Moto mkubwa ulioanza katika Mlima Kilimanjaro tangu siku ya Jumapili tarehe 7.7.2013
umeendelea kudhibitiwa kwa kiwango kikubwa bila kuathiri shughuli za utalii katika Hifadhi ya Kilimanjaro.
Hadi
kufikia leo tarehe 9.7.2013 moto umedhibitiwa kwa kiwango cha asilimia
75 na dalili zinaonyesha kuwa katika kipindi kifupi kijacho utaweza
kudhibitiwa wote.
Mkuu
wa Mkoa wa Kilimanjaro Leonidas Gama ametoa agizo kwa wilaya zote za
Mkoa wa Kilimanjaro kushiriki operesheni maalum ya kuzima moto huo kwa
kutoa askari mgambo watakaoshirikiana na TANAPA katika kuzima moto.
Hifadhi
ya Kilimanjaro imeweka kambi mbili maalum kwa ajili ya kuhudumia
wanaoshiriki zoezi la kuzima moto moja ikiwa katika eneo la Nanjara
wilayani Rombo ambako ndipo ulipo sehemu kubwa ya moto na kambi ya pili
ipo katika eneo la Marangu kwa ajili ya kuhudumia eneo la Kilema Juu.
Shughuli
za Utalii katika Mlima Kilimanjaro zinaendelea kama kawaida na hakuna
watalii wowote walioathirika na moto huu hasa kwa kuwa njia zote muhimu
za Marangu, Mweka, Machame, Umbwe, Lemosho na Rongai zinazotumika kwa
ajili ya kupandisha watalii mlimani na zile za kushukia hazijaathiriwa
na moto.
TANAPA
kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi wanaendelea na juhudi za kutafuta
waliohusika na uharibifu huu na mara zoezi la kuzima moto
litakapokamilika taarifa ya tathmini ya madhara ya moto itaweza
kufanywa.
Imetolewa na Idara ya Uhusiano
Hifadhi za Taifa Tanzania
09.07.2013
Post a Comment