine asiye Rais.
Tetesi hizi inaonekana kutimia kwani kabla tu ya kuanza kwa mkutano mkuu wa CCM huko Dodoma tetesi hizi zimekuwa kweli ambapo vikaratasi na hoja mbalimbali zimekuwa zikitolewa dhidi ya "Mwenyekiti wa CCM".
Kwa mara ya kwanza Mwenyekiti wa CCM nafasi ambayo ilikuwa na nguvu sana huko nyuma inaonekana kuweza kuulizwa, kukataliwa, na kubezwa. Kwa mara ya kwanza Mwenyekiti wa CCM anashambuliwa na wanachama wa chama chake na tusije kushangaa kuwa hata kama atashinda ushindi wake unaweza ukawa kwenye usawa wa chini ya asilimia 60 za wajumbe.
Baadhi ya Mawaziri na wana CCM wengine ambao walijipambanua kuwa wanapiga vita ufisadi nguvu yao inaonekana haipo. Wameshindwa kusimamia "kujivua gamba" na wote wameshindwa kutetea CCM dhidi ya ufisadi.
Kama nilivyoondika miezi kadhaa huko nyuma kusema Lowassa asijiuzulu tuone wana CCM watafamfanya nini na ukweli ni kuwa Lowassa, Chenge, na wanachama wengine ambao wamehusishwa na vitendo vya ufisadi wamegangamala ndani ya CCM na hakuna aliyethubutu kuwaondoa.
Chombo pekee bila ya shaka cha kuweza kuwaondoa bila nafasi ya kukata rufaa ni Mkutano Mkuu wa CCM (ambao unaendelea) na kama huu utashindwa kuchukua hatua dhidi ya wanachama wake wanaotuhumiwa ufisadi basi tutakuwa na ushahidi mkubwa tu kuwa CCM siyo sawa na chama cha Kikomunisti cha China.
Kule China kulikuwepo na mwanasiasa mashuhuri sana ambaye kama mambo yasingegeuka kinyumenyume ndiye alikuwa anaandaliwa kuja kurithi kiti cha Hu Jintao RAis wa China na Mwenyekiti wa CCP.
Bo Xilai alikuwa ni mwanasiasa aliyeibuka na kupata umaarufu mkubwa kutokana na siasa zake za mrengo wa kushoto na akipendwa na maelfu ya watu. Lakini sifa zake zote zimekuja kutoweka mara moja baada ya yeye mwenyewe kuhusishwa na vitendo vya ufisadi na mke wake kushtakiwa kwa mauaji ya mfanyabiashara wa Kiingereza.
Hatimaye Bo aliondolewa katika nafasi mbalimbali za chama na wiki chache zilizopita kabla tu ya Mkutano Mkuu wa CCP (Kama huu wa CCM) Bo alitimuliwa kutoka kwenye chama na kuna uhakika wa kutosha tu kuwa atashtakiwa kwa makosa ya kihalifu.
CCM siyo CCP kwani japo wanachama wake kadhaa wa ngazi za juu wameshashtakiwa na kuhusishwa na ufisadi hakuna hata mmoja aliyevuliwa uanachama!
Kushindwa kwa CCM kujivua gamba kunathibitisha kile kilichosemwa na wengine gamba limeganda; haliganduki. Na kushindwa huku kunatokana kwa kiasi kikubwa na kushindwa kwa mifumo ya CCM kwani karibu kila anayetakiwa kumsafisha mwenzie yeye mwenyewe ni mchafu.
Katika uchangu huu hata Mwenyekiti wa CCM na familia yake hawajaachwa nje na hivyo kuthibitisha tu hakuna mtu wa kuweza kumsafisha mwingine. Na hapa ndipo ilipo siri ya nguvu ya Lowassa na kundi lake.
Miezi kadhaa huko nyuma niliwahi kuzungumza na mmoja wa watu wa karibu sana na Lowassa ambaye aliniambia neno lile lile - kwani nani msafi ndani ya CCM Mwanakijiji? aliniuliza.
Inawezakana wapo wasafi ndani ya CCM lakini kama wapo hawana nguvu. Nguvu walizonazo ama zinatokana na nafasi zao na siyo na kanuni walizonao.
Kwa mfano, mtu ambaye ni waziri anaweza kuwa na nguvu kwa kadiri ya kwamba ni waziri akitoka uwaziri anakuwa kimya. Nje ya madaraka hakuna wana CCM wenye ujasiri wa kupambana na ufisadi. Hapa ndio crux of the matter ipo.
