Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

LOWASSA, SUMAYE WATAJWA SAKATA LA UUZWAJI NYUMBA ZA SERIKALI

Uuzwaji wa nyumba za serikali umegeuka mwiba huku wabunge wakiendelea kuhoji hatua zilizochukuliwa kutokana na kadhia hiyo

Hatua hiyo iliyotekelezwa mwaka 2002  hadi 2004 ilizusha malalamiko mengi tangu wakati huo na sasa imeibuka tena bungeni

Akichangia mjadala wa bajeti ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na mawasiliano jana, mbunge wa Nachingwea, Hassani Masala (CCM) alihoji mfumo uliotumika kuuza nyumba za serikali

Alisema haungi mkono kwa vile umesababisha viongozi wapya wa serikali wanaoteuliwa kujikuta wakiishi katika nyumba za wageni.

Mjadala huo uliibuliwa juzi na msemaji wa kambi ya upinzani Bungeni kupitia kwa waziri kivuli wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Godbless Lema kabla ya Mwenyekiti wa Bunge Mussa Azzan Zungu kumtaka kuondoa baadhi ya maneno katika hotuba yake likiweo suala la uuzwaji wa nyumba za serikali.

 Ritha Kabati Amvaa Lowassa
Akichangia mjadala huo jana, Mbunge wa Viti Maalumu (CCM), Ritha Kabati alimtaja aliyekuwa mgombea urais wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Edward Lowassa kuwa alinunua nyumba ya serikali iliyouzwa mwaka 2002 yenye jengo namba 68.

Alisema hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni ilisema nyumba za serikali 7,921 ziliuzwa tangu mwaka 2002 hadi 2004 na kutaka serikali ya awamu ya tano kurejesha nyumba hizo kutokana na walionunua kukiuka mikataba na malengo ya mauzo.

“Naomba niwaambie usiangalie boriti lililo katika jicho la mwenzako wakati kwako lipo, kwani hata mgombea wao wa urais Edward Lowassa alihusika kwa kununua nyumba ya plot namba 68 na Fredrick Sumaye alikuwa Waziri Mkuu na kuhusika kuuza nyumba hizo,” alisema Kabati.

Baada ya kueleza hayo, Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni na Mbunge wa Hai, Freeman Mbowe (Chadema) aliomba kumpa taarifa mbunge huyo kuwa taarifa hiyo ni kwa maslahi ya taifa, hata kama mhusika atakuwa katokea kambi ya upinzani sheria itachukua hatua.

"Kambi ya upinzani tunapoibua jambo huwa linakuwa kwa maslahi ya Taifa, hivyo ni vyema wabunge wote mtambue kuwa kosa likifanywa na kiongozi  ni lazima hatua zichukuliwe bila kujali ni wa Chadema, CUF au CCM.

"Tunapokuwa tunatoa uamuzi kama kambi ina maana sheria ifuate mkondo wake." Alisema Mbowe huku akishangiliwa na wabunge wa UKAWA

Awali katika michango mbalimbali ya wabunge wa upinzani wamekuwa wakilalamikia kuuzwa nyumba hizo za serikali na kudai kuwa watumishi wapya wengi walioajiriwa, wamekuwa wakikosa maeneo ya kuishi.

Mbunge wa Kawe, Halima Mdee (Chadema) akichangia mjadala huo alilalamikia kuuzwa kwa nyumba hizo pamoja na nyingine za Tazara zipatazo 500 na kuamua kumpatia Waziri wa Ujenzi ,Uchukuzi na Mawasiliano ripoti aliyodai inaonesha nyumba hizo zilivyouzwa.
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top