Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

CCM YALAANI MAALIM SEIF NA CUF KUTANGAZA USHINDI

 
Chama cha Mapinduzi (CCM) kimelaani vikali kitendo cha Mgombea Urais wa Zanzibar kupitia Chama cha Wananchi (CUF) kujitangaza mshindi kinyume na sheria ya Uchaguzi huku ikiishangaa Tume ya Uchaguzi Zanzibar-ZEC kwa kukaa kimya dhidi ya kitendo hicho.

Akizungumza na waandishi wa habari jioni hii, Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai amesema kitendo cha Maalim Seif kujitangaza mshindi kimekiuka sheria ya uchaguzi na kuhoji dhamira ya kiongozi huyo kufanya hivyo.

“Ni tukio la kushitusha sana na hatujui malengo ya kitendo hiki au anataka kuitia nchi katika mtafaruku?” Alihoji Vuai na kuitaka ZEC itekeleze majukumu yake kwa kuzingatia Katiba na Sheria.

Katika mkutano huo, Vuai alieleza kusikitishwa kwake na baadhi ya matukio yaliyotawala uchaguzi huo ambayo aliyaeleza kuwa yalilenga kukihujumu chama hicho ili kuharibu ushindi wa wagombea wake.

“Huko Pemba katika jimbo la uchaguzi la Chonga wakala wa CUF alikamatwa na karatasi za kupigia kura akishirikiana na afisa wa Tume” alieleza Vuai na kuhoji ni kura ngapi zimepita bila ya kugunduliwa.

Aidha, chama hicho kilieleza kitendo cha wakala wake wote katika Wilaya za Magharibi ‘A’ & ‘B’ kutopewa vitambulisho kilikuwa na lengo la kuharibu ushindi wa chama hicho kwa kuwa ZEC iliruhusu uchaguzi kuendelea kwa muda mrefu bila ya kuwepo mawakala wake.

“Tulikwenda Tume tarehe 24 Oktoba, 2015 tukahakikishiwa na kwa kuviona vitambulisho vya mawakala wa vyama vyote, lakini siku iliyofuata tulipokwenda kuvichukua vyetu tukaambiwa havionekani” alifafanua Vuai na kuhoji kilichotokea baina ya upigaji wa kura ulipoanza saa moja hadi wakala wa kwanza kupata kitambulisho baada ya saa karibu nne ambapo sehemu nyingine wakala wao walifika saa saba hawajapata vitambulisho.

Alipoulizwa kuwa malalamiko hayo yanamaanisha chama chake hakina imani na ZEC, Naibu Katibu Mkuu huyo aliwaeleza waandishi wa habari kuwa chama chake bado kinaiamini Tume hiyo lakini inaikumbusha wajibu wake.

“CCM ni chama kikubwa,tujiulize kama tukio hili lingewakuta wenzetu wa CUF ingekuwaje. Kwa nini vitambulisho vyetu vipotee katika eneo lenye wapiga kura wengi zaidi kuliko sehemu nyingie yeyote Zanzibar”alifafanua Vuai na kuongeza kuwa wajibu wa kutii sheria ni wa kila mtu na kila chombo hivyo isingekuwa busara kwa CCM kukaa kimya kwa yaliyotokea.

Wakati huo huo, Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, Shamsi Vuai Nahodha amesema kitendo cha Maalim Seif kutangaza matokeo ni njama za kuishinikiza Tume ya Uchaguzi kufuata matakwa yao.

“Kitendo cha Maalim kujitangazia ushindi ni njama za kuishinikiza ZEC ifanye kile inachokitaka. Tungeelewa kama wajumbe wa ZEC kutoka chama cha CUF wangekuwa wamejizulu”alieleza Shamsi wakati wa kujibu maswali kutoka kwa waandishi wa habari.

Akijibu swali kuhusu lawama kuwa serikali imeleta askari wengi vituoni, Shamsi ambaye ni Waziri Kiongozi mstaafu na pia amewahi kushika nafasi ya Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa alisema vyombo hivyo vinafanyakazi wakati wote si wakati wa uchaguzi tu na viko kuhakikisha ulinzi wa wananchi na mali zao.

Leo asubuhi Maalim Seif Sharif Hamad alitangaza ‘matokeo’ ya uchaguzi mkuu kinyume na sheria ambapo alijitangaza mshindi wa nafasi ya urais.

“Hoja ya msingi hapa yupo mtu amefanyakazi kinyume na Katiba na Sheria.Tumekuja kukumbushia wajibu wa kufuata Katiba na Sheria, tunataka muielimishe jamii kuwa kitendo cha Maalim kujitangazia ushindi ni cha uvunjifu wa Katiba na Sheria” Alieleza Mheshimiwa Haji Omar Heri.
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top