|  | 
| Bwalya | 
KALUSHA 
BWALYA:
SAHAU kuhusu 
Zambia iliyochukua Kombe a Challenge mwaka 2006, wakati huo imekwishajitoa 
katika nchi wanachama wa Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati 
(CECAFA) na kuingia nchi za Kusini mwa Afrika (COSAFA).
Zambia 
iliyotikisa katika soka ya Afrika Mashariki na kati ni ile iliyokuwa ikiitwa KK 
Eleven kuanzia miaka ya 1970 hadi 1990 mwanzoni, kabla ya ajali ya ndege iliyoua 
nyota wa kikosi hicho pwani ya Gabon mwaka 1993.
Kalusha 
Bwalya alikuwa katika orodha ya wachezaji waliotakiwa kuingia kwenye ndege 
iliyopata ajali, lakini bahati nzuri kwake alisema atatokea kwenye klabu yake 
moja kwa moja Ulaya kwenda Tunisia, hivyo akanusurika.
Katika 
historia yake ya ushiriki wa Challenge, KK Eleven ilibeba taji hilo mwaka 1984 
na 1991 ambao, Kalusha Bwalya aliungana na Majid Musisi katika ufungaji bora, 
kila mmoja akifunga mabao yake matatu.
Challenge ya 
mwisho kwa Bwalya ilikuwa mwaka 1992 mjini Mwanza, alipoiongoza Zambia hadi Nusu 
Fainali ilipotolewa na Uganda kwa penalti 4-2, Uwanja wa CCM Kirumba kufuatia 
sare ya bila kufungana ndani ya dakika 120.
Huwezi 
kuizungumzia historia ya Challenge bila ya kumtaja Bwalya, aliyezaliwa Agosti 
16, mwaka 1963 mjini Mufulira, kwani enzi zake alikuwa mkali haswa. 
Huyo ni 
mchezaji aliyeichezea Zambia mechi nyingi zaidi na kuifungia mabao mengi zaidi 
pia kuliko mchezaji yoyote hadi sasa. Ndiye mchezaji babu kubwa zaidi kuwahi 
kutokea katika ardhi ya Zambia. Unamzungumzia Mwanasoka Bora wa Afrika mwaka 
1988, ambaye mwaka 1996 aliingia kwenye kinyang’anyiro cha tuzo ya Mwanasoka 
Bora wa Dunia, ambayo ilichukuliwa na Mwafrika mwenzake, George 
Weah.
|  | 
| Omondi Philip | 
UGANDA ndio 
mabingwa wa kihistoria wa michuano ya Challenge, wakiwa wamebeba Kombe hilo 
mara 12 (1973, 1976, 
1977, 1989, 1990, 1992, 1996, 2000, 2003, 2008, 2009 na 
2011).
Wapo 
wachezaji wawili ambao huwezi kuwatenganisha na mafanikio ya The Cranes katika 
Challenge. Akina nani hao? 
Wote hawa 
wamekwishatangulia mbale ya haki hivi sasa, Philip Omondi na Majjid 
Musisi.
Phillip 
Omondi aliyezaliwa mwaka 1957 na kufariki dunia Aprili 21, mwaka 1999 huyu 
alikuwa mtu hatari sana enzi zake na waliobahatika kumuona wanaweza kukiri juu 
ya hilo.
Omondi 
aliyechezea klabu ya Kampala City Council FC kuanzia mwaka 1973 hadi 1979, 
alipotimkia Sharjah ya Falme za Kiarabu (UAE) alikuwa shukaa wa Uganda hadi 
kwenye Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika.
Omondi 
aliichezea The Cranes katika fainali za Afrika miaka ya 1974, 1976 na za 1978, 
ambazo pamoja na kuifikisha Cranes fainali, pia aliibuka mfungaji 
bora.
Kwenye 
Challenge, Omondi aliisaidia mno Uganda kutwaa mataji ya mwaka 1973 na 
1977.
Katika 
fainali za mwaka 1978, mkali wa mabao wa zamani wa Uganda, Phillip Omondi 
aliungana na Opoku Afriyie na Segun Odegbami katika ufungaji bora, kila mmoja 
akipachika nyavuni mabao matatu. Leo Omondi hayupo duniani, lakini huwezi 
kuzungumzia historia ya Challenge bila kumtaja yeye.
|  | 
| Musisi | 
MAJID 
MUSISI:
NI kweli, 
Philipo Omondi alikuwa noma enzi zake, lakini unaweza kusema nini kuhusu Majid 
Musisi Mukiibi?
Mshambuliaji 
huyo aliyezaliwa Septemba 15, mwaka 1967 kabla ya kufariki dunia Decemba 13, 
mwaka 2005 vyombo vya habari Uganda vimechekecha vikaamua kuweka bayana, huyo 
ndiye mchezaji bora zaidi kihistoria kuwahi kutokea nchini humo.
Musisi, 
ambaye ni mchezaji wa kwanza wa Uganda kucheza soka ya kulipwa Ulaya, alikuwa 
ana majina mawili maarufu ya utani enzi zake, ambayo ni Tyson na Magic. Tyson 
kwa sababu alikuwa mkorofi na Magic ni kwamba soka yake iliitwa ya 
miujiza.
Huyo 
aliisaidia The Cranes kutwaa Kombe la Challenge katika miaka ya 1989 na 1990. 
Mfumo wa maisha ya kuendekeza pombe, ulimfanya afananishwe na magwiji wa soka 
duniani akina George Best, Eric Cantona au Paul Gascoigne ‘Gazza’.
