Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

YANGA KUVAANA NA AZAM, TAIFA; SIMBA NA MTIBWA, MOROGORO



Yanga SC

Na Mahmoud Zubeiry
UHONDO wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara unatarajiwa kuendelea leo, ‘Big Three’ zikijitupa uwanjani kuwania pointi za kutengeneza mazingira ya ubingwa mskmu huu.
Mabingwa watetezi, Simba SC watakuwa wageni wa Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro, wakati washindi wa pili wa ligi hiyo msimu uliopita, Azam FC watakuwa wanaonyeshana kazi na washindi wa tatu, Yanga Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Kweli hata mchezo wa Morogoro utavuta hisia za wengi, lakini mchezo mkali zaidi na uliobeba zaidi mustakabali wa msimamo wa Ligi Kuu utakuwa Dar es Salaam.
Yanga na Azam FC kwa sasa ni wapinzani wakubwa- na hapana shaka Watoto wa Jangwani sasa wanaamini uzito wa mechi dhidi ya Wana Lamba Lamba ni sawa na uzito wa mechi dhidi ya mahasimu wao wa jadi, Simba SC.
Na bila shaka ni kwa sababu hiyo, baada ya mechi yao na Mgambo JKT Yanga wakaenda kuweka kambi katika hoteli ya Kiromo, Bagamoyo mkoani Pwani kujiandaa na mchezo wa leo.
Kwa kawaida, Yanga huweka kambi Bagamoyo katikati ya Ligi, inapokuwa inajiandaa na mchezo dhidi ya mahasimu wao wa jadi, Simba SC hivyo kwa kwenda huko kuweka kujiandaa na mchezo huo, maana yake wanaupa uzito sawa na pambano la watani.
Wakati vijana wa Yanga wakiwa Bagamoyo, Kocha Mkuu wa klabu hiyo, Mholanzi Ernie Brandts Alhamisi alikwenda kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, kuifuatilia timu hiyo ilipokuwa ikimenyana na Coastal Union ya Tanga.
Katika mchezo huo, Brandts aliyeambatana na Msaidizi wake, Freddy Felix Minziro alikuwa makini kufuatilia uchezaji wa Azam na kunukuu kwenye kijitabu chake, maana yake alikwenda kufanyia kazi katika mazoezi ya timu yake.
Azam nayo, ina ari mpya baada ya kurejea kwa kocha wake Muingereza, Stewart Hall aliyewapa mafanikio makubwa uliopita.
Stewart amerejea na ‘bonge la zali’ Azam, baada ya kuiongoza timu hiyo kuichapa Coastal mabao 4-1 siku hiyo, ikitoka kuchapwa mabao 3-1 na Simba SC, chini ya kocha aliyefukuzwa baada ya mechi hiyo, Mserbia, Boris Bunjak.
Stewart alifukuzwa Azam Agosti mwaka huu, baada ya kikiuka maagizo ya Bodi ya Ukurugenzi ya klabu, kwa kumpanga Mrisho Ngassa katika Fainali ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki, Kombe la Kagame dhidi ya Yanga. Yanga ilishinda 2-1 na kutwaa Kombe.
Lakini amerejeshwa kufuatia wachezaji wa Azam kuuandikia barua uongozi ya kumkataa Bunjak na kupendekeza Muingereza huyo arejeshwe. Na uongozi wa Azam pia ulizingatia kushuka kwa kiwango cha timu na kukubaliana na pendekezo la wachezaji wake.
Azam itaingia uwanjani ikiwa na kumbukumbu ya ushindi wa 4-1, uliowafanya wafikisha pointi 21, baada ya kucheza mechi 10 na kurejea nafasi ya tatu kwenye msimamo wa Ligi Kuu, nyuma ya Simba na Yanga, zenye pointi 23 zote baada ya kucheza mechi 11, kila timu.
Yanga SC nao watashusha timu yao wakiwa na kumbukumbu ya wimbi la ushindi katika Ligi Kuu ikiwemo mechi ya iliyopita, ambayo waliichapa Mgambo JKT ya Handeni, Tanga mabao 3-0 Jumatano kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kuifikia kwa pointi Simba SC iliyotoa sare ya 1-1 na Polisi mjini Morogoro siku hiyo.
Faraja kwa Yanga ni kurejea kwa wachezaji wake tegemeo, beki Kevin Yondan na mshambuliaji Said Bahanuzi ‘Spider Man’, ambao walikuwa majeruhi. Yondan aliingia kipindi cha pili katika mechi dhidi ya Mgambo, wakati Bahanuzi alipewa mapumziko zaidi, ingawa leo anaweza kupangwa.
Kwa Azam nako, faraja yao mbali na kurejea kwa Stewart, pia ni kurudi kwa mpachika mabao wao tegemeo, John Bocco ‘Adebayor’ aliyekuwa anasumbuliwa na maumivu ya kifundo cha mguu.
Wakati Brandts akionyesha kutilia mkazo mechi hiyo kiasi cha kwenda hadi Chamazi kushuhudia mbinu za wapinzani wake, Stewart naye alisema baada ya mechi ya Coastal wanataka kuwafunga Yanga leo.
Katika mchezo wa leo, bila shaka Stewart hatafanya mabadiliko makubwa kutoka kikosi kilichotandika Coastal 4-1.
Langoni anaweza kuendelea kusimama Mwadini Ally, kulia Samir Hajji, kushoto Ibrahim Shikanda, katikati Aggrey Morris na Said Mourad katika safu ya ulinzi, Jabir Aziz kiungo mkabaji, viungo wa pembeni Kipre Balou na Khamis Mcha ‘Vialli’, kiungo mchezeshaji Salum Abubakar na washambuliaji John Bocco na Kipre Tcheche.
Brandts pia hatarajiwi kuwa na mabadiliko makubwa kwenye kikosi chake leo, kutoka kile kilichoichapa 3-0 Mgambo JKT.
Utata tu utakuwa baada ya kurejea Yondan, Mbuyu Twite atampanga pembeni au ataamua kumuanzishia benchi mmoja kati ya mabeki wake watatu wa kati, mwingine akiwa ni Nadir Haroub Cannavaro.
Leo bila shaka Yawe Berko atadaka badala ya Ally Mustafa ‘Barthez’ na kama Twite ataanzishwa kulia, maana yake Nahodha Nsajigwa Shadrack atapumzika, kushoto Oscar Joshua, katikati wawili kati ya Twite, Cannavaro na Yondan, kiungo mkabaji Athumani Iddi ‘Chuji’, viungo wa pembeni Simon Msuva na Hamisi Kiiza, kiungo mchezeshaji Haruna Niyonzima na washambuliaji Said Bahanuzi na Didier Kavumbangu.
Lakini katika mechi za karibuni, Brandts amekuwa akitumia viungo wawili wakabaji na mshambuliaji mmoja, ili kumfanya Niyonzima acheze zaidi na Frank Domayo ndiye amekuwa akichukua nafasi ya mshambuliaji.
Haijulikani katika mchezo wa leo kama Mholanzi huyo ataendelea na mbinu hiyo hiyo au ataamua kutumbukiza washambuliaji wawili.
Mara ya mwisho Yanga na Azam zilikutana katika fainali ya Kombe la Kagame, Agosti 10, mwaka huu na Watoto wa Jangwani wakaibuka vinara na kutwaa Kombe kwa ushindi wa 2-1.
Mjini Morogoro nako, nyasi za Uwanja wa Jamhuri zitahimilii vishindo vya Simba na Mtibwa, ambao katika miaka ya karibuni, wamekuwa vibonde wa Wekundu hao wa Msimbazi.
Simba iliendelea kubaki mkoani Morogoro, baada ya sare ya 1-1 na Polisi Jumatano, kujiandaa na mchezo wa leo, ikiwa imeweka kambi maeneo ya Nane Nane mkoani humo, huku ikijifua kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro.
Wekundu hao wa Msimbazi, wamepania kushinda mechi ya kwanza nje ya Dar es Salaam leo, baada ya awali kutoa sare katika mechi zake zote za ugenini.
Kwenye Uwanja wa Mkwakwani, Tanga Simba ilitoka sare za bila kufungana na wenyeji Coastal Union na Mgambo JKT kabla ya juzi kufungana 1-1 na Polisi, tena yenyewe ndio ikihaha hadi kipindi cha pili kukomboa bao, baada ya Mokili Rambo kutangulia kuwafungia Maafande hao kipindi cha kwanza.
Mkombozi wa Wekundu hao wa Msimbazi, alikuwa ni kiungo Amri Kiemba juzi, ambaye hilo linakuwa bao lake la tano msimu huu.
Pamoja na hayo, Simba inajivunia kuwa timu pekee ambayo hadi sasa haijapoteza mechi hata moja katika Ligi Kuu, ikiwa inaongoza ligi hiyo kwa pointi zake 23 sawa na Yanga, baada ya kucheza mechi 11, lakini ina wastani mzuri zaidi wa mabao.
Zaidi ya sare hizo tatu, Simba ilitoa sare nyingine mbili Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, dhidi ya Kagera Sugar ya Bukoba 2-2 na Yanga SC, wapinzani wao wa jadi, 1-1.

