Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

Sehemu Ya Maoni Mahsusi Ya CPT Katiba Mpya


 

3.0 MAPENDEKEZO MAHSUSI


3.1 Vigezo na misingi ya kikatiba na kisheria


Kuna umuhimu wa kuwa na Vigezo na misingi ya kikatiba-kisheria ya kuhakikisha kuwa watu, ambao ndio wanaoiunda Katiba Mpya na kwa niaba yao Bunge la Katiba linatarajiwa kupitisha hiyo Katiba, watakuwa na mamlaka kwa Serikali:

3.1.1 Nafasi ya watu katika kusukuma Serikali


Nguvu ya watu katika kusukuma Serikali kutimiza wajibu wake wa kusimamia kwa dhati na kistadi mambo ya kiutendaji ya huduma na shughuli zote za umma ipate fursa za kufanya kazi kihalisia na kuifanya nchi kuendeshwa vizuri kwa manufaa na maslahi ya wananchi, wakiwemo wanyonge kihali na mali.

3.1.2 Nguvu ya watu kupewa nguvu kupitia vyombo vya kikatiba na kisheria


Jambo hili liwe wazi na halisi, sio tu kwa njia ya vigezo na misingi, bali pia kimuundo kupitia vyombo vya kikatiba-kisheria ambavyo vinashirikisha na/au kuwakilisha wananchi katika maamuzi juu ya mambo muhimu kuhusu maisha na maslahi ya kijamii/kitaifa.

3.2 Uwajibikaji na uzingatiaji wa maadili mema kikatiba na kisheria


Katiba ielekeze uwajibikaji na uzingatiaji wa maadili mema, pamoja na udhibiti wa madaraka. Tunasisitiza: Mambo haya ni ya msingi, yasiende kisiasa bali yapewe nguvu kikatiba/kisheria. Ili kufanikiwa katika hili, haitoshi tu kuwa na Katiba bali iwe niKatiba inayotekelezeka kikamilifu.

3.3 Maadili Mema


3.3.1 Mmomonyoko wa maadili kamajanga la kijamii na kitaifa


Kiwango cha maadili na uwajibikaji kiadilifu na kizalendo nchini kimeshuka mno kiasi kwamba mmomonyoko wa maadili ni janga la kijamii kitaifa. Hatua maalumu za dhati zinahitajika kulinusuru Taifa letu kutokana na janga hilo:
3.3.1.1 Elimu ya maadili iendeshwe mashuleni na vyuoni.
3.3.1.2 Serikali itakiwe na Katiba na sheria husika kuchukua wajibu huu na kuutekeleza katika mfumo rasmi wa elimu kupitia Tume Huru ya Elimu ambayo ndiyo iwajibike moja kwa moja katika kusimamia kazi hii.

3.3.2 Tume Huru ya Elimu:


CPT inapendekeza kwamba, kwa njia ya Tume Huru ya Elimu:
3.3.2.1 Katiba au sheria mpya ielekeze Elimu kutolewa kwa umma ikilenga kuwezesha wananchi kusaidia Mahakama na Bunge kutimiza wajibu wake wa kudhibiti, kuelekeza na kuwajibisha Serikali katika utekelezaji wa wajibu wake kwa umma na kuhakikisha utawala bora ambao unawajibika, unawajibisha na unawajibishwa; ni shirikishi na wakilishi.
3.3.2.2 Aidha, uwepo wajibu kikatiba/kisheria, wa kuelimisha watu juu ya maovu ya kijamii na athari zake hasi kwa jamii nzima na kila mwana-jamii (social evils and their negative impact on the whole society and each of its members) na kuhimiza maadili mema kwa viongozi, wafanyabiashara, na raia wote.

