Ndugu Waandishi wa Habari.
Awali
ya yote napenda kuwakaribisha katika mkutano huu ambao nitaelezea
Mafanikio ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi katika kipindi cha
Serikali ya Awamu ya Nne.
Ukiacha
Idara za Utawala, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi inaundwa na Idara
kuu tano ambazo ni Jeshi la Polisi, Jeshi la Magereza, Jeshi la Zimamoto
na Uokoaji, Idara ya Uhamiaji na Idara ya Huduma kwa Jamii. Pia katika
Wizara yetu tuna Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa.
Majukumu
ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi ni kulinda usalama wa raia na mali
zao, kuhifadhi na kuwarekebisha wafungwa, kutoa huduma za zimamoto na
uokoaji, kudhibiti uingiaji na utokaji nchini kwa raia na wageni,
kusimamia utekelezaji wa Sheria ya Huduma kwa Jamii na kuandaa na kutoa
Vitambulisho vya Taifa.
Katika
kipindi cha Serikali ya Awamu ya Nne, Wizara yetu imefanikiwa
kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kuiwezesha nchi yetu kuwa na
amani na utulivu. Kwa wastani tunaweza kusema kuwa nchi yetu imekuwa na
usalama ambao umewawezesha wananchi na wageni kuendelea kufanya shughuli
zao za kijamii na kiuchumi, licha ya matukio ya hapa na pale, ambayo
Wizara inaendelea kuyachukulia hatua na kuyatafutia ufumbuzi.
Jeshi la Polisi:
Wizara
yetu, kwa kupitia Jeshi la Polisi, imeweza kudhibiti vitendo vya
uhalifu vilivyokuwa vimeanza kukithiri hapa nchini. Vitendo hivyo ni
pamoja na matukio ya ujambazi wa kutumia silaha, wizi katika mabenki,
mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi, yaani albino na makosa mengine ya
kijinai. Kwa mfano, kwa juhudi zilizofanywa na Wizara yetu, makosa ya
kuwania mali (unyang’anyi wa kutumia silaha, wizi katika mabenki,
uvunjaji, wizi wa mifugo n.k) yalipungua kutoka 53,268 mwaka 2005 hadi
45,470 mwaka 2013. Mengine yaliyopungua ni mauaji ya albino kutoka 20
mwaka 2008 hadi moja mwaka 2013. Watuhumiwa waliohusika katika matukio
haya walikamatwa na kuchukuliwa hatua za kisheria. Kwa ujumla kutokana
na juhudi zinazofanywa na Wizara, makosa makubwa ya jinai yamekuwa
yakipungua kwa wastani wa asilimia sita (6) kila mwaka.
Katika
juhudi za kuongeza nguvu kazi, idadi ya askari na askari wanafunzi
katika Jeshi la Polisi imeongezwa kutoka 26,000 mwaka 2006/2007 hadi
44,000 kufikia Desemba, 2013.
Nyumba
mpya 491 kwa ajili ya askari Polisi zimejengwa kote nchini yakiwemo
maghorofa 84 yaliyojengwa Dar es Salaam, matatu Zanzibar na mengine
matatu, Pemba. Pamoja na kuendelea na ujenzi katika maeneo mengine
nchini, Jeshi la Polisi limesaini makubaliano ya awali ya kutekeleza
mradi wa ujenzi wa nyumba 350 za kuishi askari katika mkoa wa Kipolisi
wa Kinondoni mara mkataba kati ya Jeshi la Polisi na Kampuni ya Mara
Group utakaposainiwa. Aidha kwa msaada wa Serikali ya Marekani, Chuo
cha Polisi Wanamaji kimejengwa mjini Mwanza.
Kwa
upande wa vitendea kazi, magari mapya 373 na pikipiki 1,128
zimenunuliwa. Boti 10, magari 97 na pikipiki 484 zimepatikana kutoka
kwa wafadhili na wadau mbalimbali ndani na nje ya nchi kwa ajili ya
kuimarisha operesheni za Jeshi la Polisi.
Jeshi la Magereza:
Katika
kuimarisha shughuli za utunzaji na urekebishaji wafungwa, Wizara
kupitia Jeshi la Magereza imefanikiwa kukarabati majengo na miundombinu
ya magereza, likiwemo Gereza lenye ulinzi mkali la Butimba, na ukarabati
wa majengo mengine ya ofisi za Utawala umefanyika katika magereza ya
Uyui, Lilungu, Maweni, Isanga, Keko na Ukonga. Ujenzi, ukarabati na
ukamilishaji wa mabweni ya wafungwa umefanywa katika magereza 24 nchini
kwa lengo la kuhakikisha kuwa usalama wa wafungwa unaimarishwa.
