Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

SIRI YA USHINDI WA WASSIRA NEC CCM WAANIKWA

USHINDI wa kishindo ambao ameupata Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Stephen Wassira katika nafasi kumi za ujumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM, unaelezwa kuwa unatokana na yeye kutokuwa katika kambi yoyote iliyopo katika chama hicho.

Vilevile, ushindi wa Wassira ambaye aliibuka kidedea kwa kuzoa kura 2,135,unatokana kumudu jukwaa wakati wa kujieleza na kuonyesha kuwa yeye ni mwarobaini kwa wapinzani hususan Chadema.

Wakati akijinadi mbele ya wajumbe kabla ya kupigiwa kura, Wassira aliomba apewe nafasi hiyo ya ujumbe wa Nec, ili apeleke kilio Chadema.

“Nipeni kura nipate nafasi ili nipeleke kilio Chadema,” alisema Wassira huku akishangiliwa wakati akiomba kura na Rais Jakaya Kikwete akimwita kwa jina la utani, Tyson.

Baadhi ya makada wa CCM waliliambia gazeti hili kwamba kete ya kuwashughulikia Chadema, ‘ilimbeba’ Wassira ikizingatiwa kwamba chama hicho cha upinzani ndicho kinachowakosesha CCM usingizi.

Wassira ambaye aliwahi kuwa mbunge wa upinzani kupitia Chama cha NCCR-Mageuzi, hivi sasa ni mmoja kati ya makada tegemeo wa CCM na katika siku za karibuni amekuwa mstari wa mbele katika shughuli zote za chama hicho hasa za utatuzi wa migogoro na pale chama chake kinapohitaji utetezi mbele ya vyama vya upinzani.

Miongoni mwa shughuli hizo ni kuwa mmoja wa walioongoza kampeni za CCM katika chaguzi ndogo za Igunga na Arumeru Mashariki, ambako alitumia muda mrefu kukishambulia Chadema na viongozi wake. Pia kushughulikia mgogoro ndani ya CCM mkoani Arusha na bungeni amekuwa akiongoza kujibu hoja za wapinzani, ingawa umma umekuwa ukikosoa kauli zake za mara kwa mara.

Habari zilizopatikana zinaeleza kwamba sababu nyingine ya Wassira kupata kura nyingi ni kutokana na yeye kutokuwa katika kambi ya makundi ya kuusaka urais wa 2015 yaliyopo ndani ya CCM.

Pia nafasi yake ya uwaziri anayehusika na mambo ya siasa, inatajwa kwamba imempa nafasi ya kuwa karibu na viongozi wengi wa CCM kuanzia ngazi ya taifa hadi wilayani.

Mjumbe wa Mkutano Mkuu, kutoka Mkoa wa Morogoro, Semindu Pawa alisema kuwa ushindi wa kishindo wa Wassira unatokana na yeye wakati wa kiujieleza kumudu jukwaa.

Semindu Pawa ambaye ni Mbunge wa zamani wa Morogoro Kusini Mashariki alisema, Wassira alijua namna ya kutumia muda kwani alikuja na kauli ambayo iliwafurahisha wajumbe ya kueleza kuwa apewe nafasi hiyo ili apeleke kilio kwa Chadema.

Kauli ya Wassira
Alipoulizwa siri ya ushindi wake mkubwa ndani ya chama hicho, Wassira alisema: “Kilichonipa ushindi ni msimamo wangu wa kutotegemea kundi lolote na ukweli wangu ndani ya chama.”

Wassira alijinasibu kuwa yeye ni lulu ndani ya CCM na wakati wote amekuwa ni muumini wa ukweli huo bila ya kuyumba na kila mara amekuwa ni mjenga hoja za ukweli.

Alisema kuwa hata pale ambapo CCM kimekuwa kikitukanwa na wapinzani huwa anapeleka majibu ya hoja siyo matusi kama ambavyo wengine hufanya.

“Niliamini kuwa lazima nishinde na kweli ninawashukuru wajumbe kwa kuwa mimi ndiyo mwarobaini wa chama kwa wapinzani wetu, lazima tuwe pamoja na tutaendelea kuwa pamoja,” alisisitiza.

Makundi ndani ya chama hicho yanaelezwa kuwa yanatokana na mbio za kuwania urais katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.

Makundi haya ambayo tayari yamekigawa chama hicho, yamemfanya Mwenyekiti wa CCM, Rais Kikwete kuonya kuwa yanaweza kukimaliza chama hicho ikiwa hayataondoshwa.

Wassira aliongoza katika uchaguzi huo na kuwashinda baadhi ya vigogo wakiwamo Waziri wa Nchi ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe na Katibu Mkuu wa CCM, Wilson Mukama.

Chanzo: Mwananchi
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top