Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

TANZANIA YAHITAJI SANA VIONGOZI WENYE UWEZO, TABIA, HAIBA NA KARAMA KAMA ZA MWALIMU JULIUS KAMBARAGE NYERERE

     Na Akili Philipo                                                 "…Kwa hiyo jambo mojawapo lililo ndani ya Serikali ni kukataa makuu ya Nchi bila ya kuwepo maisha bora kwa raia wake, na pia kukataa kutafuta utajiri wa kuchezea. Ndiyo kuikubali imani kwamba kuna vitu vingine vingi vyenye maana zaidi maishani kuliko kujaza utajiri, na kama kutafuta utajiri kunakwenda kinyume cha vitu kama heshima ya binadamu, au usawa wa hali ya maisha, basi jambo litakarofikiriwa kwanza litakuwa heshima na usawa wa binadamu. Maana katika nchi ya Tanzania, Serikali imeanza kutimiza shabaha ya utaratibu wote wa maisha, uchumi na siasa, lazima iwe binadamu; yaani raia, raia wote, wa nchi hii. Kuongeza mali ni jambo zuri, na ni wajibu wetu kuongeza mali. Lakini faida ya mali hiyo itatoweka wakati itakapokoma kuwatumikia watu na kuanza kutumikiwa na watu. Katika hali yetu ya sasa ya uchumi, jambo hili linaweza likaonekana kama jambo la vitabuni tu; lakini kwa kweli ni jambo kubwa sana. Kwa sababu tunasema kwamba kuna baadhi ya vitendo ambavyo tutakataa kufanya au kuvikubali, kila mtu binafsi au Taifa zima, hata kama matokeo ya vitendo hivyo vingeleta maongezeko ya uchumi. Kwa mfano, hata kama ni kweli kwamba yangepatikana maongezeko makubwa sana ya hesabu ya utajiri wa nchi na mapato ya watu wetu walio wengi, kama nchi ya nje, au mabepari wangelima mashamba makubwa, wangeleta, au kuanzisha makampuni au kujenga viwanda vikubwa na vidogo, n.k. (na mimi nina shaka na ukweli huo), bado tungekataa mapendekezo hayo. Tungeyakataa kwa sababu ya matokeo yake kwa uhuru wetu, na kwa sababu idadi kubwa ya watu wetu watapata ujira mdogo sana, watakuwa vibarua wa nchi  nyingine au wa mtu mwingine. Katika hali hiyo riziki na maisha yote ya watu wa Tanzania yatakuwa mikononi mwa nchi nyingine au watu wachache. Lo lote katika haya mawili halitafanana na uamuzi wetu wa kuulinda uhuru wa Tanzania, na uhuru na usawa wa raia wake wote. Lakini hayo maana yake si kusema kwamba tumekubali hali tulio nayo hivi sasa; hata kidogo. Serikali inataka watu wafanye juhudi kubwa kuinua hali ya maisha yao. Tunasema kwamba mambo yaliyozichukua nchi kubwa miaka mia nyingi kutimiza, sisi tutachukua miaka michache tu. Tunachojitahidi kufanya ni kufanya mapinduzi ya haraka ya maisha yetu na uchumi wetu. Hili si jambo lisilowezekana kwa binadamu. Imechukua miaka mamia ya milioni kwa maisha ya ulimwengu kubadilika kutoka katika hali ya vidudu kufikia hali ya juu ya maisha yaani binadamu. Lakini mimba inapita katika hatua zake zote mnamo miezi  tisa tu. Kuongezeka kwa uchumi wa Taifa letu kunaweza kukaharakishwa, na bado kukabaki kuwa ni kwetu. Itachukua zaidi ya miezi tisa, lakini wananchi wakitumia raslimali zao, ardhi yao kwa kutumia ujuzi uliopo wa karne hii, tuna hakika ya kupunguza sana muda ambao nchi kama Uingereza au Marekani zimechukua kufikia hali yao ya sasa. Wananchi wa Tanzania wenyewe tu ndio wanaoweza kuwa na dhati ya kutosha kuijenga Tanzania, kwa faida ya Watanzania; na ni Watanzania tu ndio wanaoweza kusema faida hizo ni zipi, kwa hiyo hatuna budi kujitegemea sisi na amali yetu wenyewe katika kuleta maendeleo. Amali hizo ni ardhi, na watu, fikira zetu zielekezwe katika vitu tulivyo navyo, au vinavyoweza kupatikana, kwa gharama ndogo, na ambavyo vinaweza kutumiwa na wananchi. Tukiendelea kwa njia hii tunaweza kuepuka kuharibu utaratibu na kuepuka shida za binadamu. Wakati huo huo tunaweza tukajenga viwanda na huduma katika vijiji, ambako ndiko watu wengi waliko, na hivyo tukasaidia kuendeleza uchumi vijijini. Kwa njia hiyo watu wengi zaidi wanaweza kupata maongezeko ya mapato yao, badala ya kukazania kuongeza uchumi uliomo mikononi mwa watu wachache. Fedha tulizo nazo lazima zitumiwe kuleta faida kubwa, katika kununua mbolea, vitu muhimu kwa maendeleo, kuwakopesha watu wanunue ng’ombe wazuri, kuboresha, kuzalisha amali; katika kuunda utaratibu bora zaidi wa uchumi, na vitu vingine kama hivyo. Mambo hayo yataleta maongezeko makubwa katika pato la mwananchi. Wala maneno haya maana yake siyo kwamba hakutakuwa tena na maendeleo ya mijini, au kwamba sasa hatutajenga viwanda