Waziri Mkuu, Mizengo Pinda
---
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda amesema hatima ya uchaguzi wa
Serikali za Mitaa mwaka huu utategemea uamuzi wa wajumbe wa Umoja wa
Katiba ya Wananchi (Ukawa) kurejea katika Bunge Maalumu kuipitisha
Katiba Mpya kwa wakati.
Pinda alisema hayo jana katika kikao chake na
mameya na wenyeviti wa halmashauri za wilaya na miji nchini uliofanyika
hapa ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Wiki ya Serikali za Mitaa.
“Uchaguzi wa Serikali za Mitaa mwaka huu
umegubikwa na kitendawili kutokana na wajumbe wa Bunge hilo kugawanyika
na kushindwa kufanya kazi waliyopewa kwa wakati ili Katiba iweze
kupatikana mapema.
“Ni kama kitendawili kidogo kwa sababu bado Bunge
la Katiba wanavutana. Tuna changamoto hiyo, tunaendelea kumwomba Mungu
ili Ukawa waondoe hasira warejee bungeni,” alisema Pinda.
Hata hivyo, alisema ofisi yake inajiweka tayari
kwa uchaguzi huo mwaka huu kama ulivyopangwa na kwamba hata kama
utasogezwa, mipango iwe imeandaliwa na kuwa tayari kwa wakati wowote.
Alisema hata kama itatokea vinginevyo, Serikali kwa upande wake
haikatazwi kuendelea kufanya maandalizi, ndiyo maana ofisi yake iko
kwenye pilikapilika za kuweka mambo tayari kwa ajili ya kufanikisha
uchaguzi huo.
“Sisi tunakwenda na yote mawili, kama utakuwapo
mwaka huu na hata kama utasogezwa mbele kwa sababu tusipofanya
maandalizi nyie wenyewe mtakuja kunigeuka,” alisema Pinda.
Kauli hiyo ya Pinda imekuja wakati viongozi wa
Ukawa wakisisitiza kuwa hawatarudi bungeni hadi pale
watakapothibitishiwa kuwa Rasimu ya Katiba itakayojadiliwa ni ile
iliyowasilishwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba
Wajumbe wa Ukawa ambao ni wajumbe wa bunge hilo
kutoka vyama vya CUF, NCCR-Mageuzi, Chadema na baadhi kutoka Kundi la
201, walisusia bunge hilo wakidai kuwa wenzao wa CCM walikuwa wanataka
kuingiza rasimu mpya inayoendana na mfumo wa Serikali mbili badala ya
rasimu ya Tume iliyopendekeza serikali tatu.Kwa habari zaidi Bofya na Endelea...............
Post a Comment