Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

BINGWA CECAFA TUSKER CHALLENGE KUPATIKANA LEO KAMPALA

 

Uganda watatetea ubingwa leo?

Na Mahmoud Zubeiry wa Bin Zubeiry
BINGWA wa Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati, CECAFA Tusker Challenge, anatarajiwa kupatikana leo kwenye Uwanja wa Mandela, Namboole mjini Kampala, Uganda, wakati wenyeji The Cranes watakapomenyana na jirani na mahasimu wao wakubwa katika ukanda huu, Kenya, Harambee Stars kuanzia saa 1:00 usiku.
Mchezo huo, utatanguliwa na mechi ya kusaka mshindi wa tatu, kati ya Tanzania Bara na Zanzibar, itakayoanza saa 10:00 jioni kwenye Uwanja huo huo, unaomilikiwa na serikali ya Uganda.
Mechi zote zinatarajiwa kuwa na upinzani mkali, kwani ukiacha fainali, hata mchezo wa kusaka mshindi wa tatu utakutanisha majirani na timu zinazofahamiana vema.
Zanzibar ilitolewa na Kenya katika Nusu Fainali kwa kufungwa kwa penalti 4-2, kufuatia sare ya 2-2 ndani ya dakika 120, wakati Bara ilichapwa 3-0 na Uganda juzi.
Kulingana na tathmini ya viwango vya timu zote tangu kuanza kwa mashindano haya, Uganda, ambao pia ni mabingwa watetezi, wanapewa nafasi kubwa ya kutwaa Kombe leo.
Hata hivyo, fainali ni mchezo wa maarifa mengi zaidi ya uwezo, hivyo haitakuwa ajabu hata Kenya ikiibuka na mwali leo.
Zanzibar na Bara, itakuwa mechi ya kuonyeshana ufundi na nani zaidi, kwani wachezaji wengi wanafahamiana kwa mfano, leo mshambuliaji wa Bara, John Bocco atakuwa anadhibitiwa na beki anayecheza naye klabu moja, Aggrey Morris.
Au Mrisho Ngassa wa Bara pia, ambaye yuko mbioni kuhamia El Merreikh ya Sudan akipangwa kulia, atakuwa anakabiliana na beki aliyekuwa anacheza naye klabu moja, Simba SC.
Kenya ni mabingwa mara tano wa Kombe la Challenge la CECAFA katika miaka ya 1975, 1981, 1982, 1983 na 2002, wakati pia imeshika nafasi ya pili mara nne na Uganda ndio timu iliyotwaa mara nyingi zaidi taji hilo, (mara 12) katika miaka ya 1973, 1976, 1977, 1989, 1990, 1992, 1996, 2000, 2003, 2008, 2009 na 2011 na pia imeshika nafasi ya pili mara nne.
Michuano ya mwaka huu, imedhaminiwa na Kampuni ya Bia Afrika Mashariki (EABL), kupitia bia yake ya Tusker Lager, kwa dau la la dola za Kimarekani 450,000 na lengo ya michuano ya mwaka huu ni kuzisaidia maandalizi timu za Afrika Mashariki na Kati katika kuwania tiekti ya kucheza Fainali za Kombe la Dunia mwaka 2014 nchini Brazil.
Udhamini wa mwaka huu ni ongezeko la aslimia 5, kutoka michuano ya mwaka jana mjini Dar es Salaam, ambayo Uganda waliibuka mabingwa.
Ni udhamini ambao umehusu usafiri, malazi na huduma nyingine, wakati jumla ya dola za Kimarekani 60.000 zitakuwa kwa ajili ya zawadi, bingwa akipewa dola 30.000, mshindi wa pili dola 20.000 na dola 10.000 mshindi wa tatu na michuano imekuwa ikionyeshwa moja kwa moja na Televisheni ya Super Sport ya Afrika Kusini.
Michuano hiyo ambayo huandaliwa na CECAFA, Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati, ambalo lina wanachama 13, ndiyo ya kwanza kabisa mikubwa kufanyika barani Afrika, ilihusisha mataifa manne, Kenya, Uganda, Tanganyika (sasa Tanzania Bara) na Zanzibar, ikijulikana kwa jina la Kombe la Gossage.
Michuano hiyo ya Gossage ambayo sasa imekuwa Kombe la Challenge, ilifanyika mara 37 kuanzia mwaka 1926 hadi 1966, ilipobadilishwa jana na kuwa michuano ya wakubwa ya soka kwa mataifa ya Afrika Mashariki na Kati, ilifanyika mara saba kati ya mwaka 1965 na 1971, ilipozaliwa rasmi CECAFA Challenge.
Tanganyika ilianza kushiriki michuano hiyo tangu mwaka 1945, wakati Zanzibar ilijitosa miaka minne baadaye, 1949.
Michuano hiyo ilikuwa ikidhaminiwa na bepari aliyekuwa akimiliki kiwanda cha sabuni, William Gossage, aliyezaliwa Mei 12 mwaka 1799 na kufariki dunia Aprili 9, mwaka 1877.
Michuano hiyo mikongwe zaidi barani, imekuwa ikiandaliwa na Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), ikihusisha timu za taifa za ukanda huo.
Hadi inafikia tamati michuano ya Gossage, Uganda ilikuwa inaongoza kwa kutwaa taji hilo, mara 22, ikifuatiwa na Kenya iliyotwaa mara 12 na Tanzania mara tano.
Mwaka 2005, michuano hiyo ilifanyika chini ya udhamini wa bilionea wa Ethiopia mwenye asili ya Saudi Arabia, Sheikh Mohammed Al Amoudi na kupewa jina la Al Amoudi Senior Challenge Cup, lakini sasa Tusker ndiyo mambo yote. Je, nani ataibuka bingwa wa Challenge mwaka huu, ni Uganda tena au Kenya? Bila shaka hilo ni jambo la kusubiri na kuona.
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top