vipya. Watu wengi wanapoishi pamoja, huduma Fulani huwa za lazima kwa sababu ya afya na usalama wa watu. Tutakuwa wajinga tukisahau miji, ambayo ndiyo inayotoa huduma za kusaidia vijiji vinavyoizunguka. Viwanda vinavyoifaidia nchi nzima lazima vijengwe katika sehemu zinazofaa. Lakini hata wakati tunapojenga viwanda vinavyoifaidia taifa zima, hatuna budi kufikiria kama ni lazima kwetu kutumia mitambo ya kisasa. Hatuna budi kufikiria kama mitambo ya aina ya zamani, inayohitaji wafanya kazi wengi zaidi, wasiohitajiwa kuwa na ufundi mkubwa, haiwezi kutufaa kutimiza haja yetu, na vile vile gharama yake tukaimudu. Lakini ziko njia mbili ambazo kwazo wito wetu wa kujitegemea umeeleweka vibaya, au watu wamekataa kuuelewa makusudi. Kujitegemea maana yake siyo kujitenga ama katika mambo ya uchumi, ama katika mambo ya siasa. Maana yake ni kwamba tutajitegemea wenyewe, hatuwategemei watu wengine. Lakini kusema hivyo si sawa na kusema kwamba hatutafanya biashara na watu wengine, au kwamba hatutashirikiana nao, kama ushirikiano huo unatuletea faida. Ni dhahiri kwamba tutafanya hivyo; lazima tutaendelea kuuza bidhaa zetu za kutosha katika nchi za nje kutuwezesha kulipia vifaa tunavyovipata. Mpaka sasa hivyo ndivyo Tanzania inavyofanya; na kwa kweli, kwa miaka mingi sana thamani ya bidhaa tulizouza imekuwa ni kubwa zaidi kuliko ile ya vitu tulivyo nunua kutoka nchi za nje. Lazima vitu tunavyonunua viendelee kuwa vile ambavyo ni muhimu kwa maendeleo yetu, muhimu kwa maendeleo na maisha ya watu wetu wote, na ambavyo sisi wenyewe hatuwezi kuvitengeneza. Mpaka sasa tumekuwa tukinunua kutoka nchi za nje vitu vingi ambavyo tungeweza kuvipata mumu humu nchini kwa juhudi kidogo tu. Vitu hivyo ni kama chakula au vitu vya anasa vinavyowafanya watu wetu wachache watamani mambo ambayo hawataridhika nayo kamwe. Yaani kujitegemea hakutatupunguzia biashara yetu na mataifa mengine ulimwenguni. Mambo mengine kuhusu kujitegemea ambayo ni muhimu kuelewa ni kwamba Tanzania haikusema kwamba haitaki msaada kutoka katika nchi za nje kwa kazi zake za mendeleo. Tutaendelea kupokea misaada kutoka nchi za nje kwa ajili ya mipango maalum, au kama inasaidia maendeleo kwa ujumla, basi lazima tupate fedha na wataalamu walio wengi kutoka katika nchi za nje, kutimiza mipango ambayo itaifanya juhudi yetu kuwa na maana zaidi: mahali ambapo mpango huo unasaidia kazi zingine za Tanzania. Hiyo ndiyo sababu iliyofanya Serikali itamke wazi kwamba tutakaribisha misaada kutoka nchi za nje, kama misaada hiyo ni ya Serikali ama ni ya watu binafsi, katika kujengea aina nyingi mbali mbali za viwanda, hasa viwanda vinavyotengeneza vifaa vya kutumia, au kusafisha mazao yetu kabla ya kuuza. Misaada ya elimu ya aina zote ni aina moja ya misaada mingi yenye kutufaidia ambayo nchi za nje zinaweza kutoa, mradi tu msaada huo unafanana na nguvu yetu ya kulipia gharama za kila siku. Lakini jambo lililo muhimu ni kwamba haifai sisi Watanzania kuwa na mawazo kwamba hakuna cho chote tunachoweza kufanya mpaka kwanza mtu mwingine ametupatia fedha. Jambo la maana kwetu ni kiasi tutakachofanikiwa katika kumzuia mtu asimnyonye mwenzake, katika kueneza mtindo wa kufanya kazi pamoja kwa faida ya wote badala ya kila mtu kushindania faida yake binafsi; lakini lililo muhimu zaidi ni kuhakikisha kwamba tunapanua uchumi wetu bila ya kupanua nafasi za mirija ya wanyonyaji. Shabaha yetu haina budi iwe kupata maendeleo kwa njia ambayo itahakikisha kwamba tunatumia utaalamu na maarifa yote ya kisasa, lakini bila ya kueneza ubepari. Maana yake ni kwamba katika Tanzania hatuna budi kulinda na kuimarisha utaratibu wetu wa demokrasi. Lazima tufikie hali ambapo kila mwananchi anahusika katika mambo ya Serikali yake ya kijiji, mtaa na wakati huo huo anapata nafasi ya kushiriki katika mambo ya Serikali ya Taifa lake. Maana yake ni kwamba lazima turekebishe tofauti kubwa ya mapato tulizozirithi kutopka kwa wakoloni, na kuhakikisha kwamba kila mtu anapokea pato linalolingana na juhudi yake katika nchi. Lakini wakati huo huo hatuna budi kuwafikiria wale wenzetu ambao umri wao au udhaifu wa miili yao unawazuia wasiweze kushiriki katika kazi za uchumi. Vile vile lazima tueneze nafasi sawa kwa wananchi wote, mpaka kila mtu aweze kushiriki katika kazi za uchumi katika njia anayoimudu…  " 

