MKUU WA MKOA 
Dodoma, Dk. Rehema Nchimbi amewataka wanafunzi wa vyuo vya 
elimu ya juu walioko katika mkoa huo kujihoji 
nafsi zao na kucheki matendo yao kama kweli ni ya kumpendeza Mungu kwa vile 
ndiyo yanachangia wao kutotambua umuhimu wa nafasi 
walizonazo.
Dk. Nchimbi ametoa kauli hiyo 
mwishoni mwa wiki wakati akihutubia maelfu ya wanavyuo waliohudhuria Jumuiko la 
Wanavyuo wa Dodoma (Dodoma Campus Night) lililoambatana na mkesha wa 
kusifu na kuabudu uliofanyika kwenye ukumbi wa Chimwaga mjini 
Dodoma.
Jumuiko hilo lilihudhuriwa na wanafunzi 
zaidi ya 3,500 wa dini mbalimbali kutoka vyuo vikuu vya Dodoma (UDOM), St. 
John’s, Vyuo vya Mipango, Madini, Mirembe, Hombolo, Chuo cha Elimu ya Biashara 
(CBE) na vyuo vya ualimu vya Mitumba na Capital.
Dk. Nchimbi alisema wanavyuo wengi ambao 
walifaulu kidato cha sita kwa alama za juu (first class) huwa wanaporomoka 
kimasomo wanapoingia kwenye vyuo vya elimu ya juu kwa sababu hawajiweki sawa 
kwenye mahusiano yao na Mungu aliyewaumba. “Wanaharibikiwa kwa sababu hawajiweki 
sawa na Mungu… hawakai pale ambapo Mungu anataka wawe (their right position),” 
alisema.
“Tunzeni nafasi zenu ambazo Mungu 
amewapatia… uwingi wenu huu katika usiku wa leo hauna maana kama hatutakuwa na 
uhusiano mwema na Mungu kwani hata shetani ana watu wake na huwa anawapatia 
mahitaji yote… kila mmoja wenu aanze upya na Mungu”, 
alisema.
“Tumfikirie Mungu, tuangalie mahusiano yetu 
na Mungu wetu yakoje na tumuombe atusaidie katika yote tuyatendayo, naye 
atatujibu kwa sababu Mungu huwa hawekezi kwa hasara bali huwekeza kwa faida,” 
alisema huku akishangiliwa na wanafunzi waliokuwa wamefurika kwenye ukumbi 
huo.
Alisema idadi kubwa ya wanavyuo wakishapata 
fedha za mkopo hutumbua maisha kwenye vilabu vya muziki ambavyo ni maarufu mjini 
humo kama vile  Club 84, Club La Aziz na Maisha Club na hawarudi vyuoni hadi 
fedha yote imekwisha.
“Mungu alipofanya uumbaji alisema kila 
alichokifanya ni chema sana. Sasa kama wewe ni kiumbe chema wa Mungu iweje uende 
kwenye hizo club kuponda maisha, iweje unywe pombe, iweje ufanye uzinzi na 
uasherati badala ya kukaa chuoni ukasoma, iweje ugome kufanya mtihani hadi upate 
‘kibuti’?, alihoji huku akishangiliwa na wanavyuo 
hao.
Alisema yeye kama mzazi analazimika kuyasema 
hayo kwa sababu anatambua kuwa watoto wa leo wamezungukwa na mitego mingi. 
“Hatutaki shetani awachezee, ndiyo maana tunawaonya,” 
alisisitiza.
Alisema katika kundi kubwa kama hilo wamo 
viongozi wa kesho na kwamba wasipojihadhari na kuweka mahusiano yao sawa na 
Mungu kuanzia sasa, watajikuta wanafanana na baadhi ya viongozi nchini ambao 
wamekabidhiwa dhamana lakini wanakengeuka na kufanya kinyume na matarajio ya 
wengi.
Akitoa mfano alisema: “Nchi hii wako wasomi 
wengi lakini wamekaa kiwiziwizi tu, fedha za barabara zikitolewa haziendi 
kufanya kazi iliyopangwa, wakurugenzi wakipewa fedha za kujenga shule, mabweni 
au nyumba za walimu, unakuta zinakamilika lakini ziko chini ya kiwango, 
madaktari nao wanaiba dawa za hospitali kwa kutumia magari ya kubebea 
wagonjwa.”
“Kama viongozi hawa wangesimama kwenye 
nafasi zao (right position) haya mambo yangetoka wapi? Mambo ya mikataba mibovu 
yangetoka wapi? Mnadhani nchi hii ingekuwa maskini? Haiwezekani!” alisisitiza 
huku akishangiliwa na wanavyuo hao.
Aliwasihi wanavyuo wote watambue nafasi zao 
na wazitunze nafasi hizo ili wasimkosee Mungu. “Tunzeni nafasi zenu mlizopewa na 
Mungu na wakati wote jitahidini kusikiliza sauti yake, muone jinsi 
atakavyowashindia”, alisema.
Mapema, akimkaribisha Mkuu wa Mkoa 
kuzungumza na wanafunzi hao, Mchungaji Gerald ole Nguyaine wa Kanisa la ICC –TAG 
Dodoma alisema wanafunzi walio katika vyuo hivyo ni wababa na wamama wa kesho 
hivyo hawana budi kumtanguliza Mungu katika yote 
wayafanyayo.
Naye Mchungaji Gavin Walker kutoka Kanisa la 
Calvary Christian Fellowship lililoko Columbus, Ohio, Marekani ambaye alikuwa 
mnenaji mkuu katika mkesha huo, aliwasihi wanavyuo kutambua makusudi ya Mungu 
ambayo ameyaweka juu yao. “Mungu amekuumba wewe kwa kusudi maalum hivyo ni 
lazima ujue hilo kusudi”, alisema.
Alisema kwa kutotambua kusudi la Mungu 
katika maisha yao, wako watu ambao wamejikuta wakitaka kufanana na wengine bila 
kujua ni kwa nini watu hao wamekuwa hivyo. “Wanatamani nafasi za wengine kwa 
sababu tu wao ni maarufu, ni waigizaji, ni wacheza sinema ama wasanii…  hapana! 
Kila mmoja anatakiwa kujua kusudi ka Mungu katika maisha yake,” 
alisisitiza.
Alisema duniani kuna wakazi zaidi ya bilioni 
saba lakini wengi kati ya hao wanaishi maisha yasiyotimilika kwa sababu hawamjui 
Mungu. “Hakuna kitu ambacho Mungu hawezi kukifanya maishani mwetu, tunachotakiwa 
ni kumuomba tu! Kama ni masomo soma kwa bidii huku ukimtumaini Mungu, nawe 
utashinda sababu Mungu yuko upande wako,” 
alisisitiza.
Aliwaasa wawe wavumilivu wawapo vyuoni. 
“Katika maisha ya chuo jifunze kuwa na saburi. Ukijenga saburi sasa hivi tangu 
uko chuoni, itakusaidia kuvumilia mengi katika maisha ya mbele baada ya kuhitimu 
Chuo Kikuu au chuo chochote unachosoma sasa,” alisisitiza.


Post a Comment