Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

WATANZANIA TUAMINI UKWELI NA MSEMAKWELI, TUKATAE MANENO MATAMU



Kama kuna jambo baya ambalo baadhi ya Watu wanaoneka kulipenda sana nakuamini ni kuongopewa kwa maneno matamu ya kisiasa ambayo huwa hayana uhai wala afya ya kuendelea huku Watu wengine wakishindwa kumuamini au kumpenda mtu msemakweli asiyependa kuchezea akili zao kwa kuwaongopea.

Maneno mengi ya kufurahisha hadharani aghalabu huwa hayana mwisho mwema na wala huwa hayaleti tija au manufaa kwa jamii. Waswahili husema ni heri mtu asemaye kweli na kutetea haki za wengi kuliko anayeongopa kwa kutumia lugha tamu isioleta mafanikio. 

Miongoni mwa viongozi wasema kweli ambao hawapendi  kudanganya Wananchi ni Rais John Pombe Magufuli. Kweli atasema na kusimamia ukweli, njano atasema hii ni njano na wala siyo nyeusi. Kwa jambo lisilowezekana kwa wakati husika hatamung'unya maneno ila yuko tayari msimuelewe kwa wakati  huo kuliko kuongopa. 

Wote tunajua Rais wetu amejitolea muhanga kupigania maslahi mapana ya Taifa letu huku akitaka rasilimali na maliasili za nchi ziwanufaishe wananchi wote hususan watu masikini na wanyonge walioko vijijini ambao wanaokosa huduma bora za jamii. 

Ukiisikiliza kwa umakini hotuba ya Rais wakati akizumgumzia kwenye mkutano wa 33 Jumuiya ya Serikali za Mitaa Nchini (ALAT), utajua anajua jinsi michezo michafu ya  fedha za umma ambazo ni ruzuku toka Serikali kuu zilivyopotea au kutafunwa kiholela na wajanja wachache kwenye halmashauri za wilaya. 

Kwenye hotuba yake amehimiza na kuweka msisitizo huku akiwataka watendaji wa halmashauri za wilaya, Wakurugenzi, Wakuu wa idara na Madiwani, kuongozwa na shime ya uzalendo ili kuijenga nchi yetu kwa kufuata sheria na kuheshimu  misingi ya uaminifu, uadilifu, uwazi na uwajibikaji. 

Rais anaonekana dhahiri kutambua shida na dhiki zinazowakabili  Wafanyakazi, si wale tu walioko kwenye utumishi wa umma peke yake. Anajua kuna Waganga na Wauguzi, Walimu wa shule za Msingi na Sekondari, wataalam wa ugani kwa maana ya Mabwana na Mabibi shamba, Mabwana na Mabibi afya, Wahandisi na Maafisa wa maendeleo ya jamii. 

Kuna watumishi wa umma kwenye ngazi za Serikali kuu na kwenye Serikali za Mitaa, Wafanyakazi   wa Majumbani, Walinzi, Madereva, Wahudumu wa baa na wanaofanya kazi kwenye hoteli za kitalii ambao pia wanaolipwa ujira na mishahara hafifu. 

Makundi yote hayo na mengine, kimsingi yanahitaji kutazamwa kwa macho ya kusaidiwa na kulindwa  haki zao chini ya usimamizi wa Serikali kwa mujibu wa sheria ili waweze kupata stahili zao zitakazoweza kuendesha maisha yao aidha wanapokuwa kazini au baada ya kustaafu.

Ili hayo na mengine mengi yaweze kufikiwa, Serikali inahitaji kukusanya mapato kwa uhakika. Anataka kusiwe na upotevu unaovujisha mapato hayo na kupotea  hovyo lakini pia kile kidogo kinachopatikana kilindwe ili kiwanufaishe Wananchi wote. 

Nchi yetu kwa miaka mingi imepata pigo na matatizo ya kuwepo  kundi la  mafisadi, wabadhirifu wa mali za umma, wezi na matapeli waliokuwa wakipata vipato na kutajirika huku wakiiba fedha za Serikali na kujinufaisha wao binafsi . 

Leo kama Rais atasimama hadharani akatoa maneno laini ya kisiasa ili kuwafurahisha watumishi kwenye Serikali za Mitaa wakati yapo makundi mengine bado stahili zao hazijatizamwa na kurekebishwa kimanufaa, huo utakuwa ni uongo mpya mweupe. 

Katika maelezo yake amesema, anazungumza na watumishi wa Serikali za mitaa si kwa lengo la kuwaongezea mishahara, huo ndiyo ukweli. Aongeze mishahara kwa watumishi wa kundi hilo je watumishi wengine watalipwa na nani? 

Tuna Walimu wanaoishi vijijini wakiwa hawana nyumba za kuishi, huko vijijni hakuna maji safi na salama, hawajui umeme unawakaje, barabara  ni mbovu hazipitiki, hawana zahanati, kama zipo hazina Waganga na Wauguzi, zimekosa dawa na vifaa tiba huku kina mama wajawazito wakipoteza maisha.

