Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

MABILIONI FEDHA ZA USWISI HOMA TUPU, WAZIRI MKUCHIKA ASHINDWA KUFIKA MBELE YA KAMATI YA BUNGE YA SHERIA, KATIBA NA UTAWALA JIJINI DAR ES SALAAM


WABUNGE wa Kamati ya Bunge ya Sheria, Katiba na Utawala, jana wameonyesha kukerwa na taarifa za mamilioni ya fedha yanayodaiwa kufichwa nchini Uswisi. 

Wabunge hao, walionekana kuchanganywa mno na kitendo cha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utawala Bora), George Mkuchika, kutofika mbele ya kamati ili kujibu maswali yao kuhusiana na tuhuma hizo.

Hali hiyo ilitokea mjini Dar es Salaam, wakati wa kikao cha Kamati ya Sheria, Katiba na Utawala, chini ya Mwenyekiti wake, Pindi Chana, ilipokutana na viongozi wa Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma.
 

Akichangia mjadala huo, Mbunge wa Kibondo, Felix Mkosamali (NCCR-Mageuzi), alisema Watanzania wamekuwa wakijiuliza mambo kadhaa kuhusu sakata la fedha zinazodaiwa kufichwa nchini Uswisi, lakini mpaka sasa Serikali imeshindwa kutoa majibu ya kina.

“Mheshimiwa mwenyekiti, ninasikitisha mno kutokuwepo kwa Waziri wa Utawala Bora katika mkutano huu, na badala yake sitegemei kama hawa viongozi wa Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma wanaweza kuwa na majibu mazuri katika suala hili.

“Umefika wakati, tunataka kujua hatma ya fedha zilizofichwa Uswisi kwa Serikali kutoa kauli, tunasikitika kuona kimya kinaendelea tu.

“Kuna mambo kadhaa ambayo bado yana changamoto, ikiwemo viongozi wote ambao hawakujaza fomu zinazoonyesha wana mali kiasi gani wanazomiliki na hatua gani zimechukuliwa kwa wale wote ambao hawakujaza fomu hizi,” alihoji Mkosamali.

Hadi sasa, inaelezwa asilimia 90 ya viongozi hawajahakikiwa mali hizo.

Mbali na hatua hiyo, imebainika kuwa tangu ilipoanzishwa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma mwaka 1995, hadi sasa ni viongozi wanne tu, waliobainika kutokamilisha utaratibu huo na hakuna hata mmoja wao aliyechukuliwa hatua za kisheria.

Akijibu hoja za wabunge hao, Kamishna wa Sekretarieti hiyo, Jaji Salome Kaganda, alisema kutokana na hali hiyo bado tume inakabiliwa na changamoto kadhaa, zikiwamo ufinyu wa watumishi.

Kwa upande wake, Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (CHADEMA), alitaka kufahamu tangu kuanzishwa kwa sekretarieti hiyo, viongozi wangapi wa umma walibainika kukiuka sheria hiyo na hatua walizochukuliwa.

Alisema kwa mujibu wa taarifa zilizowasilishwa mbele ya kamati hiyo, mwaka jana kati ya viongozi wa umma zaidi ya 9,000 wanaotakiwa kukaguliwa mali zao kwa mujibu wa sheria, ni viongozi 133 tu ndio mali zao zilihakikiwa, sawa na asilimia 10.

“Kutokuwapo kwa sheria kali ya maadili, tumekuwa tukishuhudia hata Ikulu imegeuzwa lango la biashara, sheria iko wapi jamani ya kuwabana viongozi hawa,” alisema Lissu.

Naye Mbunge wa Bukoba Vijijini, Jasson Rweikiza (CCM), alitaka kufahamu kama sekretarieti hiyo, inashughulika na masuala ya maadili ya kitaifa au maadili ya viongozi pekee kwa upande wa mali zao, huku akitolea mfano hali ya sasa ya kukithiri kwa vitendo vya uvunjifu wa maadili.

“Wote ni mashahidi, kuna matatizo makubwa ya maadili, vijana hawana heshima kama zamani, ulevi umekithiri kila kona na mbaya zaidi ushoga nao umepiga hodi, haya yanashughulikiwa vipi ili kukomeshwa?” alihoji.

Akijibu hoja hizo, Kaganda, alikiri tangu kuanzishwa kwa tume hiyo, hakuna kiongozi wa umma aliyekiuka sheria na aliyechukuliwa hatua, ingawa orodha yao ipo.

Alisema wakati sekretarieti hiyo inaanzishwa, kulikuwa hakuna baraza la kusimamia masuala hayo.

“Baraza la Sekretarieti ya Maadili ya Umma, lililokuwepo halikubahatika kufikia hatua hiyo, nalo limemaliza muda wake na sasa tuko kwenye mchakato wa kuunda baraza lingine ambalo litakamilika muda si mrefu, tuna matarajio ya kupata mafanikio,” alisema Kaganda.

Hata hivyo, aliiomba kamati hiyo kumpa muda ili iweza kuchambua hoja nyingine na kisha iwasilishe kwa maandishi.

Kwa muda mrefu sasa, Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, amekuwa akisisitiza kuwa kuna Watanzania wameficha kiasi cha dola za Marekani milioni 196, ambazo ni zaidi ya Sh bilioni 300 na Serikali imeshindwa kuwachukulia hatua
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top