*******
Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, vitalazimika kufanya mabadiliko katika safu zake za uongozi
kutokana na athari zilizosababishwa na mabadiliko yaliyofanywa na Rais
Jakaya Kikwete katika Baraza la Mawaziri.
Juzi, Ikulu ilitangaza mabadiliko katika baraza
hilo ambayo yaliwaweka kando mawaziri na manaibu waziri watano, huku
sura kumi mpya zikiingia, mabadiliko ambayo yameacha nafasi mbili wazi
katika sekretarieti ya CCM na nafasi nne katika uongozi wa Bunge.
Miongoni mwa walioteuliwa na kuapishwa jana ni
waliokuwa wajumbe wa Sekretarieti ya CCM; Dk Asha-Rose Migiro ambaye
ameteuliwa kuwa Waziri wa Katiba na Sheria na Mwigulu Nchemba ambaye
ameteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Fedha.
Nchemba ni Naibu Katibu Mkuu wa CCM Tanzania Bara,
wakati Dk Migiro ni Katibu wa Halmashauri Kuu ya chama hicho, Siasa na
Uhusiano wa Kimataifa.
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nauye
alisema jana kuwa viongozi wa sekretarieti ya CCM wanapoteuliwa kushika
nafasi nyingine za Serikali, wanalazimika kuziacha nyadhifa zao katika
chama.
Nape alisema kwa maana hiyo, Mwenyekiti wa CCM,
Rais Kikwete atalazimika kuteua watu wa kuziba nafasi za Dk Migiro na
Nchemba. “Huu ni utaratibu tuliojiwekea katika chama kwamba viongozi wa
sekretarieti hawatafanya kazi mbili za chama na Serikali, kwa hiyo
viongozi hawa pia wataziacha nafasi za chama,” alisema Nape.
Hata hivyo Nape alisema utaratibu huo hauwagusi
wenyeviti wa chama hicho wa mikoa, ambao wameteuliwa kuwa mawaziri ama
manaibu waziri kwani uenyekiti si nafasi ya utendaji.
Katika uteuzi huo, Mwenyekiti wa CCM, mkoa wa
Simiyu, Dk Titus Kamani aliteuliwa kuwa Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na
Uvuvi, wakati Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mbeya, Godfrey Zambi aliteuliwa
kuwa Naibu Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika.
“Hawa wanaweza kuendelea na nyadhifa zao za
uenyeviti katika chama, huku wakiwa na nyadhifa serikalini, hii haina
athari kwa sababu siyo watendaji wakuu wa chama,” alisema Nape.
Bungeni
Bunge pia litalazimika kuchukua hatua za kuziba
nafasi zilizoachwa wazi na aliyekuwa Mwenyekiti wa Bunge pia Kiongozi
wa Kamati ya Maendeleo ya Jamii, Jenister Mhagama ambaye ameteuliwa kuwa
Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi.
Wengine ni Mahmoud Mgimwa aliyekuwa Mwenyekiti wa
Kamati ya Uchumi, Viwanda na Biashara na sasa ameteuliwa kuwa Naibu
Waziri wa Maliasili na Utalii na aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya
Katiba, Sheria na Utawala, Pindi Chana ambaye sasa ni Naibu Waziri wa
Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto.
MWANANCHI
Post a Comment