Serikali imefuta leseni za uchimbaji kwa Kampuni ya Uchimbaji wa Dhahabu ya
Aureus Limited iliyopo jijini Mwanza, baada ya kubainika kuficha taarifa za
mauzo ya madini hayo na kuikosesha mapato yenye thamani ya Sh. bilioni 10.7.
Aidha, Mmiliki wa kampuni hiyo ambaye anaishi
Barcelona nchini Hispania, Marc Rene Roelandts, aliyekuwa anasakwa na serikali
kwa tuhuma hizo amekamatwa na kurejeshwa nchini ili kujibu mashtaka
yanayomkabili.
Akizungumza na NIPASHE mjini Dodoma, Naibu Waziri
wa Nishati na Madini, Stephen Masele, aalisema watuhumiwa hao watafikishwa
mahakamani wakati wowote kuanzia sasa.
“Jalada lipo kwa Mwendesha Mashtaka Mkuu wa
Serikali (DPP), hawa wote watatu watapelekwa mahakamani wakati wowote kuanzia
sasa baada ya DPP kutoa kibali cha kushtakiwa kwa watu hao,” alisema.
Aliwataja wanaotarajiwa kufikishwa makamani wakati
wowote kuwa ni raia wa Uholanzi ambaye ni kiongozi wa shughuli zote za kampuni
hiyo, David Gommeren (43); raia Afrika Kusini ambaye ni Mkuu wa Uzalishaji wa
Kampuni hiyo, Gidion Ludwick) na raia wa Israel, Andrey Vash (44).
Septemba mwaka huu, Masele alisema Roelandts
anamiliki hisa moja na Kampuni ya MS Quaester Limited ya Mauritius inayomiliki
hisa 999.
Alisema kampuni hiyo inamiliki mitambo miwili ya
uchenjuaji ambayo ipo katika kijiji cha Nyarugusu wilayani Geita na mtambo wa
pili upo Nyakato jijini Mwanza.
Masele alisema Agosti hadi Septemba mwaka jana,
Wakala wa Ukaguzi wa Madini Nchini (TMAA) ulifanya ukaguzi wa hesabu za fedha
kwa kampuni hiyo ambayo zamani ilikuwa ikijulikana kama Minextech ambayo ni
Kampuni ya uchenjuaji wa marudio ya dhahabu kwa wachimbaji wadogo kwa kutumia
teknolojia ya Kemikali ya Sayanaidi.
“Ukaguzi huo uligundua kasoro kadhaa
zilizoikosesha serikali mapato ikiwamo Kampuni ya Minextech kuficha taarifa zake
za mauzo ya dhahabu kiasi cha kilo 63.27 yenye thamani ya Sh. 2,763,426,787
katika kipindi cha kuanzia mwaka 2006 hadi 2010,” alisema.
Alisema udanganyifu huo ulibainika baada ya
kulinganisha na taarifa za mauzo ya dhahabu zilizowasilishwa serikali na kampuni
hiyo katika kipindi husika.
“Kampuni ya Minetech kutolipa kiasi cha Shilingi
9,085,031,656 kama VAT (Kodi ya ongezeko la thamani), ya mauzo ya dhahabu katika
kipindi cha mwaka 2006 hadi 2010.”
Alisema pia kampuni hiyo ilibainika kutolipa Sh.
252,683,678 kama kodi ya mishahara (Paye) katika kipindi cha kuanzia mwaka 2006
hadi 2010.
Aidha, kampuni hiyo ilibainika kutolipa mrabaha wa
Sh. 371,026,716 katika kipindi cha kati ya mwaka 2006 hadi 2010.
Masele alisema hatua stahiki zinaendelea
kuchukuliwa na serikali ili kuhakikisha malipo hayo yanafanyika.
“Serikali imechukua hatau za awali za kuhakikisha
kuwa wahusika wote wanakamatwa na kufunguliwa mashitaka. Tayari viongozi wakuu
wa kampuni hiyo wapo mikononi mwa Jeshi la Polisi na uchunguzi zaidi unaendelea
kabla ya serikali kuchukua hatua zinazostahili,” alisema na kuongeza:
“Tukio hili linadhihirisha wazi kuwa Kampuni ya
Aureus Limited ilikuwa imekusudia kuficha kiasi halisi cha uzalishaji wake kwa
lengo la ukwepa kulipa mrahaba na kodi stahiki.”
Alisema hatua zitakazochukuliwa hatua za kisheria
ikiwamo kufutiwa leseni na kutaifishwa kwa mgodi huo.
Aliongeza kuwa serikali imejipanga vizuri kubaini
na kuwachukulia hatua za kisheria wale wote wanaojihusisha na udanganyifu katika
shughuli za uzalishaji na biashara ya madini nchini.
“Wote watakaopatikana kutenda kosa hilo
watachukuliwa hatua kazi za kisheria ikiwa pamoja na kufutiwa leseni zao na
kuzuiliwa kujishughulisha na shughuli za madini hapa nchini,” alisema.
Aidha, alisema wawekezaji hao walikuwa
wakituhumiwa kuwadharau viongozi wa serikali, kutoa lugha za matusi kwa nyakati
tofauti ikiwamo wakati Waziri wa Mambo ya Mambo ya Ndani ya Nchi (sasa Ulinzi na
Jeshi la Kujenga Taifa), Shamsi Vuai Nahodha, alipoutembelea mgodi huo.
Kadhalika, wawekezaji hao wanadaiwa kwa makusudi
kukiuka makubaliano kati yake na serikali yaliyofikiwa kwa lengo la kudhibiti
shughuli zake za uzalishaji.
Alisema Septemba 9 mwaka huu, kwa kuwadanganya
wakaguzi kuwa wasingefanya uzalishaji wa dhahabu siku hiyo na badala yake
wangefanya Septemba 10, mwaka huu.
Hata hivyo, wakaguzi hao waligundua kuwa
kulifanyika uzalishaji Septemba 9, mwaka huu baada ya kuambiwa na wafanyakazi wa
kampuni hiyo.
Hatua hiyo ilifikiwa baada ya wabunge kulalamikia
kampuni hiyo kutorosha nje madini hayo.
Mbunge wa Wawi (CUF), Hamad Rashid Mohamed,
aliwahi kulieleza Bunge kuwa kampuni hiyo imekuwa ikizalisha wastani wa kilo 15
kwa wiki na kuzitorosha nje ya nchi bila kulipa kodi kwa serikali.
Masele alisema kufuatia tuhuma hiyo, Wizara
kupitia TMAA ilichukua hatua za haraka kwa kuweka usimamizi makini wa shughuli
za uzalishaji za kampuni hiyo ili kubaini ukweli.
CHANZO: NIPASHE


Post a Comment