………………………………………………………..
Ujumbe wa Serikali ya Qatar
ukiongozwa na Mhe. Zayed bin Rashid Al-Nayemi ambaye pia ni Mkurugenzi
wa Idara ya Mambo ya Amerika katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Qatar,
ulitiliana saini makubaliano ya awali ya ushirikiano katika masuala ya
ajira na Serikali ya Tanzania.
Katika kikao cha mashauriano
baina ya nchi hizi mbili, kilichofanyika tarehe 25 Septemba, 2012 makao
makuu ya Wizara ya Kazi na Ajira ambapo ujumbe wa Serikali uliongozwa na
Katibu Mkuu Wizara ya Kazi na Ajira, Bwana Eric F. Shitindi.
Akizungumza baada ya kutiliana
saini makubaliano ya awali, Katibu Mkuu Wizara ya Kazi na Ajira, Bwana
Eric F. Shitindi alieleza kuwa makubaliano haya yataimarisha juhudi za
Serikali za kupambana na changamoto ya ukosefu wa ajira kwa vijana
nchini.
Aidha, kiongozi wa ujumbe wa
Qatar, Bwana Zayed bin Rashid Al-Nayemi alisema makubaliano haya
waliyotiliana saini yatafungua ukurasa mpya wa ushirikiano baina ya nchi
hizi mbili.
Chini ya makubaliano haya ya
awali, wafanyakazi watakaokwenda kufanya kazi nchini Qatar, watalindwa
na Mkataba wa ushirikiano uliotiwa saini na nchi hizi mbili ambapo pia
kutakuwepo na Tume ya Ushirikiano itakayoundwa na wajumbe kutoka nchi
hizi mbili itakayosimamia makubaliano haya.
Katika kikao hicho, ujumbe wa
Tanzania ulikuwa na Katibu Mkuu Wizara ya Kazi, Uwezeshaji Kiuchumi na
Ushirika Zanzibar, Bibi Asha Ali Abdullah, Kamishna wa Kazi, Bwana Saul
Kinemela, Kaimu Mkurugenzi wa Ajira, Bibi Marietha Mcha, Kaimu
Mkurugenzi wa Idara ya Mashariki ya Kazi, Wizara ya Mambo ya Nje na
Ushirikiano wa Kimataifa, Bwana Christopher Mvula,Bw Eliezer
Mwasele,Mtendaji Mkuu Wakala wa Huduma za ajira Tanzania(TaESA) pamoja
na wataalam mbalimbali kutoka Serikalini.
Kwa upande wa Serikali ya Qatar,
ujumbe huo uliwashirikisha Mshauri wa Masuala ya Sheria, Wizara ya Mambo
ya Nje ya Qatar, Dk. Reyadh Al Qaysi, Mkurugenzi Msaidizi masuala ya
Sheria Wizara ya Kazi Qatar, Mwanasheria Wizara ya Kazi Qatar, Bwana Ali
Al-Hadhrami na Bwana Ali Al-Bader kutoka Wizara ya Mambo ya Nje Qatar.
Makubaliano haya ni rasimu ya
mkataba wa ushirikiano ambapo unatarajiwa kutiwa saini hivi karibuni
baina ya Mawaziri wa nchi hizi mbili.
Nchi ya Qatar ni mojawapo ya
mataifa yanayofanya nchi za Ghuba za Arabuni na ina utajiri mkubwa wa
gesi na mafuta na hivi karibuni ilichaguliwa kuandaa mashindano ya
kandanda ya Kombe la Dunia mwaka 2022.
Imetolewa na
Bw. Ridhiwan Wema
Msemaji-Wizara ya Kazi na Ajira.


Post a Comment