Musisi 
alikuwa ana utajiri miguuni mwake na mabeki kwa pamoja na makipa walikuwa 
wanamheshimu sana mtu huyo. Alikuwa hashindwi kufanya jambo anapoamua kufanya 
kwa juhudi zake zote.
Umaarufu 
wake uliwavutia vijana wengi kucheza soka Uganda na Afrika Mashariki kwa ujumla. 
Jamaa alikuwa anaijua soka. 
|  | 
| Nteze John | 
NTEZE 
JOHN:
WENGINE 
wanaweza kujiuliza kwa nini siyo Sunday Manara ama Zamoyoni Mogella, Peter Tino 
au Edibily Lunyamila, lakini jibu ni kwamba, wote hao hawafui dafu mbele ya 
Nteze John Lungu kwa kufanya vitu vikubwa kwenye Kombe la 
Challenge.
Haimaanishi 
Nteze alikuwa anawazidi kisoka akina Abdallah Kibadeni, Mogella, Lunyamila, Said 
Mwamba Kizota na wengine waliowahi kuwika katika soka ya Tanzania, la hasha- ila 
Nteze aling’ara zaidi yao kwenye michuano hiyo.
Huyo ndiye 
aliyekuwa shujaa wetu wakati tunachukua taji la pili la michuano hiyo, mwaka 
1994 mjini Nairobi, Kenya.
Mabao yake 
manne aliyofunga katika Kundi A, kwenye michuano hiyo yaliifanya Tanzania Bara 
iongoze kundi hilo kwa pointi tisa ilizokusanya kutoka na kushinda mechi zote za 
kundi lake, Nteze akifunga katika kila mechi.
Novemba 29, 
Tanzania ikiitandika Somalia mabao 4-0, Nteze alifunga mabao mawili katika 
dakika za 11 na 84, mengine yakifungwa na George Masatu dakika ya 67 na Madaraka 
Suleiman dakika ya 74.
Siku mbili 
baadaye Nteze alifunga bao pekee la ushindi dakika ya 57, Bara ikiwafunga 
wenyeji Kenya 1-0, wakati Desemba 3, Bara ikiichapa Djibouti 3-0, Nteze alifunga 
la tatu dakika ya 75, baada ya Edward Chumila (sasa marehemu) kufunga dakika ya 
pili na Clement Kahabuka dakika ya 30.
Nteze 
hakufunga katika mechi mbili zilizofuata, Nusu Fainali dhidi ya Eritrea, bao 
pekee la Said Mwamba ‘Kizota’ dakika ya saba likiipa Bara ushindi wa 1-0 na 
fainali, ambayo baada ya sare ya 2-2 ndani ya dakika 120 dhidi ya Uganda, Bara 
ilifanikiwa kutwaa Kombe kwa mikwaju ya penalti 4-3.
Ilikuwa ni 
Desemba 10, wakati mabao ya Stars yalipotiwa kimiani na Juma Amir Maftah dakika 
ya 14 na Kizota dakika ya 40 wakati Iddi Batambuze aliifungia Uganda dakika ya 
47 kabla ya George Ssemogerere dakika ya 88 kusawazisha. 
Nteze 
aliibuka pia mfungaji bora wa michuano hiyo kwa mabao yake manne na kutwaa Kiatu 
cha Dhahabu.
|  | 
| Oliech | 
DENNIS 
OLIECH:
WAMETOKEA 
wanasoka wengi Kenya ambao waling’ara kwenye Challenge, lakini kama ilivyo kwa 
wachezaji wa Tanzania unahitajika utulivu wa hali ya juu, ili kumtaja mmoja 
ambaye daima anastahili kukumbukwa katika historia ya michuano hiyo.  
Mfungaji wa 
bao la tatu na la ushindi katika dakika ya 72 ya fainali ya Kombe la Challenge 
Desemba 14, mwaka 2002 Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza, Tanzania Bara ikilala 
3-2 na kupoteza matumaini ya kutwaa taji hilo kwa mara ya tatu.
Nani zaidi 
ya Dennis Oliech. Na kwa nini asahaulike mtu huyo siyo tu kwa kuwakomoa wenyeji 
na kuwapokonya tonge mdomoni, bali soka yake iliyomuuza Ulaya 
baadaye.
Siku hiyo, 
Emmanuel Gabriel alitangulia kuifungia Bara dakika ya 28, kabla ya Paul Oyuga 
kusawazisha dakika ya 30 na Mecky Mexime kufunga la pili kwa penalti dakika ya 
59 na John Barasa kuisawazishia Harambee Stars dakika ya 70 na Oliech kupiga la 
ushindi dakika ya 72.
Oliech 
alikuwa mfungaji bora katika fainali hizo kutokana na mabao yake matano, akiwa 
ana umri wa miaka 17 tu wakati huo.
Oliech 
alizaliwa Februari 2, mwaka 1985, baada ya kung’ara kwenye fainali hizo, mwaka 
2003 alinunuliwa na Al-Arabi ya Qatar hadi mwaka 2005, aliposaini mkataba wa 
miaka minne na  FC Nantes ya Ufaransa na kuanza safari yake kuogelea kwenye 
bwala la fedha Ulaya na sasa anachezea Auxerre.
Aliiwezesha 
Kenya kukata tiketi ya kucheza Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika mwaka 2004 
na alicheza vizuri kwenye fainali hizo nchini Tunisia na mwaka huo huo 
akatabiriwa kuwa miongoni mwa washambuliaji hatari baadaye duniani, akiwekwa 
katika orodha moja na Wayne Rooney wa Manchester United. Oliech kwa sasa ameipa 
kisogo michuano ya Challenge, ingawa bado anaichezea Harambee Stars katika 
michuano mikubwa, ila Challenge ndio iliyomtoa.

 

 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
Post a Comment