Aidha,
ujenzi wa jengo la ghorofa la kuishi familia 16 za askari katika Gereza
la Mahabusu Iringa umekamilika. Ujenzi wa nyumba za maofisa na askari
unaendelea katika magereza 17 nchini. Pia nyumba nne (4) pamoja majengo
na mengine matatu (3) yamenunuliwa kutoka Shirika la Reli Tanzania (TRC)
wilayani Lushoto mkoani Tanga kwa ajili ya matumizi ya Jeshi. Aidha
ukamilishaji wa nyumba zilizojengwa kwa njia ya ubunifu unaendelea
katika magereza 11 nchini.
Ili
kutoa nafasi zaidi kwa wafungwa wanaopokelewa magerezani, idadi ya
nafasi za kuwalaza wafungwa zimeongezwa kutoka 22,699 mwaka 2005 hadi
nafasi 29,552 mwaka 2011.
Jeshi
la Magereza pia limeanzisha na kutekeleza jukumu la kuwapeleka mahabusu
kwenda Mahakamani na kurudi gerezani kwa kutumia mabasi ya kisasa.
Zoezi hili lilianza rasmi tarehe 19 Mei, 2008 kwa mahabusu waliopo mkoa
wa Dar es Salaam na wale wa mkoa wa Pwani. Kwa sasa zoezi hili
limeendelezwa katika mikoa ya Arusha na baadhi ya wilaya za mkoa wa
Dodoma, na litaendelea kutekelezwa kwa awamu nchi nzima.
Mafunzo
mbalimbali yameendeshwa ndani ya Jeshi la Magereza na watumishi 5,889
walihitimu kozi mbalimbali hadi mwishoni mwa mwaka 2013.
Jeshi la Zimamoto na Uokoaji:
Katika
kukabiliana na majanga ya moto, Wizara kwa kupitia Jeshi la Zimamoto na
Uokoaji imeweza kupunguza majanga ya moto kwa kiasi kikubwa. Pia ofisi
za Zimamoto na Uokoaji zimeanzishwa katika mikoa yote nchini na
zinaongozwa na Makamanda wa Zimamoto wa Mkoa. Aidha vituo vipya vya
Zimamoto na Uokoaji vimejengwa katika maeneo ya Lugalo, wilaya ya
Kinondoni na Mchicha, wilaya ya Temeke Jijini Dar es Salaam, na vituo
vidogo katika maeneo ya Karatu, wilayani Karatu mkoani Manyara na Same,
wilayani Same mkoani Kilimanjaro.
Jumla
ya magari ya kuzima moto 25 yamenunuliwa na askari 379 na watumishi
raia 28 wameajiriwa. Ili kuongeza zaidi nguvu kazi, Ofisi ya Rais,
Menejimenti ya Utumishi wa Umma imetoa kibali cha kuajiri askari 800
katika mwaka wa fedha 2013/2014 na kazi hiyo imeshaanza.
Idara ya Uhamiaji:
Kwa
kupitia Idara ya Uhamiaji, Wizara imefanikiwa kutoa Pasi za Kusafiria
za kawaida 534,855, za kiutumishi 4,035, za ki-balozi 2,172, na za
Afrika Mashariki 13,220. Aidha katika kipindi cha mwezi Januari, 2006
hadi Desemba, 2013, imeweza kuwahudumia wageni 6,469,876 walioingia
nchini na 6,395,167 waliotoka nchini. Pia imeweza kutoa vibali 322,603
vya ukaazi na kutoa vibali vya uraia wa Tanzania kwa wageni 1,392.
Wahamiaji haramu 65,675 walikamatwa na kuchukuliwa hatua mbalimbali za
kisheria. Kati ya wahamiaji hao haramu, 31,203 walipatikana wakati wa
Operesheni Kimbunga, iliyotekelezwa kati ya mwezi Septemba na Oktoba
mwaka 2013. Aidha jumla ya raia wa Tanzania 2,770 waliokuwa wamezamia
nchi za nje walirejeshwa na kupokelewa nchini.
Kutokana
na shughuli mbalimbali zilizofanywa na Idara ya Uhamiaji, makusanyo ya
maduhuli ya serikali yaliongezeka kutoka shilingi bilioni 14.2 mwaka
2006/2007 hadi bilioni 83.4 mwaka 2013/2014. Ongezeko hili kubwa
lilitokana na juhudi zilizofanya na Serikali kuboresha mifumo ya
makusanyo ya maduhuli ya Serikali.
