Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

UCHAGUZI UTAKUWA HURU, HAKI NA WENYE UTULIVU: DK.SHEIN




STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                              24.10.2015
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesisitiza kuwa uchaguzi unaotarajiwa kufanyika kesho utakuwa huru, haki na wenye utulivu na kuwahakikishia washirika wa maendeleo likiwemo Shirika la Misaada la Uingereza (DFID) kuwa Zanzibar itaendea kuwa na amani kwani ndio msingi wa maendeleo.

Dk. Shein aliyasema hayo katika mazungumzo kati yake na Kiongozi wa Shirika la Misaada la Uingereza anayefanya kazi zake nchini Tanzania Mhe. Vel Gnanendran, huko Ikulu mjini Zanzibar.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo wa Shirika la DFID ambaye alifuatana na Balozi wa Uingereza nchini Tanzania Mhe. Dianna Melrose kuwa Zanzibar itaendelea kuwa visiwa vya amani na utulivu katika kipindi chote cha uchaguzi mkuu na hata baada ya uchaguzi.

Dk.Shein alisema kuwa hatua za maendeleo zilizofikiwa na Zanzibar sambamba na amani na  utulivu uliopo ndivyo viliyoyapelekea mashirika mbali mbali ya Kimataifa ulimwenguni kuendelea kuiunga mkono Zanzibar likiwemo Shirika la DFID kwa kuthamini na kutambua juhudi zake hizo.

Dk. Shein alimuhakikishia kiongozi huyo wa Shirika hilo kuwa Zanzibar itaendelea kushirikiana na Shirika hilo kwa lengo la kuleta maendeleo endelevu nchini.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein alisema kuwa juhudi kubwa zimechukuliwa na vyombo vya ulinzi kwa kuendelea kusimamia amani na utulivu pamoja na vyama vya siasa wakati wote wa kampeni hivyo ni matarajio yake kuwa hatua hiyo itaendelezwa hata kwa siku za usoni ikiwemo siku ya kupiga kura hapo kesho.

Aidha, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwahimiza wawekezaji kutoka nchini Uingereza kuja kuekeza Zanzibar katika sekta mbali mbali za maendeleo ikiwemo sekta ya kilimo pamoja na  utafiti wake.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alisisitiza haja ya kuweko mpango maalum wa nafasi za masomo nchini Uingereza kwa vijana wa Zanzibar ikiwa ni pamoja na kupitia Shirika hilo la DFID.

Dk. Shein aliwaeleza viongozi hao kuwa Zanzibar itaendeleza uhusiano na ushirikiano kati yake na Shirika hilo la DFID.

Nae  Kiongozi huyo wa Shirika la DFID Mhe.  Vel Gnanendran alimueleza Dk. Shein kuwa Shirika hilo limeazimia kuiunga mkono Zanzibar kwa kutambua juhudi zake katika sekta za maendeleo.

Alisema kuwa juhudi zilizochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha sekta zake za maendeleo zinahitaji kupongezwa na kuungwa mkono ili zizidi kuimarika.

Aidha, kiongozi huyo alimpongeza Dk. Shein kwa kuendelea kusimamia amani, utulivu na mshikamano hapa Zanzibar na kueleza kuwa hiyo ndio nguzo pekee itakayoendelea kuikuza Zanzibar kiuchumi na kimaendeleo.

Balozi wa Uingereza Mhe. Dianna Melrose kwa upande wake alimuhakikishia Dk. Shein kuwa nchi yake inatambua na inathamini uhusiano na ushirikiano wa muda mrefu kati ya Zanzibar na Tanzania nzima pamoja na Uingereza uliopo ambao aliahidi kuuendeleza.

Balozi Melrose alimueleza Dk. Shein kuwa wawekezaji wengi wa nchi hiyo wanavutiwa kuja kuekeza Zanzibar kutokana na kuwepo kwa amani na utulivu sambamba na vivutio kadhaa vya utalii.

Kwa upande wa mashirikiano katika sekta ya elimu alisema kuwa juhudi za makusudi zinaendelea kuchukuliwa na zitachukuliwa katika kuhakikisha nafasi za masomo kwa Zanzibar  nchini humo zinaongezeka.
Sambamba na hayo, Balozi huyo alimpongeza Dk. Shein kwa kuisimamia vyema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar yenye mfumo wa Umoja wa Kitaifa ambayo imepata mafanikio makubwa na kuwa kigezo ndani na nje ya bara la Afrika.

Pia, Balozi huyo aliisifu na kuipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Dk. Shein kwa kutoa fursa sawa ya kufanya Kampeni zilizokuwa huru na amani kwa vyama vyote hapa nchini.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top