3.3.3 Tume Huru ya Maadili na Udhibiti wa Ufisadi


CPT inapendekeza kuwa kuwe na chombo kipya kitakachoitwa Tume Huru ya Maadili na Udhibiti wa Ufisadi (Ethics and Anti-Corruption Commission) ambayo:
3.3.3.1 itapewa uwezo wa kudhibiti na kupambana na rushwa na pia kudhibiti ukiukwaji hasa wa maadili ya uongozi (ikiunganisha shughuli za TAKUKURU na za Tume ya Maadili ya Viongozi ya sasa).
3.3.3.2 Hii itaondoa haja ya kuwa na Tume mbili zenye uwezo na tija ndogo na kuwa na Tume moja yenye sifa hizi mbili. Pia iwe na uwezo wa kuyashughulikia mambo yote ya ufisadi na rushwa nchini yenye athari kwa sekta za umma, binafsi na asasi za kijamii.
3.3.3.3 Tume hii ikishafanya uchunguzi kuhusu rushwa na/au ufisadi na kujiridhisha kuwa kuna kesi ya kupeleka mahakamani, ikabidhi jalada (faili) kwa Mwendesha Kesi za Jinai Mkuu (DPP) kwa ajili ya kuendesha mashtaka mahakamani. Pale ambapo DPP atakuwa na maoni kwamba hakuna ushahidi wa kutosha kwa ajili ya kesi ya jinai, ama ashauri uchunguzi zaidi ufanywe kuhusu maeneo/masuala atakayoelekeza wazi wazi kwa Tume au arejeshe jalada kwenye Tume kwa ajili ya hatua za kinidhamu kuchukuliwa kwa mujibu wa sheria husika isiyo ya jinai dhidi ya mtuhumiwa.
3.3.3.4 Kwa vyovyote vile, DPP awajibike kutoa sababu za maamuzi yake kuhusu mapendekezo kwake ya Tume Huru hii kwa uwazi.
3.3.3.5 Aidha, Katiba na sheria ziainishe misingi mihimili ya maadili hasa ya uongozi na hatua zitakazochukuliwa kwa wakiukaji.

3.3.4 Udhibiti na uwazi katika mapato na matumizi ya mali ya taifa


CPT inapendekeza kuwa kwa mujibu wa Katiba na sheria mpya husika:
3.3.4.1 ielekezwe kuwepo uwazi katika mapato na matumizi ya mali ya taifa;
3.3.4.2 aidha izuiliwe/iwe marufuku kwa mtu au mamlaka yoyote kuwa na madaraka au uwezo juu ya mapato na matumizi ya mali ya taifa bila kuzingatia vigezo na/au masharti yaliyobainishwa na yenye kuwajibisha kisheria.