Ili
kuboresha huduma, jumla ya magari 192 yalipatikana, 93 kati ya hayo
ikiwa ni misaada ya wafadhili. Idara pia ilinunua pikipiki 206 na boti 2
ambazo hutumika katika misako na doria katika maeneo mbalimbali nchini.
Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa:
Wizara
kupitia Mamlaka ya Vitambulisho vy Taifa imezindua Mfumo wa Usajili na
Utambuzi wa watu nchini na Vitambulisho vya Taifa vimeanza kutolewa
mwezi Februari, 2013 kwa watumishi wa Serikali 290,000 walioko Dar es
Salaam na Zanzibar. Aidha, zoezi la kusajili wananchi limeanza katika
mikoa ya Dar es Salaam ambapo katika awamu ya kwanza jumla ya wananchi
2,159,822 wamesajiliwa jiji la Dar es Salaam na wengine 220,000 katika
Wilaya ya Kilombero mkoani Morogoro. Lengo ni kuendeleza kwa awamu zoezi
hili nchi nzima.
Idara ya Huduma kwa Jamii:
Idara
ya Huduma kwa jamii inasimamia utekelezaji wa Sheria ya Huduma kwa
Jamii ambayo inahusiana na utekelezaji wa adhabu mbadala ya vifungo
magerezani. Tangu mwaka 2006 hadi 2013, Wizara kupitia Idara hii imeweza
kufikisha huduma zake katika mikoa 17 kati ya 25 ya Tanzania Bara.
Jumla ya wafungwa 6,444, kati yao wanaume 5,940 na wanawake 504,
wamefaidika na adhabu mbadala ya vifungo magerezani, ambapo jumla ya
wafungwa 5,193 wamemaliza adhabu zao za kutumikia jamii.
Kutokana
na utekelezaji wa Sheria hii, Serikali imekuwa ikiokoa kiasi cha
shilingi 3,500 kila siku kwa kila mfungwa anayepangiwa kufanya kazi za
jamii badala ya kufungwa gerezani.
Kwa
upande wa kutoa elimu kwa wadau muhimu, Wizara kupitia Idara ya Huduma
kwa Jamii imeweza kuendesha Mafunzo mbalimbali kwa wadau hao ambao ni
Mahakimu, Waendesha Mashtaka, Wasajili wa Mahakama, Maafisa Usalama wa
Taifa, Maafisa Magereza, Polisi, Wakurugenzi wa Majiji, Manispaa, Miji
na Halmashauri katika mikoa 17 inayohusika.
Maboresho ya Miundo ya Idara za Wizara;
Jeshi la Polisi:
Wizara
imefanya maboresho ya Muundo wa Jeshi la Polisi ambapo nafasi ya Naibu
Inspekta Jenerali wa Polisi imeundwa na Divisheni za Jeshi hilo
zimeongezwa kutoka nne hadi nane, ambazo zote zinaongozwa na Makamishna
kama ifuatavyo:
1. Divisheni ya Utawala na Utumishi - (Administration & Personnel Division)
2. Divisheni ya Fedha na Usafirishaji – (Finance & Logistics Division)
3. Divisheni ya Operesheni na Mafunzo – (Operations & Training Division)
4. Divisheni ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai – (Criminal Investigation Division)
5. Divisheni ya Intelijensia ya Jinai – (Criminal Intelligence Division)
6. Divisheni ya Uchunguzi wa Ushahidi wa Jinai – (Forensic Investigation Division)
7. Divisheni ya Polisi Jamii – (Community Policing Division)
8. Divisheni ya Zanzibar – (Zanzibar Division)
Kabla ya hapo kulikuwa na Makamishna wanne tu wa:
1. Utawala na Rasilimali – (Finance and Administration)
2. Operesheni na Mafunzo – (Operations and Training)
3. Upelelezi wa Makosa ya Jinai – (Criminal Investigation)
4. Kamishna wa Polisi Zanzibar.
Maboresho haya yanategemewa kuleta mabadiliko makubwa katika utendaji wa Jeshi la Polisi.
Jeshi la Zimamoto na Uokoaji:
Vikosi
vyote vya Zimamoto na Uokoaji sasa vimewekwa chini ya Komandi moja ya
Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji. Kabla ya hapo
kulikuwa na vikosi chini ya Mamlaka mbalimbali, kama vile Mamlaka ya
Viwanja vya Ndege, Mamlaka ya Bandari, na Mamlaka za Halmashauri za Miji
na Majiji ambapo vikosi hivi vilikuwa na Komandi zinazojitegemea.
