*************
Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi(CCM), Mkoa wa Shinyanga,
Hamisi Mgeja ameonya baadhi ya viongozi wa chama hicho kuwajengea chuki
wanachama kadhaa na viongozi kwa madai wako karibu na Mbunge wa Monduli,
Edward Lowassa.
Hatua ya Mgeja imekuja ikiwa ni siku chache baada
ya Mwenyekiti wa CCM, Mkoa wa Geita, Joseph Kasheku ‘Msukuma’ kumkana na
kumshutumu, Mwenyekiti wa Wenyeviti wa CCM, Mgana Msindai kuwa
anawalazimisha kuwa nyuma ya Lowassa wakati sivyo ilivyo.
Hata hivyo, Msindai alikanusha madai hayo kuwa
hakuwahi kuwazungumzia wenyeviti wa CCM wa mikoa kuwa nyuma ya Lowassa
zaidi ya kusema kuwa wanamuunga mkono katika masuala mbalimbali ya
maendeleo.
Akizungumza katika mahojiano maalumu, Mgeja
alimtetea Msindai kuhusu suala la wenyeviti wa CCM kuwa nyuma ya Lowassa
katika urais. Alisema: “Nataka kutoa angalizo kwa viongozi ndani ya
chama, Tanzania kwa ujumla, kumejitokeza tabia ya baadhi ya watu
kuchukiana eti tu kwa sababu wako nyuma ya Lowassa,” alisema na
kuongeza:
“Kumeanza watu kuchukiana, kuhukumiana kwa sababu
uko karibu na Lowassa au kuwa na imani naye katika utendaji kazi wake,
kumpenda na kumkubali mtu ni utashi wa mtu binafsi...tusihukumiane wala
kuchaguliana marafiki,” alisema Mgeja.
Mgeja alisema: “Hakuna dhambi ya kumpenda au
kumwamini Lowassa, lakini watu wanachukia, watu wananung’unika, wananuna
haya yote ni majungu, woga, wivu na kutokujiamini. Inawezekana
wanaofanya hivyo, wanatumwa na walio nyuma yao.
“Katika kipindi cha kuelekea uchaguzi, tusianze
kusakana uchawi, muda ukifika, kila mtu atabebwa kwa sifa zake na
atajibeba kwa umahiri wake.”
Mgeja alisema, kazi kubwa inayotakiwa kufanyika
kwa wabunge, mawaziri na viongozi wa kada mbalimbali ni kukaa chini na
kuwatumikia wananchi kwa kuhakikisha wanapata maji safi, dawa
hospitalini na elimu kuliko kutumia muda mwingi kuangalia nani anampenda
Lowassa.
“Kuna changamoto nyingi zinazowakabili wananchi na
kila siku wanatuangalia viongozi, suala la vijana ni tatizo kubwa
huduma za msingi kuliko kukaa na kuangalia Lowassa anafanya nini na yuko
na nani, haileti tija hata kidogo,” alisema.
Mgeja aliwataka wanaCCM kutulia na kutafakari
mambo ya maendeleo kwa kuwa hakuna mtu aliyejitangaza urais akiwamo
Lowassa zaidi ya kuanzisha safari ya matumaini ambayo ndani yake kuna
mafanikio katika elimu, huduma za afya, ajira kwa vijana na mambo
mengi,” alisema.
Hivi karibuni, Msindai alikaririwa akisema: “Mimi
ni Mwenyekiti wa wenyeviti wa CCM, lakini sikuwahi kuzungumza kuwa
wenyeviti wote wanamwunga mkono Lowassa katika Uchaguzi Mkuu 2015...
kikubwa tulichozungumza ni kumuunga mkono katika safari yake ya
mafanikio katika kuendeleza elimu, maji, ujenzi wa zahanati.”
Msindai alisema wanamwangalia Lowassa kutokana na
uwezo wake katika kusimamia mipango yake ya maendeleo na zaidi katika
kupigania elimu pana kwa Watanzania.
mwananchi
Post a Comment