          Hiyo ni Sehemu ya Hotuba ya Rais wa Kwanza wa Tanzania, Julius Kambarage Nyerere  katika     Chuo Kikuu Cha Dar Es Salaam.”

 

Julius Kambarage Nyerere alikuwa Kiongozi shupavu, makini, mkweli, muaminifu, muhalisia muadilifu, mjuzi na Mwalimu wa watu wote wa Tanzania, Afrika na Ulimwengu, alitumia maisha yake yote kuwatumikia watu wote, aliweza kupambana na dhuluma na ubaguzi miongoni mwa wanadamu, kwa maana hiyo aliweza kupigania haki, uhuru, umoja, usawa, amani na maendeleo. Nawaomba Watanzania tujitahidi sana kusikiliza na kupata habari zake, na pia kujifunza na kusoma nyaraka zake nyingi, ama alizoweza kuandika yeye mwenyewe binafsi, au zilizoandikwa na watu wengine wengi sana, na zinazoendelea kuandikwa, kwa hakika tutapata elimu kubwa sana, ufahamu mkubwa, na manufaa mazuri sana, tutaweza kufanya maamuzi makini kwa wakati muafaka, tutajikomboa na kuleta mabadiliko makubwa katika uhuru wa kiuchumi, kisiasa na kijamii na kuleta maendeleo na maisha bora kwa watanzania wote. Ninakuomba na ninakusihi sana tumlilie kwa maombi Mungu Mwenyenzi, ili atuinulie viongozi wenye uwezo, tabia, haiba na karama kama Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na timu yake ili waweze kutunusuru na hali hii ya hatari ya migogoro, songombingo, sokomoko na mashaka makubwa, nchini Tanzania, barani Afrika na Ulimwenguni.    




Akili Phillipo

E-Mail:phildeak@hotmail.com

Simu Namba:+255(0)754 262270
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top