Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

UVCCM WAFIKISHANA POLISI

Sakata la uuzwaji kinyemela wa zaidi ya hekari 200 za shamba la Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM), Mkoa wa Iringa limechukua sura mpya baada ya aliyekuwa katibu wa mkoa huo, Ally Nyawenga kukamatwa na polisi.

Shamba hilo lililopo eneo la Igumbiro, nje kidogo ya mji wa Iringa, linadaiwa kuuzwa mwaka jana kwa zaidi ya Sh800 milioni baada ya baadhi ya viongozi kubadili matumizi yake na kuwa viwanja.

Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa, John Kauga alisema jana kuwa kiongozi huyo alikamatwa Morogoro siku chache zilizopita.

“Tulituma askari wetu na leo hii wanamleta. Taarifa za kumkamata ni hizo za uuzwaji wa shamba hilo kwa hivyo tutafanya naye mahojiano zaidi, lakini kwa sasa sina taarifa zaidi ya hapo labda tuwasiliane kesho (leo),”alisema.

Nyawenga alisimamishwa kazi mwishoni mwa mwaka  jana, akituhumiwa kusimamia uuzwaji wa shamba hilo kinyume cha utaratibu wa jumuiya hiyo. 

Mali zote za jumuiya hiyo zipo chini ya Baraza la Wadhamini, linaloongozwa na Mwenyekiti, Dk Emmanuel Nchimbi.

UVCCM ilianza kumiliki shamba hilo miaka ya 1970 likitumika kwa ajili ya kilimo kwa kukodisha vijana kwa bei nafuu ili kuwasaidia kujiendeleza kiuchumi.

Ally Simba aliyedaiwa kuwa msimamizi wa shamba hilo alikana nafasi hiyo huku akisema hakuhusishwa katika mipango hiyo.

“Sikuwa msimamizi, bali mjumbe tu wa kamati ya utekelezaji, msimamizi alikuwa Katibu wa UVCCM,” alisema Simba ambaye kwa sasa ni Katibu wa UVCCM Wilaya ya Mbinga.

Alisema kabla ya kuondoka Iringa mwaka 2014, hakuwahi kusikia vikao wala mipango ya uuzaji wa shamba hilo na kwamba hahusiki.

Akizungumzia kukamatwa kwa Nyawenga, Katibu wa UVCCM Mkoa wa Iringa, Abdulkarim Halamga alisema: “Kwa sababu ni mali ya vijana na katibu aliyekuwapo anahusika, hivyo kwa kushirikiana na polisi, tumemkamata baada ya waliouziwa viwanja kuanza kutudai huku vijana wakipinga kuuzwa kwa eneo lao. Kwa sababu hakuwa peke yake, taratibu nyingine zitafuatwa akishafikishwa Iringa.”

Mjumbe wa kamati ya utekelezaji ya UVCCM mkoani hapo, Thom Muyinga alisema kuuzwa kwa shamba hilo kumesababisha mpasuko ndani ya umoja huo.“Vijana wanataka mali yao, haiwezekani mali hiyo iuzwe kinyemela na kunufaisha kundi la watu wachache,” alisema.

Mmoja wa vijana hao, Katula Kalinga alisema japo tayari tume ya UVCCM ya kuchunguza mgogoro huo ilishakwenda Iringa, hakuna kinachoendelea.

Alimuomba Rais John Magufuli kufuta hati za viwanja hivyo ili shamba hilo, lirejeshwe kwa UVCCM.

Pia, walimuomba Mwenyekiti wa CCM, Jakaya Kikwete kutumbua majipu yanayokitafuna chama kwenye mkoa huo, ili vijana waendelee kunufaika na mali yao.

Walitaka kamati ya utekelezaji jumuiya hiyo Mkoa wa Iringa isimamishwe wakati uchunguzi ukiendelea.
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top