Waziri wa
Nishati na Madini, Profesa Sospiter Muhongo, amejigamba kuwa Tanzania
haitadanganyika tena kwa wawekezaji wa sekta ya madini kutolipa kodi na
kuifanya nchi kutofaidika na rasilimali zake.
Alisema hayo baada ya Serikali za Tanzania na Finland, kutiliana saini, makubaliano katika kutafiti na kukuza sekta ya madini.
"Kama ni
kutuibia walifanya hivyo siku za nyuma, lakini kwa sasa hawawezi tena,"
alijigamba Profesa Muhongo akidai historia inaonyesha kuwa nchi zote
zenye rasilimali za madini, mwanzoni zilidanganyika.
Alikiri
kuwa awali wawekezaji katika migodi walikuwa wakijitetea kuwa walikuwa
wanapata hasara lakini kwa sasa, sheria inawalazimisha kulipa asilimia
30.
Kauli ya
Profesa Muhongo ilitokana na waandishi kumbana, kuhusu Watanzania
kutonufaika na sekta ya madini wakati ina faida kubwa.
Profesa Muhongo alisema kwa sasa sekta ya madini inachangia asilimia 3.5 ya pato la Taifa.
Alisema malengo ni kuhakikisha kuwa sekta ya madini inachangia zaidi ya asilimia 10 ifikapo mwaka 2025.
Mapema,
wakurugenzi wa sekta ya madini katika Serikali za Tanzania na Finland,
walitiliana saini ya kukuza na kuendeleza sekta ya madini hapa nchini.
Akizungumzia
makubaliano hayo, Profesa Muhongo alisema yanazingatia mambo matatu,
ambayo ni pamoja na utafiti wa madini katika mikoa ya kusini.
Alisema kimsingi tayari wamegundua kuwa ukanda huo una makaa ya mawe, shaba, niko na platiniamu.
Alisema
watakachokifanya ni kuainisha maeneo yenye madini na viwango halisi ili
wakipatikana wawekezaji wa kuyachimba, waingie kwenye makubaliano ya
uhakika. Chanzo: Mwananchi
Post a Comment