3.4 Mgawanyo wa Mali na Rasilimali za Nchi


3.4.1 Kuna Upendeleo katika Mgawanyo wa Mali na Rasilimali za Nchi


Mwelekeo wa kugawia kiupendeleo sehemu moja dhidi ya nyingine, au kundi moja dhidi ya jingine imekuwa ndio kichocheo cha wabunge kutaka ama kutakiwa na wapiga kura wao kuingia/kuteuliwa nafasi ya uwaziri. Licha ya mali na rasilimali za nchi, mambo ni vivyo hivyo kwa misaada na mikopo toka nje. Maoni yetu kwa ajili ya zoezi la Katiba yako katika sehemu mbili kama ifuatavyo:
3.4.1.1 Maliasili
(a) Kila mara inapopasa, Serikali itathmini na kuhakiki maliasili husika ili ipate kujua kwa uhakika na kwa misingi ya kisayansi kiasi na thamani yake kabla ya kuingia katika mkataba na mwekezaji/wawekezaji. Hii ifanyike hata kama mkataba ni wa aina ya ubia; makubaliano, kati ya mambo mengine, yazingatie, kwa misingi ya haki navigezo vinavyokubalika, uwiano wa thamani hiyo na thamani ya uwekezaji halisi utakaofanywa na mwekezaji/wawekezaji.
(b) Aidha, njia za kuwawezesha wananchi na taifa kufaidika zizingatiwe – kuwekeza mahalia katika viwanda (Industrial Capital investments in mining areas) km. kwa kutumia madini kutengeneza vidani/vito vya thamani (Jewelry Industry); kuandaa wataalam ambao wataweza kupata ajira nje baadaye; kuwezesha watu wa ndani kutumia fursa za uwekezaji na, hivyo, kuinua hali yao ya kipato na kujiletea maendeleo; kushiriki katika faida ya wakati huo – mkataba kunufaisha nchi na watu wake badala ya kufanya karibu kila kitu kwenda kwa mwekezaji na wataalamu kutoka nje;
(c) Kushiriki umiliki kwa njia ya ubia, inatupa nguvu ya kuhakikisha tunafaidika na pia utunzaji mazingira unazingatiwa, tutashiriki kuweka masharti ya utumiaji na uuzaji wakati uvunaji wa rasilimali unaendelea;
(d) Mikataba isifanyike kwa siri bali kwa njia zinazokidhi kanuni na maadili ya uwazi katika masuala ya mikataba ya kitaifa inayogusa maslahi ya taifa kiuchumi, kisiasa na kiutamaduni (tukiondoa masuala nyeti ya ulinzi na usalama wa Taifa ambayo uwazi wake sharti uwe ndani ya vyombo/wizara na idara husika za Dola); Mikataba itakiwe kisheria kuwa na vifungu vinavyotoa fursa au upendeleo wa makusudi kwa wananchi kutoa huduma za kawaida zinazoweza kupatikana nchini kwa matumizi ya viwanda au shughuli za uwekezaji.
(e) Hivyo, wananchi wawe na fursa kubwa ya kushiriki katika kutoa huduma zinazohitajika (service industry) - ugavi na usambazaji wake - kwenye sehemu husika.
(f) Haya yakizingatiwa, nchi na wananchi wake watafaidika kwa wakati huo na kwa vizazi vijavyo. Tuwe na msimamo, kikatiba na kisheria, kuwa kamwe tusiendelee kuvuna rasilimali bila kuhakikisha tunafaidika. Ni bora kuwa na subira, kujipa nafasi ya kujiandaa kuliko kuwaachia nafasi wawekezaji wa kigeni kuvuna faida yote kwa sababu ya kutokuwepo uwezo wa kutosha wa ndani wa kuibakisha sehemu nono ya faida hiyo (a substantial share of the profit) nchini.
(g) Hivyo, kuweko na Tume Huru ya Ardhi, Maliasili na Mazingira (Land, Natural Resources and Environmental Commission) kama chombo cha kikatiba/kisheria cha kutekeleza sera za kizalendo zinazoweza kulifanya taifa na wananchi wake wanufaike na uwekezaji na uvunaji wa rasilmali ya nchi yao bila kuathiri vibaya mazingira na tabia-nchi.

3.4.1.2 Pato la Taifa
(a) Mgawanyo wa pato la taifa (national revenue) uwe ni wa kiuwiano kwa kuzingatia idadi ya watu na ukubwa wa eneo, maeneo na makundi ya wasio na uwezo (vulnerable groups) yakipewa kipaumbele.
(b) Katika kupanga Bajeti, kila sehemu – Mikoa wapate kiwango sawa; na Mikoa iliyo nyuma ipate viwango vya ziada kutoka mfuko maalum (equalization fund) kwa lengo hilo.
(c) Fungu la matumizi ya Serikali Kuu liwekwe bayana na matumizi yasiwe ya kifujaji.
(d) Tume maalumu, Tume ya Mgawanyo wa Pato la Taifa na Udhibiti wa Bajeti (Public Revenue Allocation and Budget Control Commission) iundwe kwa ajili ya kazi ya kuweka misingi na vigezo vya Mgawanyo wa pato la taifa na Udhibiti wa Bajeti; kusimamia/kuratibu utekelezaji, uimarishaji, na tathmini yake kiendelevu kwakubainisha vema masuala ya Mgawanyo wa pato la Taifa na ya Udhibiti wa Bajeti; ilmradi masuala hayo yasiingiliane kwa kuasiana kisheria na kiutendaji.