Ni wana CCM gani wanaweza kusema wanataka chama kisafishike bila ya wao wenyewe kujiletea matatizo? Wale waliojitokeza kupambana na ufisadi walijikuta wamewekwa alama ya kushughulikiwa.
Kama kweli Lowassa ana nguvu hiyo ambayo anadaiwa kuwa nayo - wengine wanasema ana nguvu hadi ndani ya Usalama wa Taifa - basi yumkini ndiye mtu anayeweza kuja kuwa Rais baadaye. Na atakuja kuwa Rais si kwa sababu ya nguvu alizonazo bali kwa vile anaogopwa.
Fikiria kuwa badala ya uwepo wa vipeperushi dhidi ya watuhumiwa wa ufisadi kuna vipeperushi dhidi ya Mwenyekiti wa CCM! Kama ni hivi basi CCM inabidi imwachie Lowassa chama na wale wengine watoke maana sioni uwezekano wa hawa kukaa pamoja.
Kuna njia moja tu ya kumzuia Lowassa na timu yake kuja kushika madaraka ya Taifa; njia ambapo itahakikisha kuwa CCM inasafishwa kweli kweli.
Njia hii bila ya shaka inahusiana moja kwa moja na wana CCM kuukataa ufisadi, ahadi za ufisadi, mafao ya ufisadi na utegemezi wa ufisadi. Kwa vile hili ni gumu kama tulivyoliona inaonekana njia sasa ni nyeupe kwa Lowassa na timu yake kujikita ndani ya CCM kuelekea uchaguzi mkuu wa 2015.
Lakini haya yote yanatufanya tujiulize: Kama Lowassa ambaye alivunja sheria kadha wa kadha wakati wa suala la Richmond, aliyejiuzulu kwa kashfa na ambaye hakuwa na nafasi yoyote ndani ya chama ameweza kuwa nguvu kubwa ndani ya CCM namna hii ina maana CCM ina matatizo makubwa zaidi siyo? Ina maana uadilifu umegonga mwamba na ufisadi umetamalaki.
Kuna nafasi moja tu iliyobakia kwa CCM kushughulikia ufisadi na mafisadi ndani ya chama hicho - kupitia Mkutano huu Mkuu. Wakishindwa hawa, na kama makuwadi wa ufisadi wakipata majukwaa na wakasimama bila kujeruhiwa basi CCM itakuwa imejiroga yenyewe na Watanzania watakao mabadiliko watashukuru.
Kwa sisi wengine tunaombea CCM iendelee kushindwa kushughulikia ufisadi na mafisadi kwani hii ndio njia rahisi zaidi ya kukiondoa madarakani. Kushindwa kwa CCM kujisafisha ni dalili kuwa CCM ya sasa siyo "ile".
Ni kushindwa kwa Mwenyekiti wa CCM (labda ni kweli anatakiwa ang'oke); ni kushindwa kwa Kamati ya Maadili ya CCM na ni kushindwa kwa wanachama waadilifu ambao wamebakia kutoa matamko na malalamiko.
Tulivyoona kwenye uchaguzi wa Mwenyekiti na jinsi nguvu kubwa aliyotumia mzee Makamba kumpigia debe (kumwombea) Rais Kikwete ni wazi kulikuwa na hofu kubwa sana ya kura za maruhani. Kiasi cha kufikia utaratibu kubadilishwa ili kuweza kubaini ni mikoa gani itapiga zaidi kura za maruhani hofu ya Lowassa ni kubwa zaidi.
Tulioangalia upigaji kura imeshangaza kuona kuwa CCM imeshindwa kuendesha uchaguzi mzuri wa Mwenyekiti na badala yake ilikuwa ni kama kura sokoni. Je uchaguzi ulikuwa wa haki na huru? Kama Kikwete anakubalika na kupendwa sana na amefanya mengi kwanini kulikuwa na hofu ya yeye kukataliwa?
Ndio maana naamini hofu ya Lowassa na kundi iko ndani ya CCM tu na mkutano huu umethibitisha kuwa kweli ana nguvu ndani ya hicho chama japo siyo nguvu timilifu kama inavyodhaniwa.
Lakini kama kuna watu nje ya CCM wenye kuihofia "nguvu ya Lowassa" na kwamba wanatetemeka jina lake likitajwa au wanatafuta kupiga magoti mbele zake basi Lowassa ana nguvu kubwa katika pysche ya taifa.

Chanzo: Tanzania Daima
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top