Azam FC
REKODI YA YANGA AZAM FC:
Machi 10, 2012
Yanga 1 – 3 Azam
Septemba 18, 2011
Azam 1 – 0 Yanga
Machi 30, 2011
Yanga 2-1 Azam
Oktoba 24, 2010
Azam 0-0 Yanga
Machi 7, 2010
Yanga 2-1 Azam
Oktoba 17, 2009
Azam 1-1 Yanga
Aprili 8, 2009
Yanga 2-3 Azam FC
Oktoba 15, 2008
Azam FC 1-3 Yanga
Simba SC
REKODI YA SIMBA NA MTIBWA TANGU 2005:
Machi 18, 2012
Simba 2 – 1 Mtibwa Sugar
Septemba 25, 2011
Simba 1 – 0 Mtibwa Sugar
Februari 27, 2011
Simba 4 – 1 Mtibwa Sugar
Feb 27, 2011
Simba 4-1 Mtibwa Sugar
Sept 29, 2010
Mtibwa Sugar 0-1 Simba
Machi 22, 2009
Mtibwa Sugar 1-0 Simba
Sep 28, 2010
Simba 1-0 Mtibwa Sugar
Apr 21, 2010
Mtibwa Sugar 0-4 Simba
Nov 15, 2009
Simba 3-1 Mtibwa Sugar
Feb 20, 2008
Simba 1-1 Mtibwa Sugar
Okt 7, 2007
Mtibwa Sugar 1-3 Simba
2007: Hazikukutana kwenye Ligi ndogo
Sept 10, 2006
Mtibwa Sugar 1-1 Simba
Apr 9, 2006
Simba 1-1 Mtibwa Sugar
Okt 5, 2005
Simba 2-1 Mtibwa Sugar
Mei 22, 2005
Mtibwa Sugar 0-1 Simba
Mtibwa Sugar
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top