3.5 Rushwa na Ufisadi


3.5.1 Penye rushwa hakuna haki; kwani haki hugeuka na kuwa bidhaa. Wanaoweza kupindisha sheria ili kujipatia haki yao ni wale wenye fedha na wenye nafasi za madaraka na mamlaka. Tatizo hili limo nchini mwetu na ni la kijamii na mfumo mzima unatawaliwa na uovu huu. Tiba yake ni nini? Tiba itaweza kupatikana hasa kwa njia za kijamii na kisheria: Elimu na sheria inayotoa kipaumbele kwa umuhimu wa maadili mema katika nyanja zote za kitaifa na kijamii (uchumi, siasa, sheria/haki na utamaduni – dini, elimu, michezo, familia/ndoa na malezi).

3.6 Uwajibikaji na Uwajibishwaji


3.6.1 Umuhimu wa mfumo unaotuwezesha kuwajibishana


Hili ni suala pana; kwa hiyo, tunahitaji kujenga mfumo unaotuwezesha kuwajibishanakuanzia Rais na Serikali/Utawala kwa ujumla, Bunge, Mahakama hadi raia. Mathalan,Bunge liwajibike kwa wananchi, na wenye kushika nafasi za kuteuliwa wawe wanawajibika kwa wananchi moja kwa moja au kwa njia ya vyombo wakilishi-shirikishi ambamo wao ni watumishi, badala ya kuwajibika kwa yule aliyewateua tu.

3.6.2 Rais na Dola Kikatiba na Kisheria


3.6.2.1 Ihakikishwe kuwa anayeteuliwa kugombea nafasi ya Urais anakidhi vigezo msingi kimaadili na kiuongozi na kwamba umri wake usiwe chini ya miaka 40 na usizidi miaka 65.
3.6.2.2 Rais awe anawajibika kwa wananchi kupitia Bunge. Bunge lipewe uwezo wa kumwondoa madarakani kwa vigezo na njia vinavyozingatia kwa dhati maslahi ya kitaifa ya kutoyumbisha nchi bila kupuuzwa kwa athari za utovu wa nidhamu, uwajibikaji na maadili mema ya uongozi wa Taifa.
3.6.2.3 Asiwe na mamlaka ya kuteua wale wanaopaswa kumwajibisha – hasa viongozi wa Mahakama na wa Bunge.
3.6.2.4 Uteuzi wake wa viongozi uzingatie sifa na vigezo stahiki – hasa uzoefu, utaalam, weledi, uadilifu, uzalendo na ridhaa ya Bunge. Unasaba na uswahiba viepukwe kabisa.
3.6.2.5 Anapotakiwa kusaini sheria iliyopitishwa na Bunge, apewe ukomo wa muda,km. siku kumi, bila kuhesabu siku zisizo za kazi.
3.6.2.6 Kuna haja ya kuwa na serikali ndogo lakini yenye ufanisi au tija. Wizara naMawaziri wawe si chini ya 15 na wasizidi 20. Idara za wizara na Tume Huru zitashiriki kuleta ufanisi wa Serikali.
3.6.2.7 Wabunge wasiwe mawaziri. Mawaziri wateuliwe na Rais kwa kuzingatia sifa na vigezo stahiki tajwa katika 3.6.2.4 hapo juu. Na Rais apendekeze na wajadiliwe na kuidhinishwa na Bunge kabla ya kuteuliwa rasmi. Aidha, kusiwe na manaibu mawaziri.
3.6.2.8 Kwa kuwa mawaziri watakuwa wataalamu na wenye uwezo wa kusimamia mipango na utekelezaji wa programu za wizara, nafasi ya waziri itaunganisha kazi za mawaziri wa sasa na makatibu wakuu.
3.6.2.9 Bunge lipewe uwezo wa kumwondoa waziri asiyefaa kwa misingi au vigezo mwafaka vya kisheria na kwa njia ya kura ya Wabunge ya kutokuwa na imani nayeambayo Rais alazimike kuikubali.

