Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

TRA HALI SI SHWARI ... NI MWENDO WA PANGA PANGUA

MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) imefanya mabadiliko makubwa baada ya kuwahamisha wafanyakazi 104 waliokuwa Mkoa wa Dar es Salaam na kuwapeleka mikoa mbalimbali nchini.

Mbali na wafanyakazi hao, uhamisho huo umemkumba pia mmoja wa wakurugenzi wake, Aboubakar Kunenge ambaye alikuwa Mkurugenzi wa Rasilimali Watu na Utawala aliyehamishiwa mkoani Rukwa.

Akizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Idara ya Elimu na Huduma kwa Walipa Kodi wa TRA, Richard Kayombo alithibitisha wafanyakazi hao 104 kuhamishwa.

“Ni kweli wafanyakazi hao wamehamishwa, lakini huu ni utaratibu wa kawaida wa kiutawala na tumekuwa tukiufanya mara kwa mara, kila baada ya muda tunawahamisha baadhi ya wafanyakazi wetu,” alisema Kayombo.

Aidha, Kayombo alithibitisha kuwa ni kweli Kunenge ni mmoja wa watumishi wa mamlaka hiyo waliohamishwa na kukiri amepelekwa Rukwa, ambako ataendelea kushughulikia masuala hayo ya utawala na rasilimali watu.

Katika uhamisho huo, wafanyakazi wanaotoka kituo cha TRA Ilala waliohamishwa ni 43 ambao wamepelekwa mikoa ya Iringa, Kigoma, Mbeya, Rukwa, Shinyanga, Ruvuma, Manyara, Tanga, Kilimanjaro, Pwani, Tabora, Morogoro, Lindi na Arusha.

Katika kituo cha Kinondoni, jumla ya wafanyakazi zaidi ya 11 wamehamishiwa katika mikoa Singida, Iringa, Rukwa, Mbeya, Ruvuma, Kagera, Mara, Tabora, Arusha na Tanga. Aidha, katika vituo vya Temeke, wafanyakazi zaidi ya 10 walihamishiwa katika mikoa ya Arusha, Morogoro, Iringa, Tabora, Mara, Kagera, Lindi, Morogoro, Kigoma na Rukwa.

Aidha, pia wamo wafanyakazi wawili kutoka Iringa waliohamishiwa Kinondoni Dar es Salaam, mmoja kutoka Iringa kwenda Ilala, Kisarawe kwenda Shinyanga na Bagamoyo kwenda Ruvuma.

Ingawa mkurugenzi huyo alikataa kuzungumzia sababu za kuhamishwa kwa mkupuo kwa watumishi hao, lakini kwa muda mrefu tangu Waziri Mkuu Kassim Majaliwa afanye ziara ya kushtukiza katika Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA) Novemba mwaka jana, kumekuwa na msukosuko pia katika TRA.

Baada ya kukuta uozo wa kashfa ya ufisadi wa makontena, Waziri Mkuu huyo aliamuru kusimamishwa kwa Kamishna Mkuu wa TRA, Rished Bade baada ya kubaini kupitishwa kwa makontena zaidi ya 300 bandarini bila kulipa kodi na kusababishia hasara Serikali ya zaidi ya Sh bilioni 80.

Pamoja na hayo, maofisa wote wa TRA ambao walihusishwa na sakata hilo walitakiwa kutosafiri nje ya nchi na kukabidhi hati zao za kusafiria mpaka pale uchunguzi dhidi yao utakapokamilika.

Aidha, miongoni mwao tayari wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakihusishwa na uzembe uliosababisha kutoroshwa kwa makontena TPA bila ya kulipiwa ushuru.
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top