Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) 
linatoa pongezi kwa timu ya Azam ya Tanzania Bara kwa kufanikiwa kusonga mbele 
katika michuano ya Kombe la Shirikisho iliyo chini ya Shirikisho la Mpira wa 
Miguu Afrika (CAF).
Ushindi wa jumla ya mabao 8-1 ambao Azam 
imeupata dhidi ya Al Nasir Juba ya Sudan Kusini si fahari kwa timu hiyo tu, bali 
Tanzania kwa ujumla, na unaonyesha jinsi klabu hiyo ilivyojipanga kiushindani 
katika michuano hiyo ya Afrika.
Hata hivyo, ni vizuri Bodi ya Wakurugenzi ya 
klabu hiyo, benchi la ufundi na wachezaji wa timu hiyo wakautazama ushindi huo 
kama changamoto kwao kuhakikisha wanajipanga vizuri zaidi kwa raundi 
inayofuata.
Timu ya Azam inayofundishwa na Mwingereza John 
Stewart Hall ilishinda nyumbani mechi ya kwanza mabao 3-1, na jana kuibuka na 
ushindi wa mabao 5-0 ugenini jijini Juba.
Kwa kufanikiwa kuing’oa Al Nasir Juba, Azam sasa 
watacheza raundi ya kwanza (raundi ya 16 bora) ya michuano dhidi ya Barrack 
Y.C.II ya Liberia ambayo katika raundi ya awali iliitoa Johansens ya Sierra 
Leone. Barrack ilishinda bao 1-0 nyumbani katika mechi ya kwanza na kulazimisha 
suluhu katika mechi ya marudiano jijini Freetown.
Azam itaanzia mechi hiyo ugenini kati ya Machi 
15,16 na 17 mwaka huu wakati mechi ya marudiano itachezwa Tanzania kati ya 
Aprili 5,6 na 7 mwaka huu.
Boniface 
Wambura
Ofisa 
Habari
Shirikisho la Mpira wa 
Miguu Tanzania (TFF)



Post a Comment