3.6.3 Bunge Kikatiba na Kisheria


3.6.3.1 Wabunge wawajibike kwa wananchi ambao wapewe uwezo wa kumwondoa madarakani Mbunge katika jimbo lake la uchaguzi kabla ya ukomo wa muda wa kipindi chake cha kuwa mbunge ikiwa hawajibiki. Kwa ajili ya kupokea taarifa za mara kwa mara kutoka kwa mbunge wao na, panapopasa, kumwajibisha:–
(a) liweko baraza/jukwaa (forum) katika kila jimbo la uchaguzi litakalokutana angalau mara nne kila mwaka na kuwasilisha mapendekezo/maazimio na maamuzi yake kwa Spika wa Bunge
(b) Katiba Mpya impe Spika madaraka ya kuchunguza mapendekezo au maazimio ya kuwajibisha mbunge kama inavyoelezwa kwenye kifungu 3.6.3.2 hapa chini.
(c) Utawala wa kila Mkoa, ngazi ya wilaya, uwajibike juu ya maandalizi, uratibu na kumbukumbu za baraza/jukwaa hili.
3.6.3.2 Wabunge wote wawe wa kuchaguliwa ili wawajibike kwa wapiga kura wao na wawajibishwe nao. Katiba iweke vigezo vya mbunge kusimamishwa au kutakiwa kuonyesha kwa nini asiondolewe katika wadhifa wake wa kuwa Mbunge kwa kushindwa kukidhi matakwa ya vigezo hivyo. Km. Ukiukwaji wa maadili ya uongozi; kitendo/vitendo vya rushwa/ufisadi vilivyodhihirishwa kwa mujibu wa sheria; kosa/makosa mengineyo ya jinai; kufirisika; kutohudhuria vikao vya Bunge bila sababu mwafaka mara tatu mfululizo; kutofuatilia kwa makini na uweledi masuala muhimu ya jimbo lake; au uzembe uliokithiri katika kutimiza wajibu wake wa Ubunge.
3.6.3.3 Spika asiwe mbunge wala asiwe na cheo katika chama cha siasa.
(a) Mfumo wa sasa unaonyesha udhaifu katika eneo hili kwa kuwa Spika amekuwa akichaguliwa kutokana na chama tawala na waliopendekezwa au waliojitokeza kugombea wametegemea hali yao ya kuwa wanachama wakereketwa wa vyama vyao. Katika kuongoza shughuli za Bunge, kumekuwa na mwelekeo wa Spika kushinikizwa na/ au kupendelea/kulinda chama chake. Hali hii haijengi mazingira adili ya demokrasia ya vyama vingi katika Bunge, chombo kiteule cha uwakilishi na kutunga sheria za nchi.
(b) Hivyo, ni jambo la msingi na adili kwamba Spika awe mtu huru mwenye hekima na busara na ambaye si kiongozi katika chama chochote cha siasa chenye uwakilishi Bungeni wala mbunge.
3.6.3.4 Viti maalum viwe kwa:–
(a) wanawake watatu (3) kila Mkoa na kijana mmoja (1) tu kila Mkoa ambao watapendekezwa na vyama kwa kila chama kupendekeza wawili wawili na hao watachaguliwa kwa kura mkoani mwao na wananchi wakati wa Uchaguzi mkuu;
(b) makundi ya wenye ulemavu yapate mwakilishi mmoja (1) ambaye atapatikana kwa njia ya ushindani wa kupigiwa kura na makundi husika wakati wa Uchaguzi Mkuu kutokana na mapendekezo ya mgombea mwenye ulemavu mmoja mmoja kwa kila kundi.
3.6.3.5 Muundo wa uwakilishi uwe wa kiuwiano nchi nzima kwa kuzingatia idadi ya watu na ukubwa wa eneo kama itakavyobainishwa kisheria, kutekelezwa na kuratibiwa kitaalamu. Suala la Muungano lisisababishe kukiukwa kwa kanuni au msingi huu wa uwakilishi katika Bunge la Muungano au chombo chochote cha Muungano chenye uwakilishi. Hii itaifanya hoja ya kwamba Tanganyika/Tanzania Bara imemezwa na Muungano au kuwa Zanzibar imemezwa na Tanganyika/Tanzania Bara ikose msingi halali kwani kila sehemu itapata stahili zake kwa vigezo mwafaka vyenye kuzingatia kanuni za kisayansi na haki.
Inaendelea.....
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top