Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

Ofisi ya Spika yaibiwa



HALI si shwari katika ofisi ndogo za Bunge zilizopo jijini Dar es Salaam, baada ya watu wanaodaiwa kuwa watumishi wa Bunge, kuiba seti ya televisheni ya kisasa (flat screen) ya nchi 42 ndani ya ofisi ya Spika wa Bunge, Anna Makinda, Tanzania Daima Jumatano limebaini.
Habari zinaeleza kuwa watu hao ambao hadi sasa wanaendelea kusakwa, walifungua mlango wa ofisi ya Spika na kuishusha seti hiyo ya televisheni, iliyokuwa ukutani na kutimka nayo.
Habari kutoka ndani ya ofisi hiyo, zilisema kuwa tangu tukio hilo litokee takriban wiki mbili zilizopita, ofisi hiyo imekuwa moto kutokana na msako na uchunguzi unaoendelea kubaini waliohusika, huku watuhumiwa wakubwa wakiwa baadhi ya watumishi wa idara mbalimbali, hasa walinzi wanaofanya kazi katika ofisi hiyo.
Hata hivyo taarifa zingine kutoka ndani ya ofisi hiyo zilisema kuwa jaribio la kutaka kuiba seti hiyo ya televisheni lilikwama kwani mwizi huyo alishindwa kuitoa nje na kuondoka nayo.
“Ukweli ni kwamba kuna mtu au watu walifanya jaribio la kutaka kuiba seti ya televisheni katika ofisi ya Spika kwani alifanikiwa kuharibu kitasa cha mlangoni na kufanikiwa kuingia ndani, lakini pamoja na kufanikiwa kuishusha chini, alishindwa kuitoa kutokana na uzito wake,” kilisema chanzo chetu cha habari.
Kwa mujibu wa habari hizo, haijajulikana kama watu hao walitaka kuchukua televisheni hiyo pekee au na vitu vingine vilivyokuwa ndani ya ofisi hiyo.
Mtoa taarifa wetu, alilieleza gazeti hili kuwa mazingira hayo ya mtu aliyetaka kuiba yanaonyesha kuwa hayakufanywa na mtu wa mbali bali ni wa karibu kabisa na inawezekana na mmoja wa watumishi wa ofisi hiyo hiyo.
Taarifa za awali zinaeleza kuwa, tayari kampuni moja ya ulinzi iliyokuwa inalinda katika ofisi za Bunge za Dar es Salaam na kule bungeni Dodoma imeondolewa.
Alipotafutwa mmoja wa maofisa wa Kitengo cha Habari na Uhusiano wa Kimataifa wa ofisi za Bunge, Prosper Minja, alikiri kuwapo kwa taarifa hizo za wizi katika ofisi za Spika.
“Ni kweli tukio hili nililisikia, lakini lilitokea zamani, tangu wakati ule wa sensa… lakini haijajulikana ni nani aliyetaka kuiba,” alisema Minja..Alipoulizwa juu ya kuwapo kwa taarifa za kufukuzwa kwa moja kati ya kampuni za ulinzi zilizokuwa zikilinda katika ofisi hizo za Bunge na zile za Dodoma, alishindwa kukubali wala kukataa.
Akifafanua kuhusu hilo, alisema anachofahamu yeye ni kwamba Tume ya Maadili inayoundwa na wenyeviti wa kamati za Bunge ndiyo inayoweza kuzungumzia juu ya suala hilo kwa sababu lipo mikononi mwao.
Alisema chini ya tume hiyo kuna kamati ndogondogo ikiwamo ile ya ajira na utumishi ambayo kimsingi inashughulikia ajira zote za watumishi au kampuni zinazopitishwa kufanya kazi katika ofisi za Bunge.
Kwa mujibu wa Minja hata kampuni za ulinzi ajira zao zinapitishwa na kamati hiyo ya ajira na utumishi kwa kushirikiana na Wizara ya Utumishi wa Umma.
“Kama kuna kampuni imefukuzwa basi hilo linaweza kuzungumziwa na kamati hiyo, lakini ninachofahamu mimi ni kwamba kampuni za ulinzi binafsi na nyingine kama zile za usafi zinazoajiriwa chini ya mkataba wa Public Private Partnership (PPP) zinaajiriwa kwa mkataba wa muda fulani.
“Kwa maana hiyo mkataba ukiisha zabuni zinaitishwa upya, kampuni iliyokuwa labda inalinda nayo inalazimika kuomba tena, sasa hapo inaangaliwa kampuni ambayo ni bora zaidi ndiyo inayopewa zabuni… kama imeondolewa inawezekana imeondolewa kwa sababu hiyo, sina uhakika na taarifa ya kampuni ya ulinzi kuondolewa.
“Lakini sidhani kama imeondolewa kwa sababu nilipofika hapa asubuhi mlinzi aliyenifungulia mlango na kunifuata kunisainisha ni yule yule wa siku zote,” alisema Minja.
Habari za Ofisi ya Spika kutaka kuibiwa zimekuja ikiwa ni takriban zaidi ya miaka mitatu tangu ufanyike wizi katika ofisi za aliyekuwa Spika wa Bunge lililopita, Samuel Sitta.
Chanzo: tanzania daima.
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top