Mabwana na Mabibi shamba hawana nyenzo wala usafiri, maafisa uvuvi na mifugo wakikabiliwa na upungufu mkubwa wa zana za uendeshaji wa shughuli muhimu  kwa Wananchi ili kuwapa taaluma aidha katika sekta za uvuvi, kilimo cha kisasa na ufugaji wenye tija na manufaa.

Vijijini kina Mama Wajawazito na Watoto chini ya umri wa miaka  mitano wanahitaji chanjo na kinga, vifaa tiba na huduma bora vya upimaji wa afya zao karibu kila wiki wakitakiwa kufika zahanati na kliniki ili kujua maendeleo ya afya zao .

Vijijini wakulima hawapa pembejeo za kilimo na mifugo kwa wakati muafaka, hawana zana za kisasa ikiwemo matrekta, hadi sasa katika karne ya 21 watu bado  wanatumia kijembe cha mkono kulima zaidi ekari tano huku wajanja wachache wakitafuna fedha za umma na kujenga mahekalu na nyumba za kifahari. 

Katika Shule za Msingi na Sekondari huko vijijini watu zinakabiliwa na upungufu wa madarasa, maabara, idadi ndogo ya  Walimu, hakuna  mashimo ya vyoo, hawapati  maji safi na salama,  kuna magonjwa ya milipuko kama kipindupindu, matumbo ya kuharisha, malaria na maambukizi ya virusi vya ukimwi .

Rais anayejua shida, dhiki na matatizo ya Wananchi wake katu hawezi kuwa muongo au mnafik wa kulifurahisha kundi moja la Wafanyakazi ili wampigie makofi, nderemo na vigelegele vya uzandiki wakati kwenye maeneo mengine ya nchi yake kuna shida kubwa na matatizo yasiyokadirika.

Rais Dk Magufuli amehimiza na kuwataka Watumishi waliopewa dhamama za utendaji wakiwemo Madiwani, Wakurugenzi wa halmashauri za wilaya na wakuu wa idara, kujali uzalendo na utaifa. Kulinda na kutunza vyema fedha za umma na kuitumia vizuri  kwa kadri ya miradi yote ilivyopangiwa, kuidhinishwa na vikao utekekezaji wake utoe matokeo chanya.

Mataifa ya wenzetu kama China, Taiwan, Malaysia, Vietnam, India, Dubai, Oman au Hong Kong, kwanza yaliweka kando siasa , wakatupa pembeni  maneno maneno na uongo hatimaye yakaongozwa na ukweli hadi kufika mahali walipo sasa kimaendeleo kwa kujali uzalendo na dhima ya kupigania maendeleo ya kiuchumi . 

Kwa kukataa uongo na kwa kutambua hayo yote Rais Dk Magufuli amesema Serikali yake itashughulikia mishahara ya Walimu na Wafanyakazi wote, katika bajeti ijayo ataongeza mishahara ya kawaida kwa Wafanyakazi (annual increments)  maana ilisimama kwa muda mrefu.

Kwa kawaida na ada ya mtu msemakweli na asiyependa uongo, amesimama na kusema analoliamini kuwa hajapandisha mishahara na hatapandisha mishahara kwa wakati huu. Alichaguliwa ili kusaidia wananchi wanyonge walioko vijijini na mijini nao wapate huduma bora. Jukumu la Rais yeyote bora mwenye uzalendo  ni kuweka mkazo katika utoaji wa huduma kwa wananchi wote. 

Kimsingi, kimantiki na kiuhalisia maneno hayo hutamkwa na Rais mwenye nia na dhamira njema  yenye muhimu au ulazima na dhati ya kuyatazama maisha ya Wananchi wengi masikini, wanaokosa huduma bora, wenye dhiki, shida na matatizo ya kukosa elimu ili kufuta ujinga, wanaondamwa na adui umasikini pamoja na kusakamwa na maradhi .

Wapo wanasiasa waliozoea kuwadanganya wananchi wakati wa kampeni na wengine hata kufikia kusema na kuahidi wakichaguliwa watajenga mabomba yatakayotoa maziwa na asali, kujenga barabara za lami, watakaotibiwa hapa hapa nchi huku wanapoumwa huenda nje ya nchi kwa matibabu na wengine wapo waliodai wana uwezo wa kuleta mabadiliko ya kiuchumi wa siku mia moja.

Pia wapo Waandishi wadaku, wakuda na wajuba wasio na mioyo ya uzalendo ambao nao wameanza kupotosha maana na msingi wa matamshi ya Rais ili kueneza na kuendeleza utamaduni wa kupika uongo  kwa jamii huku wakimlisha maneno ambayo hayakuyatamka .
Jambo muhimu kwa Watanzania wote, tutambue kuwa wakati umefika tukatae maneno matamu ya kisiasa yenye siha hafifu na uongo mwingi, afya duni ya muda mfupi huku tukibadilika na tukimtambua mtu msemakweli na mwenye dhati ya kujenga Taifa la watu wenye lengo la kujikwamua na madhia ya umasikini hatimaye kujitegemea. 


Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top