Wakati kamati ya nidhamu ya shirikisho la soka duniani FIFA ikimtaka
mshambuliaji wa timu ya taifa ya Uruguay Luis Suarez, pamoja na
shirikisho la soka la nchi hiyo kuwasilisha ushahidi wa kupinga shutuma
za kumng’ata beki wa timu ya taifa ya Italia ya Gorgio Chiellini, kabla
ya saa kumi na moja kwa saa za nchini Brazil, mshambuliaji huyo ameanza
kujitetea kupitia vyombo vya habari.
Luis Suarez, ambaye amechukuwa nafasi kubwa katika vyombo vya habari
hii leo kufuatia tukio la kumng’ata mchezaji wa Italia wakati akiwa
kwenye majukumu ya kulitetea taifa lake hapo jana, amesema anashangazwa
na taarifa zinazoendelea kuandikwa na kuzungumzwa kwenye vyombo vya
habari.
Suarez, amesema hakumng’ata Chiellini kama mashabiki wanavyopokea
taarifa hizo, bali waligongana kwa bahati mbaya na beki huyo wa klabu
bingwa nchini Italia Juventus, hivyo kinachoendelea dhidi yake kwa sasa
anakichukua kama uonevu wa kutaka apewe adhabu kali kutoka FIFA.
“Nakumbuka tukio lilivyokuwa, wakati mpira uliopigwa kutoka sehemu
ya kulia kwangu ukiwa angani nilikuwa nautazama, hivyo sikuangalia
pembeni na sikujua nani anakuja kunikabili, lakini nilipogeuka
nilikutana na Chiellini na kwa bahati mbaya niligongana nae katika
sehemu za bega lake la upande wa kushoto. Amesema Suarez.
Wakati
FIFA kupitia kamati ya nidhamu ikisubiri ushahidi wa Luis Suarez kwa
njia ya maandishi, imeanza kuhisiwa huenda mshambuliaji huyo wa klabu ya
Liverpool ya nchini Uingereza akaadhibiwa kwa kufungiwa kucheza michezo
kadhaa ambayo itakuwa chini ya shirikisho hilo.
Post a Comment