CHANGAMOTO:
Pamoja
na mafanikio tuliyopata bado kuna changamoto mbalimbali zinazokabili
utendaji wa shughuli za Wizara. Changamoto hizo ni pamoja na:
1) Ongezeko la kasi la mahitaji ya huduma ya ulinzi na usalama wa raia ikilinganishwa na rasilimali na vitendea kazi vilivyopo.
2) Kubadilika kwa mbinu za kutenda uhalifu.
3) Ongezeko la makosa makubwa na madogo yanayofanywa kwa njia ya mtandao (cyber crime).
4) Ufinyu
wa bajeti ambao unakwamisha utekelezaji wa baadhi ya majukumu na miradi
ya maendeleo, kama vile shughuli za ujenzi wa ofisi na makazi ya
watumishi na askari, ununuzi wa vifaa na dhana mbalimbali za kazi na
uhaba wa watumishi.
5) Ujenzi holela katika maeneo ya mijini, ambao unachangia kukwamisha juhudi za kuboresha huduma za zimamoto na uokoaji.
6) Kujengeka kwa tabia ya baadhi ya wananchi kujichukulia sheria mkononi na kufanya vitendo vya uhalifu.
MALENGO NA MASUALA YANAYOENDELEA KUFANYIWA KAZI:
i. Kuwa na Sera ya Kitaifa ya Usalama wa Raia. Rasimu ya Sera hii inaendelea kufanyiwa kazi na inategemewa kukamilika hivi karibuni..
ii. Kupunguza msongamano magerezani. Kutumia
njia mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuimarisha matumizi ya adhabu
mbadala ya kifungo, kama vile Vifungo vya Nje, Adhabu ya Huduma kwa
Jamii na Parole, na kushirikiana kikamilifu na wadau wengine kuhakikisha
kuwa usikilizwaji wa kesi zinazowasilishwa unaharakishwa.
iii. Kuwa na Sheria ya Taifa ya Uhamiaji – Waraka
wa mapendekezo ya kutunga Sheria ya Taifa ya Uhamiaji umepelekwa kwa
Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ili kupata maoni kabla ya kuendelea na
utaratibu wa kuuwasilisha kwenye Baraza la Mawaziri.
iv. Kuwa na Sera ya Taifa ya Uhamiaji na Uraia – Rasimu ya Sera hii pia imepelekwa kwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kupata maoni ili kufikia muafaka wa kuikamilisha.
v. Matumizi ya Uhamiaji Mtandao –
Maandalizi yameanza kwa ajili ya kutoa huduma zote za kiuhamiaji kwa
kutumia mfumo wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano. Hadi sasa
upembuzi yakinifu wa mfumo huo umekamilika na mchakato wa kumtafuta
mzabuni wa kutekeleza kazi hiyo umeanza.
vi. Kujenga vituo vitano (5) vya Zimamoto katika maeneo mbalimbali ya jiji la Dar es Salaam – Lengo ni kuzipeleka karibu kwa wananchi huduma za Zimamoto na Uokoaji.
vii. Kushirikiana na Mipango Miji – Kuhakikisha kuwa miji yetu mikubwa na midogo inapangwa vizuri ili kurahisisha huduma za Zimamoto na Uokoaji.
viii. Kujenga Ofisi za Utambuzi na Usajili wa watu (2014/2015) –
Wizara kupitia Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa ina mpango wa kujenga
Ofisi za Utambuzi katika wilaya 45 za Tanzania Bara na tano (5) za
Zanzibar ili kuharakisha zoezi la utambuzi na usajili wa watu kwa ajili
ya kuandaa Vitambulisho vya Taifa.
Hata
hivyo, ni lazima kueleza kuwa mafanikio ya Wizara yetu kwa kiasi
kikubwa yamepatikana kutokana na ushirikiano wa wananchi na wadau
wengine ambao kila mara wamekuwa wakitoa michango yao ya hali na mali.
Ili kuendelea kupata mafanikio na kutekeleza mipango yetu ya baadaye kwa
ufanisi zaidi, Wizara yetu itategemea ushirikiano wa wananchi kupitia
mikakati yetu mbalimbali kama ile ya Polisi Jamii na Ulinzi Shirikishi
na mingineyo.
Kwa
kupitia mkutano huu napenda kutoa shukrani za dhati kwa wananchi na
wadau wengine wote ambao mara zote wamekuwa wakisaidiana na Wizara yetu
kuhakikisha kuwa nchi yetu inakuwa na amani na utulivu na naomba
ushirikiano huu uimarishwe zaidi katika siku zijazo.
Ahsanteni kwa kunisikiliza.
Post a Comment